Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Dr. Regina Christopher Malima (2 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027
MHE. DKT. REGINA C. MALIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nikushukuru kwa kunipatia nafasi ili niweze kuchangia hotuba muhimu sana katika Wizara ya Elimu na Teknolojia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue fursa hii kwanza kabisa kupongeza wasilisho ambalo limefanywa na Mheshimiwa Waziri. Hongera sana kwa Mheshimiwa Waziri Profesa Mkenda pamoja na Msaidizi wake, Mheshimiwa Wanu na timu yote ya wataalam katika Wizara hii. Zaidi ninamshukuru sana Rais, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuleta mageuzi makubwa katika sekta ya elimu nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama kuna uwekezaji mkubwa ambao wananchi wanapaswa kufahamu ambao umefanyika katika sekta ya elimu, basi ni Wizara hii kuchukua jukumu kubwa la kuleta mageuzi katika sekta ya elimu nchini. Mengi yamesemwa na Wabunge wenzangu na sintotaka nirudie sana, lakini niendelee kupongeza juhudi za Wizara hii katika kupanua miundombinu kupitia Mradi wa HEET (Higher Education for Economic Transformation). Mradi huu unatekeleza ujenzi wa campus mpya 16 katika nchi yetu. Hili ni jambo la kupongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo hivyo tu, kuna kozi maalum ya kuwainua wanawake wanaotoka kwenye mazingira au kaya maskini kupitia Mradi huu wa HEET. Mradi huu katika kuendesha programu hii wanashirikiana na Chuo Kikuu Huria cha Tanzania. Mpaka sasa wanafunzi zaidi au vijana zaidi ya 711 wamenufaika na 137 wanatokea Zanzibar, jambo hili ni la kupongeza sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nina hoja mbili tu na kama muda hautaruhusu nitaleta hoja binafsi kwa ajili ya haya ambayo ninataka kuyasema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza kabisa ninatambua Wizara hii ipo katika kupitia Sera ya Elimu ya Mafunzo ya Mwaka 2014, Toleo la 2023 pamoja na mapitio ya sheria na mitaala. Kama tunavyofahamu nchi yetu iko katika changamoto ya mmomonyoko wa maadili, jambo hili linapaswa kuchukuliwa kitaifa, ajenda hii ni ya msingi sana kuitazama katika jicho la kitaifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaiomba tu Wizara hii kupitia wataalam wake pamoja na taasisi nyingine zilizoko chini ya Wizara kuanzishwa rasmi kwa somo la maadili kama somo linalojitegemea katika mfumo wa elimu. Kwa nini ninasema hivyo? Tafiti zinaonyesha kabisa kwamba nchi yetu iko kwenye mmomonyoko mkubwa wa maadili, tunafanya nini kunasua kizazi chetu kutokana na changamoto hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imefanya juhudi kubwa sana katika kutengeneza miundombinu, katika kuboresha mambo muhimu katika sekta ya elimu, lakini haya yote yatakuwa bure kama maadili tuliyonayo katika Taifa hili kwa sasa yataendelea kubaki hivyo. Kwa hiyo, niseme tu kwamba kuna mwenendo wa maadili ambao siyo mzuri katika jamii na tafiti zinaonyesha, lakini pia tunaona nidhamu, vitendo vya rushwa, vitendo vya rushwa hivi haviji kwa bahati mbaya, hivi ni mwendelezo tu wa tabia ambazo yumkini mtu hakupata malezi katika utoto wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, masuala ya uadilifu na uzalendo yote haya yamekosekana katika nchi, elimu bora bila maadili ni bure. Kwa maana hiyo, ninapendekeza katika Wizara hii rasmi tuweke somo la maadili kama somo linalojitegemea. Niombe Wabunge wenzangu waniunge mkono katika hili kwa sababu bila maadili nchi yetu itaendelea kupata shida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeshuhudia vitendo mbalimbali ambavyo Serikali inatengeneza miundombinu, lakini vijana wanaharibu, hili siyo jambo la kufumbia macho. Niombe