Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Mwanahamis Athumani Munkunda (2 total)

MHE. MWANAHAMISI A. MUNKUNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaipongeza Serikali kwa majibu mazuri, na kwa kuwa imekiri kwamba Mkoa wa Shinyanga ni mkoa wa kimkakati katika masuala ya uchimbaji ya madini, je, haioni haja sasa Serikali kuanzisha kozi maalum au taasusi maalum kwenye Chuo chetu cha VETA cha Mkoa wa Shinyanga; kama Kozi ya Teknolojia ya Maabara, Kozi ya Jiolojia ya Msingi (Basic Geographical Survey), na Kozi ya Usindikaji wa Madini (Mineral Processing), kwa kuwa kina uwezo wa kuchukua kozi hizi ili kuwarahisishia kazi wachimbaji wadogo walioko Mkoa wa Shinyanga?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali pili, ni kweli kabisa Serikali imefanya kazi kubwa katika kuanzisha hivi vituo vya umahiri; center of excellence. Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa kituo cha umahiri katika eneo letu la wachimbaji wadogo pale Mwakitolyo Halmashauri ya Shinyanga?
NAIBU WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza ninampongeza Mheshimiwa Mwanahamisi Athumani kwa maswali yake haya mawili mazuri. Pia nitambue uzoefu wake katika sekta yetu ya madini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi katika swali lake la kwanza la taaluma ambazo zitatolewa katika hivi vituo vya mfano, au vyuo ambavyo tumevianzisha, ni kweli katika vituo ambavyo tumevianzisha hadi sasa kama kile cha Katente, Luamgasa, na Itumbi zilizoko katika Mkoa wa Geita na Chunya, wale wachimbaji wadogo wanapewa mafunzo ya uchakataji mahiri wa madini kwa kutumia teknolojia rahisi na za kisasa pia ambazo ni rafiki kwa mazingira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuanzisha chuo chochote cha uchakataji madini au kituo cha mfano, mahitaji mahususi ya walengwa yanazingatiwa. Katika masuala geographical survey au katika utambuzi wa miamba na kila aina ya taaluma ambayo inahitajika kwa jinsi wahitaji wa kile kituo watakavyokuwa wamejipanga, yatazingatiwa na Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa swali lake la pili, vituo hivi vya umahiri ambavyo tumevianzisha nimetaja kwamba kuna cha Katente, kiko Bukombe, kuna cha Luamugasa ambacho kipo Wilaya ya Geita na Chaitumbi ambacho kiko Wilaya ya Chunya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hiki cha Mwakitolya ambacho kinakwenda kujengwa na Shirika la STAMICO ambaye ndiyo mlezi wa wachimbaji wadogo nchini, kitakapojengwa, kitazingatia maslahi na mahitaji ya wananchi wa eneo hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mpango wa Serikali kupitia Shirika la STAMICO ni kuanza ujenzi wake katika mwaka ujao wa fedha kwa sababu hii pia ilikuwa ni ahadi ya Rais alipofanya ziara katika Mkoa wa Shinyanga mwezi Disemba mwaka 2025.
MHE. MWANAHAMISI A. MUNKUNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa, ninaipongeza sana Serikali hasa Wizara ya Madini kwa kuendelea kufanya vizuri hasa kwa wachimbaji wadogo, na kwa kweli kutujengea CIP kwenye eneo letu la Mwakitolyo, tutakuwa tumewasaidia sana wachimbaji wadogo na hasa wanawake na vijana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na pongezi hizi na jitihada zote ambazo Serikali inafanya ya ujenzi wa CIP ambayo itakuwa na uwezo wa kuchakata tani 120 kwa saa, ni uwekezaji mkubwa. Sasa Serikali haioni haja wachimbaji tunaowazungumzia hapa, ambao ni wachimbaji wadogo, ambao hawana uwezo wa kuzalisha mzigo huu utakaochakatwa kwa siku kwa tani 120; ushauri ni kwamba Serikali ije na CIP ndogo ndogo ili tuweze kuwasaidia wachimbaji wadogo…

MWENYEKITI: Mheshimiwa uliza swali. Umeuliza swali la kwanza. Uliza swali la pili.

MHE. MWANAHAMISI A. MUNKUNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, CIP ambazo ninashauri ni zile ndogo ambazo zitawasaidia wachimbaji wadogo tunaowalenga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, Serikali haioni haja sasa, kwa kuwa ujenzi wa vituo hivyo vya umahiri vinahitaji uwekezaji mkubwa, watumie Vyuo vya VETA kama Centre of Excellence kwa sababu vyuo hivyo vya VETA viko kila halmashauri ndani ya nchi yetu?
NAIBU WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza ninampongeza Mheshimiwa Mwanahamisi kwa jinsi ambavyo amekuwa mtetezi wa kweli wa wachimbaji wadogo katika masuala ya kusaidia Vituo vya Uchakataji Madini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mwanahamisi, hata mwezi haujaisha aliuliza swali ambalo limekaribia kufanana na hili, na nimelijibu hapa hapa, lakini kwa maswali yake haya mawili ya nyongeza, moja ni ushauri. Ushauri wake kwamba hiki kituo kinachochakata tani 120 kwa siku siyo kwa saa, huenda hakitatoa huduma kwa wachimbaji wadogo ambao hawawezi kuleta mzigo wa kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwondoe wasiwasi Mheshimiwa Mwanahamisi kwamba vituo hivi vinajengwa na Taasisi ya Serikali na haimkatalii mtu yeyote mchimbaji mdogo mzigo wowote anaoleta ili asaidiwe kuchakata. Dhamira ya kweli ya Serikali siyo tu kuwachakatia madini yao, ni kutumia vituo hivyo kuwapa mafunzo ili wale ambao wataweza kufikia vigezo na wakawa na mitaji inayoridhisha, wakaanzisha vya kwao hata vidogo vidogo. Ushauri wake tunaupokea kwamba Serikali iendelee kusaidia utengenezaji wa CIP ndogo ndogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami pia ninatoa wito kwa wachimbaji wadogo ambao wanaokuja kwenye vituo vyetu kujifunza, wachukue teknolojia wakazalishe vituo vidogo vidogo vya CIP. Ninawapongeza wale wote ambao wameshajifunza pale na wameanzisha maana wako wengi kabisa katika kila mkoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili kuhusu kutumia VETA zetu kama mbadala wa maeneo ya kutolea haya mafunzo na kuanzisha CIP katika maeneo ya wachimbaji madini, huu ushauri ni mzuri sana, ninampongeza kwa kuishauri Serikali. Hivyo na sisi tutapenda pia kuupokea huo ushauri na kuona namna zile VETA zilizoko katika maeneo ya wachimbaji zinavyoweza kuingiza somo la kujenga mitambo ya kusaidia uchakataji. Pale pale wanafunzi wetu wanaosoma kwenye vyuo hivyo wapate hiyo taaluma, na baadaye nao wakawe wachimbaji wanaojua kufanya kazi hizo.