Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Johannes Lembulung’ Lukumay (2 total)

Mpango Elekezi wa Maendeleo wa Muda Mrefu 2026/2027–2050/2051, Mapendekezo ya Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2026/2027–2030/2031 na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Mwaka 2026/2027; na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali Katika Muda wa Kati ya 2026/2027 hadi 2028/2029.
MHE. JOHANNES L. LUKUMAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa ninachukua nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kuridhia mimi kusimama hapa leo. Ninachukua pia nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kupendekeza jina langu Kamati Kuu ya Chama Cha Mapinduzi, Halmashauri Kuu ya Taifa na hatimaye kwenda kuchaguliwa kuwa Mbunge wa Jimbo la Arumeru Magharibi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninawashukuru sana wananchi wangu wa Jimbo la Arumeru Magharibi kwa kumchagua Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kura nyingi kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Pia, ninawashukuru wananchi hao kwa kuwachagua Madiwani wote wa Jimbo la Arumeru Magharibi kuwa Madiwani wa Chama Cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zaidi hawa wananchi wa Jimbo la Arumeru Magharibi ninawashukuru sana kwa imani kubwa waliyonayo kwangu wakanichagua kwa kura nyingi sana kuwa Mbunge wao wa Jimbo la Arumeru Magharibi. Wananchi wa Jimbo la Arumeru Magharibi ninawahakikishia imani waliyonipa sitawaangusha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho katika shukrani, ninapenda pia kuchukua nafasi hii kuishukuru sana familia yangu hususan mke wangu kwa kipindi chote cha harakati kuhakikisha kwamba yupo na mimi katika masuala mengi hususan kuniombea Mwenyezi Mungu, ilikuwa siyo rahisi. Mama ninakushukuru sana kwa jitihada zako na ninakuombea na wewe Mungu aendelee kukulinda na kuweza kwenda kuona matunda ambayo wananchi wa Jimbo la Arumeru Magharibi wataenda kuyapata kupitia uwakilishi wangu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitakuwa sina fadhila nisiposhukuru uwekezaji mkubwa ambao Serikali ya Awamu ya Sita imewekeza katika Jimbo la Arumeru Magharibi. Zaidi ya shilingi bilioni 69.9 ziliwekezwa katika Jimbo la Arumeru Magharibi, ikilenga kwenda kushughulikia changamoto za afya, elimu (elimu sekondari na elimu msingi), nishati (umeme) na miundombinu ya barabara. Ninajua bado tuna changamoto kubwa katika Jimbo la Arumeru Magharibi ikiwemo changamoto ya miundombiunu ya barabara, changamoto ya miundombinu ya maji na Sekta ya Umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachukua nafasi hii kumshukuru tena Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuchagua kwa umakini wasaidizi wake ambao waliendelea kufanya kazi kubwa sana. Tukianza na Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba, Mbunge na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Ninamshukuru ametembelea na nimemweleza mambo mengi katika Jimbo langu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi karibuni alitembelea Mheshimiwa Mohamed Mchengerwa. Yule ni Waziri wetu wa Afya na amezindua, siyo tu bima ya afya lakini mpango au Programu ya Ongea na Waziri wa Afya, yaani Mtanzania wa kawaida unaongea na Waziri anakujibu pale pale. Ile itaenda kutusaidia katika suala la Bima ya Afya kwa Wote, watu wataelezea matatizo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimemwona Mheshimiwa Reuben Mheshimiwa Naibu Waziri wa TAMISEMI alikuja, lakini pia kuna Mheshimiwa Ulega, Waziri wa Ujenzi na Mheshimiwa Naibu Waziri wa TAMISEMI aliyeko upande wa ujenzi. Hawa Waheshimiwa wote walipokuja niliwaeleza changamoto za Jimbo la Arumeru Magharibi na wamesema wataenda kufanyia kazi. Ninamshukuru sana sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa umakini na upendo kwa watu wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ninaomba nichangie Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano kama ilivyowasilishwa. Mpango unaelekeza kuchukua hatua 10. Kwa sababu ya muda nitachangia kidogo, kidogo sana hatua ya nne na kama utaridhia ninaomba ninukuu. Inasema hivi: “Kutokana na muda ...” ninarudia tena kunukuu. Inasema hivi; “Kulenga kuwa na kituo kinara cha Utalii wa Tiba ambacho kitaboresha ubora wa maisha ya Watanzania wote na kitakuwa na sekta ya afya kama engine muhimu ya maendeleo na uchambuzi wa Kimataifa.