Wizara ya Profesa Mkenda iliangalie jambo hili kwa umakini na somo hili liwe ni somo la lazima katika ngazi ya elimu ya msingi, awali lakini pia sekondari na hata vyuo lijitegemee, liwe na maudhui maalum ambayo yataonesha namna ambavyo jamii au vijana wetu na jamii kwa ujumla wanaopaswa kuwa na kuna faida nyingi tu katika kuweka somo la maadili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, zipo nchi ambazo zimeendelea sana baada ya kuwa na mifumo kama hii, Profesa Muhongo aliongelea habari ya nchi kama Japan, Singapore, South Korea, kuna Finland. Nchi hizi ni nchi ambazo zimeendelea, wana somo la maadili katika mitaala yao na linajitegemea kwa namna fulani na limeleta heshima kwa hizi nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna mifano Barani Afrika tunayo Nchi ya Rwanda, Nchi ya Rwanda sasa hivi wana somo linaloitwa values and ethics. Pia tuna Nchi ya Kenya wana somo linaitwa life skills education. Tuna Nchi ya South Africa wana somo linaitwa life orientation, Nchi ya Ghana hawa wana somo linaitwa religious and moral education. Yote haya yametengeneza msingi wa maadili katika nchi yao na tumeona namna ambavyo wanapiga hatua katika masuala ya maadili na namna ambavyo vijana wameendelea kuwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nipendekeze somo la maadili liwe ni somo, lazima katika mfumo wetu wa elimu na kuanzia sasa Wizara ijipange tu, nitaleta hoja binafsi kama ambavyo nimesema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni suala la ubora wa elimu. Ubora wa elimu uko katika nyanja mbalimbali, lakini tumeona namna ambavyo Serikali imejipanga au imeboresha miundombinu na mambo kama hayo, lakini bado kuna changamoto kwa wahadhiri au wakufunzi wetu. Wabunge wenzangu walielezea hiyo kwa upana zaidi, lakini niendelee tu kusisitiza, bado tunahitaji motisha kwa wahadhiri na wakufunzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini ninasema hivyo? Hotuba ya Mheshimiwa Waziri imeonyesha namna ambavyo enrollment ya wanafunzi imeongezeka, lakini bado hatuoni namna ya ku-balance workload ya jambo hili. Kwa hiyo, niombe Mheshimiwa Waziri na hili nalo alifanyie kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, niunge hoja hii mkono. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu Mwaka wa Fedha 2026/2027
MHE. DKT. REGINA C. MALIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru kwa kunipatia nafasi ili na mimi niweze kuchangia katika Bunge lako Tukufu. Kwanza kabisa, ninamshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ametuwezesha kuwepo mahali hapa leo tukiwa na majukumu makubwa katika nchi, ili kuweza kuchangia hotuba ya Waziri Mkuu, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee kabisa nichukue fursa hii kwa moyo wa dhati kumpongeza Rais Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa maono makubwa katika Taifa letu na namna ambavyo ameendelea kufanya kazi kwa kugusa maeneo mbalimbali ya maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa, pamoja na yote haya tumeona kuwa amekuwa ni Rais wa kwanza kuhakikisha kabisa Taifa linakuwa na mpango wa maendeleo wa muda mrefu wa mwaka 2050. Hili ni jambo kubwa ambalo Mheshimiwa Rais amelifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninawapongeza watendaji wake wote ambao ni wasaidizi kuanzia Makamu wake wa Rais, Mheshimiwa Nchimbi, pia Mheshimiwa Waziri Mkuu na watendaji wote katika Wizara zote, bila kusahau watendaji katika nafasi mbalimbali za mikoa, wilaya hadi huku chini, na sisi Waheshimiwa Wabunge kwa namna moja au nyingine tumekuwa tukimsaidia Rais kuhakikisha kwamba maono haya yanafikiwa kama ambavyo amepanga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeipitia kwa kina hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, imesheheni data katika kila eneo. Hiki ndicho kinachotakiwa kufanyika tunapokuwa tukitoa taarifa mbalimbali. Kwa maana hiyo, ninampongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu, ameonyesha hili na amegusa maeneo yote. Sekta mbalimbali zimeonekana na namna ambavyo output zinaonekana kwa kila eneo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kuipongeza Serikali ya Awamu ya Sita ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa sababu yeye ndiye anaye-facilitate haya yote kuhakikisha yanafikiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo, nitakuwa na mambo machache ya kuongea. Nitaongea kwenye sekta ya elimu, eneo ambalo pia nimekuwa ni Mbunge mwakilishi wa kundi la vyuo na vyuo vikuu, kwa namna ambavyo nchi imekuwa na mwelekeo katika kuboresha sekta hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, elimu ni msingi wa dira ya mwaka 2050. Sambamba na malengo mengine ya muda mfupi, na hata ya muda wa kati, kwa nini tuboreshe elimu? Ni katika elimu hii ndipo tunapata nguvu kazi yenye ujuzi. Ni katika elimu ndipo tunapata wahitimu mahiri ambao wanaenda kukabiliana na changamoto za karne za 21. Ni katika elimu, endapo itaboreka ndipo tutapunguza suala la umasikini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja hayo, ninapongeza juhudi kubwa ambazo zimefanyika na Serikali. Tumeona mageuzi makubwa katika elimu ya msingi, elimu ya sekondari na elimu ya juu, kwa maana ya vyuo na vyuo vikuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bajeti ya mikopo imeongezeka, miundombinu imeboreshwa, na mambo kama hayo, yamesaidia vijana wetu kusoma katika mazingira ambayo ni rafiki kwa ajili ya masomo yao. Uwekezaji huu ni muhimu ili kujenga Taifa lenye watu wenye ujuzi, lenye watu wenye maarifa na uwezo wa kujitegemea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazo nchi Barani Afrika ambazo zimewekeza katika elimu na wamefika mbali. Kuna nchi ya Rwanda wamewekeza katika elimu ya msingi, na pia katika elimu ya TEHAMA. Hivi sasa tunavyoongea Rwanda inaongoza katika eneo hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile tunayo nchi ya Botswana, wao wametenga fedha inayopatikana kutoka katika sekta ya madini na kuiwekeza kwenye elimu. Mambo kama hayo yanaleta tija kwa sababu elimu inapoboreka ndipo ambapo tunapata wanafunzi au wahitimu mahiri ambao watakuwa na faida katika Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na jitihada zote hizi, kuna changamoto moja ambayo binafsi kama mtaalamu na mtafiti nimeendelea kuiona. Changamoto hii ni kuhusu ubora wa elimu sambamba na ujuzi wa wahitimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, utaona namna ambavyo Wabunge wamekuwa wakichangia na kuona kabisa kwamba kuna changamoto ya ajira, kuna changamoto ya vijana wengi kuwa katika mitaa, na kadhalika na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tafiti zinaonyesha kuna changamoto ya ubora wa elimu na ujuzi wa wahitimu. Eneo hili ni muhimu sasa Serikali iliangalie. Mheshimiwa Rais amefanya mageuzi makubwa sana kwenye miundombinu na kwenye mambo kama hayo, lakini bado eneo la ubora wa elimu ni changamoto katika nchini yetu, sambamba na ujuzi wa wahitimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaiomba Serikali yangu iliangalie eneo hili, na lipo katika maeneo mawili. Tunaposema ubora wa elimu, kuna wanafunzi au wahitimu, lakini pia kuna waalimu au wahazili. Kila mwaka takribani wahitimu 50,000 hadi 70,000 wanahitimu kutoka katika vyuo vikuu. Hapo bado hatujaweka watu au wahitimu wanaotoka kwenye Vyuo vya VETA na kwenye vyuo vya kati. Sasa hawa wote wanatengeneza zaidi ya 50% ya wahitimu wetu kukosa ajira, iwe ni za kujiajiri au