Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Dr. Yahaya Esmail Nawanda (3 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027
MHE. DKT. YAHYA E. NAWANDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Awali ya yote, ninachukua nafasi hii kwanza kumshukuru Mwenyezi Mungu. Pili, ninachukua nafasi hii kumshukuru Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kazi kubwa ambayo anaifanya, hasa katika kuiendesha nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika nishati ninaweza kusema katika Mkoa wetu wa Mtwara tayari vijiji 785 vyote vina umeme. Sasa hivi vitongoji 2,798, kati ya vitongoji 3,421 tayari vimeshapata umeme na kazi inayoendelea ni kupeleka umeme katika vitongoji 555. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya pongezi hizo, ninapenda kujikita katika mambo machache. Mheshimiwa Profesa Muhongo, mwalimu wangu, ameongea kuhusu data na nitajitahidi kidogo kuzungumzia mambo mawili, matatu ya Mkoa wa Lindi na Mtwara. Jambo la kwanza ni suala la Gridi ya Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika nchi yetu leo tuna miaka zaidi ya 65, lakini Mkoa wa Lindi na Mtwara haujaunganishwa na Gridi ya Taifa. Sisi Lindi na Mtwara kwa Miradi ya SONGAS, ambayo wakati inafanya kazi ilikuwa inazalisha zaidi ya megawatt 180 mpaka 190, lakini pia, gesi asilia inatoka Mtwara na hizo zote zinachangia katika Gridi ya Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatukatai matumizi ya rasilimali za nchi hii ni ya watu wote, lakini mpaka leo Mheshimiwa Waziri atakapokuja kuhitimisha bajeti yake kesho, ninaomba alete majawabu kwa wananchi wa Mkoa wa Lindi na Mtwara. Ni lini wataunganishwa na Gridi ya Taifa, ambayo katika mikoa yote sasa hivi tumebaki sisi Lindi na Mtwara? Yaani wote wameunganishwa, bado sisi Lindi na Mtwara. Halafu sisi ndiyo tunatoa gesi nyingi, ambayo pia, inachangia katika Gridi yetu ya Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatukatai gesi ni rasilimali ya nchi yote, lakini sisi ambao tuna gesi ni muhimu pia, kupata vipaumbele hivyo. Kwa hiyo, sisi tunajua kuna mkandarasi anayejenga line kubwa, ambayo inatoa umeme kutoka Songea mpaka Masasi anaidai Serikali zaidi ya shilingi bilioni 53. Ninaomba Mheshimiwa Waziri aje na majawabu ya lini sasa mkandarasi yule alitoka site? Je, kama yupo, tayari ameanza kazi? Kama hajaanza kazi, Mheshimiwa Waziri ni rafiki yangu, nitashikilia shilingi yake na shemeji yangu yupo pale ili anipe majawabu ya Lindi na Mtwara, lini sasa mradi mkubwa huu na hii mikoa miwili itaunganishwa katika Gridi ya Taifa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikizungumzia kwenye REA, hesabu ni rahisi sana. Kwa hesabu ya kawaida, hapa katika Mkoa wa Mtwara kuna vijiji 77 katika huu mpango wa pili, yaani Home let Electrification Project 2B, Mkoa wa Mtwara una vijiji 77, Mkoa wa Lindi una vijiji 159, jumla kuu ukijumlisha hivi vijiji vyote unapata vitongoji 77 na vitongoji vya Lindi 159. In total ukijumlisha unapata vitongoji 555.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeamua tu kuchukua sample. Ukienda Ruvuma wenzetu vitongoji ambavyo vipo katika hii Hepic Two ambayo ni Home let Electrification Project 2B wana jumla ya vitongoji 634, ni zaidi ya vitongoji vyote vya Mtwara na Lindi. Nikachukua hesabu nyingine, Mkoa wa Mwanza wao wana jumla ya vitongoji 634, lakini jumla kuu ya Mtwara na Lindi ni vitongoji 555.