Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Kassimu Amari Mbaraka (3 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027
MHE. KASSIMU A. MBARAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, shukrani sana kwa kupata fursa hii ya kuchangia katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa siku hii ya leo. Jambo kubwa la msingi zaidi, ninamshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kutujaalia sote kuwepo hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninawapongeza Waheshimiwa Wabunge wote kwa michango yao mizuri waliyoiwasilisha hapa Bungeni kwenye hotuba hii ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, michango yenye kujenga, kuonyesha mwelekezo na kutoa njia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuchangia kuna machache ambayo nimeyaona nikasema nichangie ili hatimaye niweze kuunga mkono hoja juu ya hotuba hii. Jambo la kwanza ni kuhusiana na mikopo ya 10%. Kwanza tuipongeze Serikali kwa kutoa mikopo hii kwa muda mrefu sana ya 10% kwa makundi ya vijana, akina mama na walemavu. Ni jambo kubwa na jambo zuri sana. Tukiangalia kwa muhtasari na muktadha tulionao sasa na kule tunakokwenda, tunahitaji kufikiria upya suala hili la mikopo ya 10%, hususan kwa kundi la vijana (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa muda mrefu sana vijana wamekuwa wakipata asilimia nne kwenye mikopo hii ya 10%. Sasa, tunatakiwa tubadili fikra kwa kule tunakokwenda. Idadi ya vijana sasa hivi ndani ya nchi yetu ni kati ya 60% hadi 70%. Ukiangalia katika taasisi mbalimbali za fedha utabaini kuwa kuna programu nyingi sana za uwezeshaji za mikopo ya akina mama, au tuseme wanawake; lakini kundi hili la vijana limeachwa nyuma kwa namna moja ama nyingine, liko kwenye mikopo hii ya 10% ambao wanaambulia asilimia nne. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa, ninaomba tubadili fikra na mtazamo kwa kushauri kwamba, tuanze kufikiria kuwa na Benki ya Maendeleo ya Vijana ndani ya Taifa hili la Tanzania. Vijana hawa 60% hadi 70%, ambayo ndiyo idadi ya population ya Tanzania ni muhimu sana kuwalea, kuwajengea uwezo kwa sababu hawa ndiyo mabilionea na wawekezaji wa kesho ndani ya Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa harahaharaka ukiangalia utaona kuna takribani milioni moja ya vijana au tunazungumzia rural-urban migration. Kila mwaka nguvu kazi inatoka vijijini inakuja mjini, lakini wakati huo huo kuna wanaohitimu shuleni na ambao wamefikia umri wa kuajiriwa takribani nao milioni moja. Yaani wako tayari kuingia kwenye soko la ajira. Hawa wote tunawapeleka wapi? Hatuwezi kuwaajiri wote, lazima tuwe na benki itakayowalea. Isiwe benki kama benki zilivyo za sasa hivi, iwe benki ya ulezi katika kusimamia startups za hawa vijana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitatoa mfano mdogo, kijana ana andiko mradi zuri, ana wazo zuri, anapokwenda kwenye financial institution yoyote leo hii atahitajika collateral. Amehitimu chuo huyu kijana, hana collateral yoyote ataweza kuanzia wapi? Jambo kubwa na la msingi zaidi linalohitajika kufikiriwa upya, benki hiyo ianzishwe, ikishaanzishwa ifanye kazi ya kushirikiana na hawa vijana katika ufanyaji wa biashara. Haya yatasaidia vijana na itaweza kuwajengea uwezo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesikia pia suala zima la matumizi ya vyeti wanapohitimu, viweze kutumika kuweza kuwapatia fedha. Sasa, idadi kubwa hii ya vijana tusipoitengenezea mazingira mazuri leo, kesho yao itakuwa ngumu na inaweza ikawa bomu la Taifa. Kwa hiyo ninaomba sana, katika hoja hizi