zile ajira ambazo ziko katika mfumo rasmi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tujiulize, ni kwa nini vijana wengi wanakosa ajira? Kwa nini vijana wengi wako mtaani? Sasa basi, ni muhimu Serikali kutafuta ufumbuzi katika eneo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaiomba Serikali tuangalie pia wahadhiri au waalimu ambao wamekuwa wanafundisha, hasa katika eneo la vyuo vikuu. Kumekuwa na changamoto. Juzi tulikuwa na ziara katika baadhi ya vyuo vyetu nchini, tumekuta mtu ambaye amepata demotion kwenye taasisi fulani anapelekwa kwenda kufundisha. Hii haikubaliki kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina imani kabisa taasisi hizi zina vigezo vya namna ambavyo zinapaswa kupata wahadhiri au waalimu. Mtu ambaye amepata demotion, anaendaje kufundisha mwanafunzi? Hii haikubaliki kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tuangalie ujuzi wa vitendo au ubunifu wa hawa vijana wetu, namna ambavyo wako katika eneo hilo vizuri. Pia uwiano wa ujuzi na uhitaji wa soko la ajira ukoje? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninaomba Wizara zinazohusika ziliangalie suala hili. Pamoja na uwekezaji mkubwa katika eneo hili, kuna haja ya kuangalia ubora wa elimu, ili tuweze kupata products ambazo zitakuwa ni nzuri za kuweza kuajirika na pia kujiajiri wenyewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nisemee upande wa wahadhiri. Mheshimiwa Waziri wa Elimu yuko hapa ananisikia. Kuna changamoto moja ambayo wahadhiri wamekuwa wanakutana nayo. Tuna vyuo vikuu ambavyo viko chini ya TCU, pia kuna taasisi nyingine ambazo ziko chini ya NACTVET.

Mheshimiwa Mwenyekiti, upande wa TCU retirement age ni miaka 65, lakini upande wa NACTVET retirement age ni miaka 60. Sasa nimekuwa nikifanya ziara mbalimbali kuonana na wadau hawa. Wengi wanaomba retirement age iwe sawa, TCU pamoja na NACTVECT, kwa maana ya miaka 65 kwa wote wanaofundisha katika hizi taasi zetu. Hiyo itasaidia kuendelea ku-maintain wahadhiri ambao wana uzoefu ili waweze pia kuendelea kutoa huduma hiyo kwa wanafunzi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna jambo lingine amblo ninataka niliongelee, ni kuhusiana na vyuo vyetu vya kati. Mheshimiwa Rais amewekeza sana, hadi sasa tuna vyuo vya VETA takribani nchi nzima, lakini vyuo hivi bado havina programs ambazo zinahusu eneo husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikitoa mfano, kule ninakotokea mimi, Wilaya ya Ukerewe tuna Chuo cha VETA. Katika chuo hiki 99% ya watu wa Ukerewe tuna-depend kwenye uvuvi, lakini cha kushangaza Chuo hiki cha VETA hakina program yoyote ambayo inahusiana na masuala ya uvuvi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekuwa tukilipigia kelele jambo hili. Vyuo hivi mahali vilipo viendelee kutoa programs ambazo zitawanufaisha wale walengwa au wanaokaa maeneo husika. Nina imani kabisa kuwa ushauri huu utafanyiwa kazi ili tuweze kuwa na wanufaika wanaotoka katika maeneo husika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna eneo moja ambalo nitaomba niligusie kidogo kuhusu ajira kwa vijana. Tumeona kabisa kila Mbunge anapiga kelele kuhusu ajira, lakini uwekezaji mkubwa umefanyika. Ninaomba coordination ya miradi mbalimbali ya vijana ambayo Mheshimiwa Rais ametenga iweze kufanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo hivyo tu, na ufuatiliaji. Tumeona mambo ya ufuatiliaji yakiwa raised na watu, na Waheshimiwa Wabunge mbalimbali hapa. Kwa hiyo, ninaomba Bunge lako Tukufu liweze kuhakikisha huduma hizi zinapatikana kwa vijana na kuondoa changamoto kubwa ya vijana ambayo inaonekana kuwa tatizo kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru sana ninaunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)