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba Waziri atakapokuja kuhitimisha bajeti yake aje na mpango kabambe wa kuongeza vitongoji katika Mikoa ya Lindi na Mtwara, ili atuongezee tufikie vitongoji 700 ambapo sasa tutakuwa na 350 Lindi na 350 Mtwara, tutakuwa tumefanya kazi kubwa na tumepiga hatua kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukizungumza Mradi wa Dharura wa Masasi - Newala. Nichukue nafasi hii kumshukuru sana Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa hakika, mwaka huu tulikuwa na RCC, nilizungumza kuhusu shida ya umeme katika Jimbo la Newala na Mkoa mzima wa Mtwara. Mtwara unakatika umeme zaidi ya mara 20, leo Waziri alinipigia aliniambia siyo mara 20 nipunguze kidogo, lakini nikamwambia twende Newala tukakae mimi na yeye, akaniambia ni kweli unakatika sana, lakini hakutaka kukubaliana na mimi zaidi ya mara 20.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba niseme, baada ya kelele zangu, kumbe Waheshimiwa Wabunge kupiga kelele inasaidia. Mheshimiwa Rais alisikia akaidhinisha 4.6 billion kujenga Mradi wa Dharura kutoka Masasi mpaka Newala. Nichukue nafasi hii, mimi ni mgumu wa kupongeza, lakini nimkupongeze Waziri, pia ninampongeza DG wa TANESCO. Hakika nilimwambia Waziri, asingeweza kukamilisha huu mradi leo hii, kama ningeikamata shilingi yake na mradi huu ukikamilika wananchi wa Newala wanaenda kupata umeme wa uhakika, tena umeme usio na matatizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekuwa tunatumia umeme wa kilometa zaidi ya 1,850 kufika Newala. Maana yake utoke unakotoka Lindi, ufike Mtwara, ufike Nanyamba, ufike Tandahimba, unakuja Newala tayari. Shida ikitokea Nanyamba tayari wananchi wa Newala wanaenda kupata matatizo. Kwa hiyo, Waziri anapokuja kuhitimisha bajeti yako, aje na majawabu atuambie sasa huu mradi wetu wa dharura ambao alisema unakamilika Machi mwaka huu, je utakamilika lini ili wananchi wa Newala waweze kunufaika na mradi huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo pia ningependa kuchangia ni Mradi wa LNG. Mradi wa LNG kila siku umekuwa kwenye maneno tu. Nilikuwa Mkuu wa Wilaya ya Lindi, wakati huo ndiyo gesi inatoka, haitoki, tulipambana sana na Rais Mstaafu Jakaya Kikwete, alitoa shilingi 6,000,000,000 mwaka 2015 kulipa wananchi wa eneo la Likong'o.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiwa DC kipindi hicho na wakatuambia mradi huu utakuja kusainiwa ndani ya miezi minne au mitano ijayo. Ameondoka, amekuja Mheshimiwa Magufuli naye tukaambiwa mradi huu sasa unahitajika ufanyiwe marekebisho, review kubwa inatakiwa kufanyika, lakini tukae mkao wa kula, lakini wale wananchi wa Likong'o tayari tumeshawalipa fidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia amekuja mama yetu kipenzi Dkt. Samia Suluhu Hassan, wanatuambia sasa tuko katika majadiliano ya mwisho. Sisi hatutaki kusikia majadiliano ya mwisho, watuambie wanasaini lini mkataba ule. Maana yake ni nini? Wenzetu wa Msumbiji wana matatizo makubwa sana, tayari wameshakamilisha kusaini, wameshasainiana mikataba ya dola 20,000,000,000 katika Mkoa wa Cabo Delgado, ambayo ni zaidi ya 50,000,000,000,000 katika Mkoa wa Cabo Delgado.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzetu walikuwa na matatizo ya Al-Shabaab na nini na TotalEnergies tayari wameshaanza kazi wanaendelea na kazi pale. Sisi bado maendeleo, sisi mchakato unaendelea, sisi mchakato unaendelea, mchakato unaendelea, wenzetu wa Cabo Delgado, Msumbiji na Mtwara ni baba mmoja, mama mmoja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ningependa Waziri anapokuja kuhitimisha atuambie sasa huu Mradi wa LNG utaanza lini ili na sasa wenzetu wa Msumbiji wakianza kufanya kazi na sisi huku tuanze kufanya kazi ili tuwe na win-win situation.