zilizotolewa, ushauri wangu Serikali ianze kufikiria upya sasa kuleta Benki ya Maendeleo ya Vijana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuanzisha Wizara ya Vijana. Wizara hii ya Vijana imeanzishwa imetengewa takribani shilingi bilioni 200 ziko pale. Leo tungekuwa na benki ya maendeleo ya vijana fedha hizi zote zingewekwa pale, za kwenye kilimo kama kuna zinazowahusu vijana zingewekwa pale, asilimia nne za halmashauri zingewekwa kwenye Benki ya Maendeleo ya Vijana. Hatimaye vijana wa Taifa hili wakanufaika na wakaweza kujiajiri na kuja kutengeneza ajira nyingi kwa hapo baadaye. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nukta nyingine ya msingi ninayotaka kuchangia ni kuhusiana na suala zima la sekta binafsi. Sekta binafsi imekuwa ikifanya vizuri sana ndani ya nchi yetu na imekuwa ikichangia sana maendeleo ya nchi yetu na pato letu la Taifa, lakini yapo mambo ya msingi ambayo tunahitaji kuyaangalia kwa upana na kwa sura ambayo ni nzuri zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kwa kiwango gani Watanzania wanaofanya kwenye sekta binafsi wananufaika, ambapo kundi kubwa bado ukienda huko ni vijana? Tarehe 13 Oktoba, 2025 Wizara ya Utumishi wa Umma ilitoa tangazo la kuongezeka kwa kima cha mshahara katika sekta binafsi, lakini ukiangalia kwa harakaharaka ukifuatilia mchanganuo uliowekwa kwenye lile Gazeti la Serikali, tangazo lile lililosainiwa na Mheshimiwa Waziri wa Utumishi wa Umma, ukipitia na ukiangalia hali halisi ilivyo huoni utekelezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niishauri Serikali, sekta binafsi wakati inakua na maisha ya watu wanaofanya kazi ndani ya sekta binafsi, basi tuhakikishe nayo yanakua na mishahara ile iliyotangazwa kuongezeka ifuatiliwe iongezeke. Nitatoa mfano katika hili; Bandari ya Tanga kumefanyika uwekezaji mkubwa takribani shilingi bilioni 423, lakini kwa muda wa miaka 10 vibarua walioajiriwa pale kuna kampuni zimechukua tender ndani ya TPA (Tanzania Ports Authority).

Mheshimiwa Mwenyekiti, zile kampuni baada ya kuchukua tender kwa muda wa miaka 10, vijana wale wanalipwa kati ya shilingi 9,500 mpaka 11,000 na wapo vijana takribani 17,000. Tangazo la Serikali limetoka, TPA inazilipa zile kampuni vizuri kabisa, wale watu wanachelewesha mishahara kwa wale vijana, lakini mwisho wa siku kilichokuwepo ni kwamba mpaka leo wale vijana bado hawajaongezewa mishahara wala hawajaongezewa ujira wao kwenye vibarua. Hii ni changamoto wakati maelekezo ya Serikali yametoka na yametolewa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mawaziri wetu wanafanya kazi kubwa nzuri sana. Katika hili ninaomba waamke, wapite kwenye viwanda na kwenye sekta mbalimbali za binafsi waangalie maelekezo yaliyotolewa kutoka kwa Waziri wa Utumishi wa Umma, je, yanatekelezeka ili hali za maisha ya wananchi wetu yazidi kustawi na kuboreka? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nukta nyingine ya msingi ninayotaka kuchangia ni sehemu ya uvuvi. Niipongeze Serikali kwa kutoa boti na kuwasaidia wavuvi hususan watu wa ukanda wa bahari na sehemu ya maziwa; wanafanya kazi nzuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, ninataka niliambie Bunge hili Tukufu, zaidi ya 80% ya uvuvi wa Tanzania ni traditional. Boti zilizopelekwa kule ni modern: boti zimepelekwa zina rangi nyeupe, wavuvi wanaenda kuvua usiku baharini wana karabai zao, kunatokea reflection ya light samaki wanatawanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi watu wa Pwani, unapoenda kuvua basi unapaka lile dau lako au mashua yako inaitwa sifa, iwe na rangi nyeusi kama rangi ya lami ili itengeneze kiza samaki wakusanyike karibu kwenye mwanga ili mwisho wa siku upate samaki wa kutosha ili mambo yaweze kwenda vizuri. Matokeo yake boti zile zimepelekwa, watu wanafukuzana na waliopewa boti kwa ajili ya marejesho, kumbe ukiangalia watu wameshindwa ku-consider point moja kwamba, uvuvi wetu 80% ni traditional, tunawapelekea vifaa ni modern. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashauri katika hili ikiwezekana Wizara husika ikae na wavuvi kwanza iangalie modality kwenye maeneo yao husika ni aina gani ya boti wanazozihitaji kuliko kutumia gharama kubwa ya pesa na kuleta boti ambazo kwa namna moja ama nyingine mwisho wa siku zinakuwa hazina tija kwa wavuvi kulingana na ile sekta ya uvuvi jinsi ilivyo. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. KASSIMU A. MBARAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuzungumza haya, ninaunga mkono hoja. Shukrani sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Katiba na Sheria kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027
MHE. KASSIMU A. MBARAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, shukrani sana. Kwanza kabisa ninamshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kutujalia sote kuwemo humu tena na kuendelea kulitumikia Taifa katika hili Bunge Tukufu, Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, nikushukuru wewe kwa kunipa fursa hii na nafasi hii ya kuweza kuchangia katika suala zima la msingi linalohusiana na masuala ya Wizara ya Katiba na Sheria katika siku hii ya leo. Pia, nitumie fursa hii kumpongeza kwa kiwango cha hali ya juu Mheshimiwa Waziri wa Katiba na Sheria, Naibu wake, wasaidizi wao wote pamoja na Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa kazi kubwa wanayoifanya ndani ya Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sote ni mashahidi na sote tunafahamu na tunaona namna wanavyoratibu mambo na namna yanavyokwenda hususani kuhusiana na kliniki mbalimbali za misaada ya kisheria hususani ile Samia Legal Aid ambayo inafanya kazi vizuri sana kwa kiwango cha hali ya juu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nijikite katika mchango wa msingi kabisa na umuhimu kwenye masuala ya kisheria. Jambo la msingi kubwa zaidi ni kwamba kuna madai mengi sana ambayo yanakuwepo Mahakamani na yanachelewa sana kupatiwa ufumbuzi kwa muda mrefu sana kiasi ambacho yanaathiri miradi mingi sana ya maendeleo katika jamii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, imefika mahali wakati mwingine kama imekuwa sehemu ya Mahakama ya watu kufanya kitu kitaalam, tunakiita technical delaying, yaani kuchelewesha mambo kwa ajili ya faida binafsi au kwa ajili ya maslahi yao binafsi. Nitatoa mfano katika jambo ambalo limetokea katika Jimbo letu la Tanga Mjini. Hapa nitafanya reference kidogo ya land case namba tatu ya mwaka 2021 ndani ya Jimbo la Tanga Mjini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pale pana hospitali ambayo ni binafsi, ilianza kuwa dispensary ikaja mpaka ikafikia hatua ya kuwa hospitali. Inafanya kazi kubwa sana na kusaidia watu wa Tanga, lakini ukatokea mgogoro baina ya wamiliki pamoja na watu ambao ni wawekezaji katika lile eneo. Kesi ile imekwenda mpaka leo ni mwaka 2026 bado haijatoka Mahakamani na shauri lile halijakwisha, imekuwa ikiisha ikikatiwa rufaa, imebakia katika hali hiyo. Nini kilichotokea sasa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kilichotokea...

MWENYEKITI: Mheshimiwa kwa mujibu wa Kanuni zetu kama kuna kesi iko Mahakamani inaendelea, haturuhusiwi kuijadili humu ndani.