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili haya yatokee sasa, kutekeleza hii hatua ya nne Taifa liwekeze katika huduma ya kinga kuliko kuwekeza katika huduma ya tiba. Uwekezaji wa kutosha kwenye huduma za kinga una manufaa makubwa sana katika Taifa. Kinga inasaidia kupunguza gharama kubwa ya tiba. Kinga inasaidia kufanya Taifa kuwa lenye nguvu kwa sababu watu wanakuwa wanafanya kazi. Tunakuwa tuna uwezo mkubwa kushiriki shughuli za kiuchumi hususan uzalishaji mali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kinga inasaidia pia hata ile tiba kuwa rahisi, kwa sababu watakaokuwa wanaugua ni wachache. Kwa hiyo, watu wanapata huduma nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba niende sehemu ya pili kwenye hilo. Kuna utoaji wa huduma nchini na mgawanyiko wa rasilimali. Vituo vya kutolea huduma Tanzania hii ni vituo 13,774. Hiyo inajumuisha maabara binafsi na kliniki mbalimbali, lakini kati ya hizo, vituo vya kutolea huduma (zahanati, vituo vya afya na hospitali) ngazi mbalimbali vinafika 10,588. Kati ya hizo tena, vituo 7,689 sawa na 85% ziko chini ya Mamlaka ya Serikali za Mitaa (Primary Health Care) na hizi ziko chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu ambayo ni TAMISEMI.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia mgawanyo wa rasilimali kama alivyoelezea ndugu yangu Mheshimiwa Dkt. Mahera hapa, fedha nyingi zinabaki katika sehemu ya uratibu. Wale watu wengi ambao tumesema ni 73% wanapata sehemu kidogo. Kwa hiyo, kuna haja ya Serikali kuangalia namna ya kugawa rasilimali hizi kwa kufuata formula.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapendeeza labda tutumie formula ya Mfuko wa Pamoja ambao tunasema kwamba ni Basket Fund ambao unaweza ukasaidia kugawa rasilimali hizi hususan rasilimali fedha, ili wale wananchi wengi walioko vijijini waweze kupata huduma bora za afya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kumalizia kwamba, tukiwekeza kwenye kinga hususan suala la chanjo, suala la uchunguzi tunaita Screening ambayo inasaidia kutambua magonjwa kabla hayajafika mbali au kwa hatua za mwanzo ambazo zinaweza zikapata tiba zinaweza kusaidia kuimarisha maisha ya watu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kusema hivyo ninaomba kusema kwamba ninaunga mkono hoja. Mungu ibariki Tanzania na Mungu libariki Jimbo la Arumeru Magharibi. Ninakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027
MHE. JOHANNES L. LUKUMAY: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa, nichukue nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu, Mwingi wa Rehema, kwa kuniwezesha kusimama hapa mbele ya Bunge lako Tukufu kuchangia hoja ya Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuteuliwa na Umoja wa Nchi za Afrika kuwa Bingwa wa Afya ya Mama na Mtoto.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia, nimpongeze Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuweka msisitizo kwenye Bima ya Afya kwa Wote na kuhakikisha kwamba wale wananchi wote ambao wana magonjwa sugu ikiwemo ugonjwa wa moyo, figo, sukari na hawana uwezo kabisa, wanaenda kupata tiba ambayo Serikali imegharamia. Hiyo yote imeenda sambamba na watoto chini ya miaka mitano akina mama wajawazito, wazee na wale wote wanaotoka katika jamii ambayo ni maskini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba nitoe hizo shukrani kwa Mheshimiwa Rais wetu, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan. Ninampongeza pia kumteua Mheshimiwa Dkt. Mwigulu, Waziri Mkuu wetu. Ningependa nimwone nimweleze moja kwa moja, lakini atapata habari.