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninataka nikwambie, huu Mradi wa LNG, ninafikiri wananchi wa Mtwara na Lindi hawataki tena kusikia haya maneno wanasaini, wanasema basi tumwachie Mwenyezi Mungu.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. DKT. YAHYA E. NAWANDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kuhitimisha, baada ya kusema hayo, ninaomba kuunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027
MHE. DKT. YAHYA E. NAWANDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu, lakini pia nichukue nafasi hii kumwambia kaka yangu Chongolo sasa ashike peni, nimpe elimu ya korosho kwa dakika saba, halafu niende zangu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, zao la korosho katika Mkoa wa Lindi na Mtwara zaidi ya 85% inazalishwa na wananchi wa Mkoa wa Lindi na Mtwara. Mikoa ya Mtwara na Lindi ina jumla ya wakulima 462,803 na jumla kuu ya wakulima wote nchi nzima ni 549,936. Hoja ya msingi inakuja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mtwara na Lindi ndiyo vinara wa uzalishaji wa korosho nchini. Hoja yangu kubwa hapa leo nitachangia kuhusu bima ya afya. Chongolo kaka yangu katika jambo kubwa ambalo atatusaidia wananchi wa Mtwara na Lindi hususan wanaolima korosho na tukumbuke na zahanati zetu zote tuweke sanamu yake twende na bima ya afya kwa kila mkulima wa korosho na hesabu iko ifuatavyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika zao la korosho mjengeko wa tozo kuna jumla ya fedha shilingi 469. Ushuru shilingi 59, uhifadhi wa korosho, magunia na kila kitu. Leo ninataka nijikite hapa ukisema kwa makisio ya mwaka huu 2026/2027, tunategemea kuzalisha tani 750,000 sawa sawa na kilo milioni 750. Sasa Chongolo kaka yangu katika hizi tozo zote ambazo ni shilingi 469, hapa ninaomba tu tufanye hesabu kidogo, tutoe shilingi tano tano kwa kila mtu hapa na kwa sababu wengine hawa tumekuwa tunawachangia lakini mambo mengine wala hatuyaoni, sasa tukiamua kuchukua hizi fedha tukarudisha kuwapa bima wananchi wote wanaozalisha korosho inawezekana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunawezaje? Twende tukisema kwa makisio ya korosho kilo milioni 750 tukisema tutoe tu shilingi 15 kwenye kila kilo moja tutaenda kutengeneza jumla ya bilioni 11.25 hizi bilioni 11.25 tunaweza kuwahudumia wananchi 75,000 lakini kwenye kitita cha afya ya msingi ambacho mwananchi anaenda kulipa shilingi 150,000 hapa ukijumlisha au ukizidisha mara sita jumla ya wananchi 450,000 wanaenda kunufaika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukisema tunatoa tu shilingi 15 maana yake Lindi yenyewe ina jumla ya population ya wananchi 1,192,000. Kwa hiyo unaweza kusema tukiweza kuwapa bima ya afya wananchi 450,000 maana yake nusu ya watu wote wa Lindi wanaenda kupata huduma ya afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili ni jambo kubwa sana na hapa nimekupa mfano wa Lindi pekee yake. Kwa hiyo, tukiweka na Mtwara tukisema tuweke shilingi 20 tunaenda kuongeza na kupata fedha bilioni 15 ambayo itasaidia wakulima 100,000 tukizidisha mara sita maana yake ni 600,000. Maana yake wakulima wa Lindi na Mtwara 50% ya wananchi wote wanaenda kupata bima ya afya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukisema tuweke shilingi 30 tu Chongolo kaka yangu tunaenda kuongeza au tutapata