MHE. KASSIMU A. MBARAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru kwa kunifahamisha na kunielimisha kwa hilo. Kutokana na hilo naendelea, nukta nyingine ya msingi ya pili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaipongeza Wizara ya Sheria na Katiba kwa kuonesha na kudadavua vizuri sana katika randama yao, hususan, kuonesha suala zima la elimu ya kisheria. Nimeona pale kwamba, kuna mchakato mzima wa kuingiza masuala ya elimu ya kisheria VETA, hali kadhalika mchakato mzima wa kuingiza kwenye mtaala elimu ya kisheria, hususan kwenye Chuo Kikuu cha Mzumbe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya ni mambo ambayo Wizara inayachopeka kule ni ya msingi sana kwa sababu, migogoro yote tunayoiona kwenye jamii inatokana na Watanzania walio wengi sana katika masuala mbalimbali kutokufahamu vizuri sheria za nchi hii, ambalo ni tatizo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hili ninawapongeza sana, wamefanya jambo kubwa sana la kimageuzi na kimabadiliko na liende katika vyuo vyote nchini Tanzania. Kila kijana anayehitimu walau ngazi ya diploma aelewe sheria za msingi za nchi hii, aelewe Katiba ya Nchi yetu, aelewe sheria za mambo ya ardhi na umiliki wa ardhi. Itasaidia sana kutatua migogoro mingi hapo baadaye.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiacha hilo kuna suala la Katiba Mpya. Ninaipongeza sana Wizara ya Katiba na Sheria, jambo hili limekuwa katika Ilani ya Chama cha Mapinduzi ambapo tumelinadi sana Wabunge wote Mwaka 2025 mpaka 2030 katika kipindi hiki. Nimeona tayari mchakato na utaratibu umeanza kupitia Wizara yetu ya Katiba na Sheria kwamba, jambo hili tayari limeshawekwa Mezani na mchakato umeanza kwa kuanza kushirikisha wadau na kuandaliwa taratibu zake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili ninapongeza na ni jambo kubwa sana kwa sababu, mabadiliko ya Katiba ni jambo la kitaifa na linatuhusu sisi sote. Wakati umekwenda sana, muda umesogea, mazingira yamebadilika, jamii tuliyonayo ni changamani sana, tunahitaji zaidi kuliangalia hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninawapongeza walioliweka kwenye ilani, hali kadhalika ninaipongeza Wizara ya Sheria na Katiba, kwa mara nyingine tena, kuliona hili na kuanza kuchukua hatua mapema na kufanyia kazi utekelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa ninachangia kwa kusema, Samia Legal Aid, msaada ule wa kisheria ni jambo kubwa na adhimu sana, linawasaidia watu wengi sana ndani ya Taifa hili. Tumeona kliniki ile ikifanyika, sasa ninashauri msaada ule, wale mawakili 171 wa kujitegemea ambao Wizara ya Katiba na Sheria inawatumia kati ya mawakili wengi wa Serikali walionao, sasa uende magerezani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kule kuna watuhumiwa wengi, wako mahabusu, wasikilizwe na wayasimamie mashauri yao mahakamani, wenye hatia wapate hatia, ambao hawana hatia watoke waungane na ndugu zao. Hii itasaidia sana iwapo Samia Legal Aid itafika magerezani na kusikiliza wafungwa mbalimbali ambao hawana msaada wa kisheria kuweza kuwasaidia katika hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa haya ninasema ninashukuru sana kwa siku ya leo nami kuweka mchango wangu kwenye randama hii ya Wizara, hoja hii ya Wizara ya Katiba na Sheria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa ninaunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027
MHE. KASSIMU A. MBARAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, shukran sana kwa kupata fursa hii nami kuchangia kwenye bajeti hii ya Wizara ya Elimu. Awali ya yote ninamshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema kutujalia kuwepo hapa Bungeni na kuendelea kulitumikia Taifa letu la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika nukta ya pili ninapenda kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayoifanya ndani ya Taifa letu la Tanzania kwenye kuisimamia na kuleta mageuzi makubwa chanya hususan mageuzi ya kielimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona miaka mingi sana tumepita na kauli mbalimbali za elimu, lakini leo ile azma ya kauli kubwa ya Taifa hili ya elimu ya kujitegemea inaenda kutimia kwa kuona mabadiliko makubwa yaliyofanyika kwenye mitaala ya elimu ambayo inawawezesha vijana kuhitimu kidato cha nne akiwa pia amehitimu masomo yanayosimamiwa na NACTVET na kuweza kupata cheti na kuingia kwenye soko la ajira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, atakuwa na ujuzi ndani ya umri mdogo au hata kuendelea katika vyuo vya kati na kuweza kupata elimu. Hili ni jambo kubwa sana kwa sababu soko la dunia ya leo linahitaji watu wenye ujuzi na si nadharia tena. Kwa hiyo, wataweza kushindana katika soko la ajira hapo baadaye. Hilo ni jambo kubwa sana. Tunampongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa hiyo aliyoifanya kuisimamia mageuzi ya mitaala. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri Profesa Adolf Mkenda pamoja na Naibu wake Mheshimiwa Naibu Waziri, Wanu Hafidh Ameir kwa kazi kubwa wanayoifanya kwenye Wizara hii ya Elimu pamoja na watendaji wao Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu na watendaji wote wa Wizara ya Elimu. Kwa kweli wanafanya kazi kubwa sana kuisimamia maono mapana ya Taifa hili pamoja na maono mapana ambayo yamo katika Dira yetu ya 2050 kuhusiana na masuala elimu ndani ya Taifa letu la Tanzania. Ni jambo jema kabisa hilo na mambo yote yanakwenda vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuongea hayo kwa muhtasari sasa nijikite kwenye jambo la msingi. Ukichunguza zaidi utakuja kugundua kwamba Wizara ya Elimu 100% maisha yake inagusa maisha ya vijana wa Taifa la Tanzania na katika Taifa la Tanzania vijana katika population ni takriban 68% hadi 70%.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii tafsiri yake ni nini? Tafsiri yake ni kwamba idadi ya ongezeko la watu inakua Tanzania, lakini ukiacha hivyo idadi ya vyuo vikuu vinaongezeka Tanzania. Maana yake ni nini? Ni lazima tujifunge mkanda vizuri kuhakikisha tunaihudumia vizuri elimu ya juu kupitia Higher Education Students’ Loan Board kwa kuhakikisha mikopo ya vyuo vikuu (elimu ya juu) na ya kati inayotolewa na Higher Education Students’ Loan Board inatoka kikamilifu na bajeti ile inatoka kama vile ilivyopitishwa na kuidhinishwa na Bunge. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitatolea mfano, ukiangalia bajeti ya Mwaka wa Fedha 2023/2024, 2024/2025 na 2025/2026 kuna kitu utakigundua. Bajeti iliyoidhinishwa na Bunge katika jumla ya vipindi hivyo vitatu ni shilingi 2,442,851,755,519.98. Hii ndiyo bajeti iliyoidhinishwa kipindi cha Mwaka wa Fedha 2023/2024, 2024/2025 na 2025/2026. Iliidhinishwa hii iende kwenye Higher Education Students’ Loan Board, ifike pale watoto wale wakopeshwe, vijana wetu waweze kusoma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kiasi kilichopokelewa Loan Board ni shilingi 1,788,017,499,927.58. Hiyo ndiyo fedha ambayo imepokelewa takriban shilingi bilioni 654 na ushee bado haijapokelewa. Tafsiri yake ni nini? Ni kwamba kampasi zinaongezeka, kampasi zinakuwa nyingi zinazidi kutanuliwa, idadi ya enrolment inakua vyuo vikuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maana yake ni kwamba tunaishauri Serikali fedha tunazozipanga hapa Bungeni kuhusiana na Higher Education Student Loan Board na tunazoziidhinisha katika bajeti hii ikishapitishwa na Bunge Tukufu fedha hizo ziende kama zinavyohitajika. Watoto wetu wapate mikopo kwa sababu ukiangalia takwimu hii Bodi ya Mikopo inafanya kazi vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, takribani 70% ya pesa wanayotoa wanaikusanya takribani 70%. Afrika Mashariki, Afrika kwa ujumla na duniani ni moja katika organ muhimu na inafanya kazi vizuri sana. Kwa nini fedha hizi tusiziidhinishe zote zikafika zikapokelewa zikaingia kwenye matumizi vijana wetu wakapata elimu tukawa tunawasaidia kikubwa zaidi? Hilo ni jambo la msingi kwenye Higher Education Students’ Loan Board. Fedha tunazoidhinisha hapa Bungeni ziende Bodi ya Mikopo kama tulivyoidhinisha, vijana wa Tanzania wakanufaike. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, ninalotaka kuchangia ni kuhusiana na Wadhibiti Ubora. Ukiangalia wale Wadhibiti Ubora ni kama CAG katika elimu. Yaani ni wakaguzi ambao wao wanakagua masuala yote yanayohusiana na elimu ndani ya nchi ya Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hebu ifike mahali tuwaondoe kwenye Fungu 56 - TAMISEMI tuwapeleke kwenye Fungu 46 la Bajeti ya Wizara ya Elimu. Kwa nini ninasema hivyo? Mkurugenzi wa Halmashauri ndiye anasimamia karibu shule zote katika eneo lake. Mkurugenzi anaposimamia mwisho wa siku ndiye anayelipa ile capitation grant fee kwa ajili ya wale Wadhibiti Ubora kufanya kazi zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa siku zote anayemlipa mpiga zumari ndiye anayechagua wimbo. Hii maana yake ni nini? Tuwafanye Wadhibiti Ubora wawe huru wafanye kazi zao vizuri. Wakipita kule wakiona hakuna madawati, hakuna miundombinu mizuri ya matundu ya choo au shule zina hali mbaya waweze kuandika ripoti na kushauri vizuri ili tuweze kupata matokeo bora kwenye shule zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninachoshauri hawa moja kwa moja wasimamiwe na Wizara ya Elimu, TAMISEMI wasihusike nao. Malipo yao yote yatoke Wizara ya Elimu waje kwenye Fungu - 46 la bajeti. Hili ni jambo muhimu sana kwa sababu hili ndilo jicho letu katika majimbo ili wafanye kazi zao kiweledi na vizuri zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine la msingi zaidi ni kuhusiana na suala zima la VETA. VETA ndiyo inajenga taswira kubwa ya kutengeneza ujuzi wa nchi hii, ndiyo masterplan ya ujuzi kwa vijana wetu ndani ya Taifa la Tanzania. Fedha zinazotengwa kwa ajili ya VETA zitoke, VETA zikatengenezwe zisimame ili vijana wetu waweze kuingia katika enrolment hiyo na kuweza kupata tija kubwa ya kupata ujuzi hapo baadaye.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka unaokuja mbeleni, darasa la sita wanamaliza, hali kadhalika wanamaliza na darasa la saba, kutakuwa na double cohort. Maana yake huko mbeleni kutakuwa na enrolment kubwa ya wanafunzi kuingia vyuo vya kati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nini kinachohitajika? Kinachohitajika vyuo vya VETA vijengwe kwa haraka viwepo nchi nzima ili vijana hao waingie hapo waweze kupata ujuzi. Wakitoka pale wana ujuzi kamili wataweza kujiendeleza hapo baadaye katika shughuli zao mbalimbali za ajira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, VETA isiishie kujengwa, tuvilinde kwa thamani kubwa. Kwa nini tuvilinde kwa thamani kubwa? Nitatolea kesi moja ya Tanga. Nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri wa Elimu. Tanga tuna Chuo cha VETA kizuri sana. Pale panatolewa mafunzo ya udereva (Passenger Service Vehicle) na HDV (Heavy Duty Vehicle). Palitokea kidogo purukushani lakini baada ya muda kuna mtu alitokea akalala, akaamka, akasema hii kozi nimeifuta.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamshukuru Mheshimiwa Waziri wa Elimu, mtu bingwa kabisa, Profesa Mkenda. Nilikaa naye nikazungumza naye akamtoa Director wa VETA, akamtoa na Naibu Katibu Mkuu wa Elimu, waende Tanga. Leo hii Alhamdulillah Chuo cha VETA Tanga kinatarajia kurudisha kozi ya PSV na kozi ya HDV waweze kusoma pale VETA. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, isiishie kuvijenga hivi vyuo tuvisimamie kwa ari kubwa na kuvitolea jicho. Ndivyo vilivyoshikilia mhimili wa vijana wa Tanzania. Mheshimiwa Rais Dkt. Samia ameweka mtazamo mkubwa sana kwenye suala la VETA kwa sababu ndipo ujuzi wa vijana wetu utapatikana hapo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kusema hayo sasa nitoe pongezi zangu za dhati kabisa kwa Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kupitia Mradi wa HEET (Higher Education for Economic Transformation) na sisi Tanga tumenufaika kupitia Mzumbe University Mkinga Campus; mradi wa dola milioni saba. Haya ni mabadiliko makubwa na ni mageuzi makubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninataka niliambie Bunge hili Tukufu, Tanga ndio chemichemi ya elimu ya Taifa hili. Shule ya kwanza ya Msingi ilikuwa Magila na Shule ya kwanza ya sekondari ni Tanga. Sisi ndiyo watu wa mwanzo kusoma na kuwa na mwanga wa elimu. Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ndani ya awamu yake kuileta Mzumbe University, Mkinga Campus ameiongezea ladha na utamu fahari ya elimu ndani ya Mkoa wa Tanga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwapongeze sana Wizara kwa kuisimamia Miradi hii ya HEET. Tumeitembelea miradi hii value for money unaiona na wakandarasi wazawa wamepewa nafasi. Mfano Mradi ule wa Mloganzila pale mkandarasi mzawa kama Mohamed Builders ameufanya mradi vizuri na unamalizika kwa wakati. Miradi ile iko takriban 70%. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kusema hayo, ninaunga mkono hoja, bajeti hii tuipitishe kwa kishindo. Shukrani sana. (Makofi)