Mheshimiwa Naibu Spika, Waziri Mkuu amekuwa kimbilio la wananchi. Watu wamejenga matumaini makubwa kwa kazi anayoifanya. Amekuja kwenye jimbo langu, ametatua mambo mengi. Ameenda moja kwa moja akatatua matatizo makubwa sana yaliyokuwa yanakabili wananchi wangu.

Mheshimiwa Naibu Spika, moja kubwa ni maji. Nilimweleza kuhusu matatizo ya maji katika Jimbo la Arumeru Magharibi na shilingi bilioni 520 ambayo ilikuwa inaenda Jiji la Arusha nikamwomba mwezi Novemba tarehe 30, mwaka 2025 kwamba kata zilizoko karibu na mradi huo zipate hayo maji sasa, na amefanyia kazi, akaenda akamweleza Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, tukapewa shilingi bilioni 2.7, na sasa wananchi wanapata maji. Ninamshukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, juzi nilikuwa ninagawa mipira kwenye moja kati ya hizo Kata inaitwa Kiranyi ambazo Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan amesikia kilio cha wale wananchi wa Jimbo la Arumeru Magharibi, akatoa mipira ya maji mingi sana. Bado Kata nyingine zilizobaki kama Kata ya Kimnyaki, Kata ya Sambasha, Kata ya Olorieni, Kata ya Tarakwa, Kata ya Oldonyosambu, Kata ya Oldonyowass, nao wategemea kupata mipira, tayari kupata maji na kuondokana na kero ya maji katika Jimbo la Arumeru Magharibi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikupongeze sana kwa kunipa nafasi ya kuongea kuhusu Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kazi anayoifanya. Kwa upande wa barabara amefanya kazi kubwa alitembelea Hospitali yangu ya Wilaya ya Olturumet, akatoa agizo sehemu kidogo tu ya kilometa mbili ya barabara itengenezwe, ikatengenezwa mara moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ninaomba pamoja na hayo yote, Jimbo la Arumeru Magharibi lina tatizo kubwa sana la barabara pamoja na matatizo mengine. Kuna barabara mbalimbali katika hili jimbo ambazo tunazo. Kuna Barabara ya Lolino – Selian, kuna Barabara ya Olturoto - Mringa, kuna Barabara ya TPRI kwenda Likamba, Barabara ya Kilimamoto -Mwandeti, Sanawari - Oldonyosambu, Sokoni II - Bangata, Mbauda - Osunyai, kuna nyingine inaitwa Malula mpaka Nduruma.

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hizi zitatengenezwa kwa sababu watu hawa wanafanya kazi chini ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, lakini kutokana na bajeti aliyoongeza ya TARURA, ninaomba jimbo langu liongeze bajeti kutoka shilingi bilioni 2.3 ya sasa, zifike angalau shilingi bilioni sita ili hizi barabara zilizobaki ziende kufanyiwa kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa ninaongelea suala la maji. Nilisema Mheshimiwa ametatua hilo tatizo, lakini ninaomba sasa pamoja na kwamba ametatua, ninaomba miradi tisa ya maji ambayo inaendelea ya Olmolog, ilibaki shilingi milioni 700, kuna ya Oldonyosambu, Mungushi, Engalaoni, kuna Mradi wa Ilkerin, Mradi wa Engorora, kuna Mradi wa Themi ya Simba Oljoro Lengare, ninaomba Waziri wangu wa Afya atekeleze kama alivyoahidi ili hawa wananchi wa Arumeru Magharibi waweze kupata maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie na suala la UKIMWI. Katika ziara ya Kamati yangu, tulitembela konga ya UKIMWI kule Dar es Salaam, mambo yanaenda vizuri, lakini wananchi wale wanafanya kazi vizuri hasa yule Mkurugenzi wa Jiji la Dar es Salaam, anawasaidia lakini kwa ujumla kwa Watanzania bado kuna elimu ya UKIMWI inahitajika.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, kutokana na suala lililoko sasa hivi la dawa za UKIMWI kukosekana kutoka nje za nchi, kuna kiwanda cha dawa kiko pale Arusha, ninaomba sasa zipelekwe zile shilingi bilioni 23 zilizobaki ili kiwanda kianze kufanya kazi mwezi wa sita watu wapate dawa, na pia tuweze kuuza nchi nyingine za nje hasa hizi za East Africa, tuweze kuwekeza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niipongeze Serikali yangu kuhakikisha kwamba tunaenda kuweka viwanda vya kutengeneza dawa za katika nchi hii tuondokane na suala la utegemezi wa dawa kutoka nchi za nje. Hilo nilikuwa ninaomba liwekwe maanani zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho kabisa ni suala la afya ya msingi watalaamu, tunaita primary healthcare. Katika nchi hii, huduma za afya ya msingi ni muhimu. Kwa nini? Zaidi ya 75% ya Watanzania wanapata huduma katika afya ya msingi. Afya ya msingi inaanzia hospitali ya wilaya, vituo vya afya na zahanati.