bilioni 22.5, shilingi bilioni 22 ni sawasawa na wakulima 150,000, ukizidisha mara sita unaenda kupata wakulima 900,000. Wakulima 900,000 ukizidisha mara sita watu wote tunaenda kuhakikisha wananchi wa Lindi na Mtwara wanaenda kupata bima ya afya. Ukisema sasa umalize kabisa chukua shilingi 40 na huu katika mjengeko hatuongezi hata shilingi moja kwa mkulima. Tunachofanya ni kupunguza tozo ambazo tayari tunazo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiweka shilingi 40 tunaenda kupata shilingi 30,000,000,000 ambayo jumla ya wananchi 1,200,000 wanaenda kunufaika. Kwa hiyo, hapo hatujamwingilia dada yetu katika zao lake la COPRA, dada yetu Irene, sisi tumejikita kwenye korosho peke yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukienda kwa Irene dada yetu wa COPRA anaweza kutupa jumla ya wakulima, tukiweka kwenye hesabu hiyo kwa sababu ya projection yake ni kilo 98,000,000 za ufuta, pekee yake tunaenda kusaidia wakulima 58,000 wa Mkoa wa Lindi na Mtwara. Hii ni idadi kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ninachomwomba Mheshimiwa Waziri aje na mkakati wa kuhakikisha sasa tuweze kuwasaidia wananchi wa Mkoa wa Lindi na Mtwara, tuwape bima ya afya bure na inawezekana ndiyo ndoto ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan. Hapa nimempa hesabu na inawezekana. Kwa hiyo Waziru anapokuja kwenye majumuisho aje atuambie sasa tumekubaliana tutakwenda kuendeleza jambo hili zuri la Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa wananchi wa Mkoa wa Lindi na Mtwara. Kwa kufanya hivyo atawasaidia hawa wananchi na hatutamsahau na namhakikishia tutamjengea sanamu katika zahanati zetu zote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine na la msingi ambalo pia ningependa kuchangia ni kuhusu suala la korosho. Korosho tunapopeleka ghalani tumekubaliana mikoa yote inayolima korosho; minada inafanyika siku ya Ijumaa. Siku ya Ijumaa ikifanyika minada watu wote hatutaki korosho hela siku hiyo. Ijumaa sisi hatutaki fedha zetu, Jumamosi hatutaki fedha zetu, Jumapili hatutaki fedha zetu lakini Jumatatu na Jumanne tunataka fedha zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna minada ilifanyika ilichukua zaidi ya miezi miwili bila kulipa fedha. Sasa Mheshimiwa Chongolo akija hapa aje na majawabu hayo, majawabu makubwa ya bima ya afya, lakini pia kero ya wananchi kukaa muda mrefu bila kulipwa fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuseme ukweli COPRA inafanya kazi mzuri sana kwenye ufuta, kwenye mbaazi na kwenye mazao mengine na kwa sababu dada Irene ana miaka miwili tu, bado ni mchanga, ninafikiri baada ya miaka mitano na yeye atakuwa mbobezi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, ninaunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu Mwaka wa Fedha 2026/2027
MHE. DKT. YAHYA E. NAWANDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kumshukuru sana Mwenyezi Mungu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia, nichukue nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa ambayo anaifanya. Katika jambo kubwa Mheshimiwa Rais amelifanya ni kumchagua Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba kuwa Waziri Mkuu, na pia kuwa Msimamizi Mkuu wa TAMISEMI. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, TAMISEMI ndiyo roho ya nchi yetu. Tukizungumza kuhusu TAMISEMI karibia 20% ya bajeti yetu inakwenda TAMISEMI. Kwa hiyo, tukiwa na kiongozi shupavu kama Mheshimiwa Dkt. Lameck Nchemba tunaenda kufanya mapinduzi makubwa katika TAMISEMI. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nimeshawahi kufanya kazi na Mheshimiwa Mwigulu. Yeye ni mtu ambaye anapenda matokeo, na pia ni mtu muungwa na hapendi ubadhirifu, na vile vile ni mtu ambaye anapenda wananchi wake. Kwa hiyo, ninaweza kusema Wizara ya TAMISEMI imempata mtu shupavu na kwa hakika ninaona TAMISEMI inaenda kubadilika sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, ninaomba nijikite katika hoja tatu, au nne. Kwanza ni barabara. Wabunge wote wamezungumza kuhusu ubovu wa barabara zetu. Katika Wilaya ya Newala sisi tuna jumla ya network ya barabara kilometa 966, na hizi zote zinahudumiwa chini ya TARURA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hizi barabara zetu tunategemea kupata fedha nyingi kutoka Road Board au Road Fund. Katika fedha za Road Fund Wabunge wote wamezungumza, kila Mbunge hapa anazungumza kuhusu kuongeza fedha, lakini pia barabara zetu nyingi zimeharibika sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia katika Jimbo langu la Newala Vijijini, Barabara kutoka Mkoma Moja hadi Mnyame haipitiki kabisa. Pia, Barabara kutoka Chiwonga – Pacha Nne mpaka Nambali – Mkongi haipitiki. Pia, ukiangalia Barabara ya Maputi – Chilangala mpaka Ndanda pia haipitiki. Pia, hata barabara kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu, kwa sababu mimi ni Mbunge mkazi wa Iramba, barabara ya kutoka Mtoa – Mtekente – Ndago nayo ina changamoto pia kwa sababu ya mvua kubwa ambayo imetokea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ningeiomba Wizara na Mheshimiwa Waziri Mkuu, akija basi tuletee majawabu ya barabara zetu namna gani tunaenda kuziimarisha ili ziweze kupitika mwaka mzima na kurudisha taswira ya barabara hizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, ninaomba nijikite katika kilimo. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa aliyoifanya hasa katika kukuza zao la korosho. Wakati anaingia, korosho tulikuwa tunapata tani 100,000 sasa hivi tunakwenda mpaka tani 600,000. Haya ni mapinduzi makubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika jimbo langu kwa mwaka huu 2026/2027 pembejeo ambazo Mheshimiwa Dkt. Samia anakuja kutuletea ni zaidi ya shilingi bilioni 27 ambazo zinaenda kuhudumia hekta zaidi ya 200,000. Kwenye zao la korosho ningeweza kushauri yafuatayo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ije na mpango mzuri wa kuhakikisha tunaongeza ruzuku ya pembejeo ili kila mwananchi ambaye anaweza kulima aweze kuongeza tija. Pia, Serikali imekuwa inatoa pembejeo ya sulphur, na dawa za maji. Ningependa kuishauri Serikali, sasa iongeze viuatilifu au dawa za kuuia magugu (weeder). Hii itasaidia sana kuongeza uzalishaji na hata yale mashamba ya zamani tunaweza kuyaongezea tija na kuongeza uzalishaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Serikali inaweza kuongeza fedha za kigeni, lakini pia kwa wananchi wataongeza uzalishaji, na fedha za export levy zitaongezeka kwa sababu mashamba mengi ya wananchi yatakuwa yamelimwa kwa wakati, pia tutaongeza uzalishaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia, ningependa kujikita katika suala la maji. Tunamshukuru Mheshimiwa Rais, wilaya yetu na katika mradi kwa bajeti ya Mheshimiwa Waziri Mkuu page number 69 amezungumza, katika miradi ambayo inaenda kunufaika na fedha nyingi ni Mradi wa Makonde, ambao unatoka katika Jimbo la Newala.