MHE. INNOCENT L. BASHUNGWA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, ninawashukuru. Barabara ya kutoka Omugakorongo – Kituntu – Rwambaizi – Igurwa – Murongo ipo katika Ilani ya Chama Cha Mapinduzi, imekuwa kwenye manunuzi kwa muda mrefu, ni barabara muhimu kwani inaunganisha nchi yetu na nchi za Afrika Mashariki; na kujengwa kwa kiwango cha lami kutainua uchumi wa Kagera pamoja na Taifa letu. Je, ni lini barabara hii itajengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, ninaomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba barabara hii ni kati ya zile barabara zetu kuu, inaunganisha Uganda na Tanzania kupitia Daraja la Murongo. Mheshimiwa Mbunge atakubaliana nami kwamba hii barabara ilikuwa imetangazwa na tulipata mkandarasi, lakini tukashindwana naye kimkataba. Hivyo, hii barabara imetangazwa tena, iko kwenye hatua za manunuzi kuanza kuijenga kwa kiwango cha lami. Tunaanzia Murongo kuja Omugakorongo. Ahsante. (Makofi)
MHE. EDIBILY K. KINYOMA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi niulize swali la nyongeza. Je, ni lini Serikali itaanza kujenga Barabara ya Uvinza – Kasulu kwa kiwango cha lami, ikizingatiwa ni ahadi ya Mheshimiwa Rais?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Ni kweli Barabara ya Uvinza kwenda Kasulu ina kama kilometa 60 hadi 62. Tumeshakamilisha usanifu. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba ahadi ya Mheshimiwa Rais ni kipaumbele. Sisi kama Wizara ya Ujenzi na TANROADS tumeichukulia hii barabara kwa kipaumbele kikubwa sana, kwa sababu ndiyo barabara ambayo inatoka Tunduma – Sumbawanga – Mpanda – Uvinza – Kasulu – Kibondo hadi Nyakanazi.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ninavyoongea sasa hivi, hicho kipande ndicho pekee ambacho kitakuwa kimebaki hakijajengwa kwa kiwango cha lami. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kuwa Serikali inatafuta fedha ili kuhakikisha kwamba hicho kipande tumekikamilisha ili tuweze kukamilisha hiyo barabara yote ambayo ni T9.