Mheshimiwa Naibu Spika, bajeti inavyoandaliwa ya Wizara ya Afya na TAMISEMI, japokuwa baadaye nitaongelea suala la Wizara ya Afya, ninaomba sasa iwekeze zaidi, na iweke kipaumbele kwenye afya ya msingi ili wananchi waweze kupata kinga, magonjwa yale sugu yagunduliwe mapema. Wakifanyiwa screen, kwa mfano ya haraka haraka, mtu akapatikana na saratani, anaweza akatibika kwa urahisi zaidi. Magonjwa mengine kama ya kisukari, magonjwa ya moyo yanajulikana, tupate chanjo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ninasisitiza zaidi kwamba afya ya msingi ipewe kipaumbele katika bajeti yetu. Hasa ukizingatia na ukiangalia kwa haraka haraka, ukienda kwenye vituo vya afya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan amewekeza vifaa vya kutosha.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi sasa ninavyoongea, Waheshimiwa wataniunga mkono, upasuaji wa dharura kwa akina mama wajawazito unafanyika katika vituo vya afya. Tuimarishe hivyo vituo vya afya kwa hivi sasa ambavyo viko katika ngazi ya afya ya msingi ili wananchi walio wengi kule vijijini waweze kupata huduma nzuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, tuwekeze zaidi kwenye hivi vituo vya afya wapatikane watumishi, vipatikane vifaa na tutangaze kazi nzuri iliyowekezwa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwenye hivi vituo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ninamalizia kurasa. Nimesikia watu wanaongelea bima ya afya. Bima ya afya ni ukombozi mkubwa katika nchi hii. Ninaomba watu waelezwe umuhimu wa bima ya afya. Ninasikia watu wanasema wanadaiwa hela kwa watoto chini ya miaka mitano. (Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, TAMISEMI sasa ilekeze nguvu kubwa kwa vituo vya afya kuanzia hospitali ya wilaya, vituo vya afya na zahanati, wananchi wapate taarifa sahihi. Juzi nilimwona Mheshimiwa Waziri Mkuu akimwuliza Mganga Mkuu mmoja wa wilaya sipendi kumtaja. Akasema dawa zinapatikana kwa 95%, akambana, akajichanganya, akasema mtu mwingine ameenda kufanya prescription.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba sasa watu waseme ukweli kuhusu nchi yao, waeleze ukweli, wachukue muda mdogo kuzunguza na wagonjwa. Semeni! Sera ni nzuri sana na Serikali inafanya kila jitihada, dawa zinapatikana katika vituo vya afya, wananchi hawana habari. Kwa hiyo, ninaomba ifike wakati sasa TAMISEMI ihakikishe watu wanapewa taarifa sahihi. Watu wapate tiba kama ilivyokusudiwa, na kama ilivyowekwa katika Bima ya Afya kwa Wote katika nchi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba kuwasilisha na ninaunga mkono hoja. Ahsante. (Makofi)