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais ameleta jumla ya fedha za mradi ule shilingi bilioni 84. Ningependa kumwomba Mheshimiwa Waziri Mkuu, ule Mradi mpaka sasa hivi Mkandarasi amepewa fedha shilingi bilioni 18 pekee yake na asilimia imefika 46%. Ule Mradi ulikuwa unatakiwa ukamilike tarehe 30 Machi, lakini mpaka leo mradi ule bado unasuasua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamwomba Mheshimiwa Waziri Mkuu, ule Mradi wa Maji wa Makonde unaenda kuhudumia Wilaya ya Newala, Wilaya ya Tandahimba, na Wilaya ya Mtwara, majimbo zaidi ya saba. Asilimia zaidi ya 45 ya wananchi wa Mkoa wa Mtwara wanaenda kunufaika na ule mradi wa maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kukamilika kwa mradi ule unaenda kusaidia sana wananchi wa wilaya hizi nilizozitaja hasa Majimbo ya Newala Mjini, Newala Vijijini, Tandahimba, Lulindi, Nanyamba, na Mtwara Vijijini. Hawa wote wanategemea huo mradi mzuri wa Makonde. Kwa hiyo, ningependa kuishauri Serikali tumalize huu mradi kwa wakati ili wananchi waweze kupata maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia, nichukue nafasi hii kumshukuru sana kaka yangu Mheshimiwa Aweso. Huu mradi ulikuwa ni jitihada zake, alienda kumwomba Mheshimiwa Rais na akatukabidhi huo mradi. Kwa hakika Mwenyezi Mungu ambariki sana na sisi tunamwombea heri na mwisho wa siku huu mradi ukikamilika, mambo yanaenda kukamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye vituo vya afya, Serikali imefanya kazi kubwa ya kujenga vituo vya afya vingi sana, lakini katika Jimbo la Newala Vijijini tuna vituo vitatu vimekamilika. Pia, tunaiomba Serikali, kukamilika tu kwa jengo, tungependa kuweka vifaa pia katika vituo hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Vituo vya Mkwedu, Nandwahi, na Kituo cha Malatu, hivi vituo vimekamilika. Kwa hiyo, tungependa sana hivi vituo pia vipate ambulance, na pia vifaa ambavyo vingeweza kusaidia kufanya kazi kwa ufanisi. Pia, Vituo vya Mtunguru, Mdimba Mpelepele, pamoja na Mikumbi, hivi vipo katika pipeline; na katika bajeti ningeomba Serikali pia iweze kusaidia na kukamilisha vituo hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, ningeweza kuleta mawazo kidogo katika migogoro ya wananchi. Serikali inafanya vizuri sana katika kuhakikisha migogoro hii inakwisha. Tunaisadia Serikali yetu kuhakikisha tunajikita zaidi katika kupunguza kero za wananchi. Waheshimiwa Wakuu wa Mikoa, na Wakuu wa Wilaya wanafanya kazi nzuri sana, lakini pia mimi ningeweza kushauri kuwe na institutional framework, ili kama mgogoro katika ngazi ya wilaya unahusu afya au ardhi, basi Afisa Ardhi, Mwanasheria wa Halmashauri, au Kilimo na hao watu watatue huo mgogoro. Kuwe na institution framework. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakumbuka nilivyokuwa DC Iramba nilikwenda Shelui kutatua mgogoro ambao tayari Mzee Chiligati miaka 35 nyuma alishautatua. Kwa hiyo, bila institution framework tutakuwa hatufanyi ile kazi ya kuwasaidia wananchi ambayo kwa hakika tumeona kazi kubwa ambayo Waziri Mkuu, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu anaifanya, na mwisho tutaendelea kuwalaumu tu Wakuu wa Mikoa na tutaendelea kuwalaumu Wakuu wa Wilaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwajengea nguvu kubwa tutengeneze institution framework ambayo itawasaidia wao pia katika kuhakikisha hizi kazi zinafanyika, na migogoro inaratibiwa na hata akija kiongozi mwingine mgeni, basi anajua kama katika kijiji fulani mgogoro umetatuliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, ninaunga mkono hoja, ahsante. (Makofi)