Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Charles Mhando Njama (3 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027
MHE. CHARLES M. NJAMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi. Nami nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Kilimo, na Naibu wake; Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo pamoja na Wakurugenzi wake wote kwa namna ambavyo wameleta wasilisho zuri katika bajeti yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwapongeze pia kwa kazi nzuri ambayo inaonekana kwa miradi mbalimbali ambayo wanaendelea kuitekeleza katika Wizara ya Kilimo. Wizara ya Kilimo ni uti wa mgongo wa Taifa letu. Kwa kuzingatia hilo, tunaona fursa kubwa ambayo ipo kupitia kilimo katika nchi yetu hasa kutengeneza ajira nyingi zaidi wa vijana wa Tanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili tuweze kufikia uongezaji wa ajira kwa vijana wetu wa Tanzania nafikiri tunapaswa tufanye mambo mawili makubwa. Jambo la kwanza ni vizuri tukawekeza zaidi katika utafiti kama vile ambavyo wenzetu upande wa madini wanafanya utafiti ili kuondoa uncertainties zilizopo katika wachimbaji, vivyo hivyo tunatakiwa tufanye utafiti wa kutosha katika mbegu, katika ardhi na aina ya mazao ambayo yanaweza kuwa katika maeneo tofauti tofauti ili kuondoa uncertainties kwa vijana wanaotamani kwenda kuingia katika kilimo zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili ambalo pia ni vizuri kuliwekeza kwa nguvu kubwa ni upande wa masoko wa mazao ambayo tunaenda kuzalisha tukiweka nguvu katika maeneo haya mawili, tutakuwa tumewashawishi wakulima na hasa vijana kuingia zaidi katika kilimo kwa kuwa watakuwa na uhakika mtaji wanaoupeleka katika eneo fulani la kilimo wana uhakika wa kuvuna na wana uhakika pia baada ya kuvuna wanalo eneo la kwenda kuuza mazao yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika upande wa masoko, Waheshimiwa waliochangia jana, baadhi nimesikia wakiongelea vizuri kazi nzuri iliyofanywa na COPRA. Ninafikiri ni wakati mwafaka sasa Mheshimiwa Waziri ukaona namna gani unaenda kuwekeza zaidi katika taasisi hii ili iweze kutafuta masoko zaidi na kuwahakikishia wakulima masoko ya bidhaa ambazo wanakwenda kuzizalisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo tunatakiwa tuliwekee nguvu na ninampongeza sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa ambayo ameshaifanya na Mkurugenzi wa Tume ya Umwagiliaji ambao wamefanya kazi kubwa mpaka sasa, lakini bado tunayo kazi kubwa ya kufanya kuhakikisha kwamba tunaendeleza miradi ya umwagiliaji katika maeneo mengi ya nchi, kwa kuwa hili nalo ni eneo ambalo litakwenda kuleta uhakika kwa wakulima badala ya kuendelea kutegemea mvua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Jimbo letu la Korogwe Mjini tunamshukuru Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, tuna miradi miwili mikubwa ya umwagiliaji. Tunao mradi wa umwagiliaji katika Kata yetu ya Kwamdolwa, tunao pia mradi mkubwa wa umwagiliaji katika Kata yetu ya Kwamsisi. Miradi hii miwili kwa ujumla wake inagharimu takribani shilingi bilioni 29.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, ninamwomba Mheshimiwa Waziri, katika bajeti yake na hasa atakapokuja kufanya finalization, angalau atupe tumaini kwa sababu miradi hii imekuwa ikisuasua kwa muda mrefu sana. Tunahitaji twende tukaone utekelezaji wa miradi hii inatekelezwa kwa kuwa inaenda kuleta chakula kwa wananchi, lakini pia inaenda kutengeneza ajira nyingi kwa watu wa Korogwe Mjini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine kwa upande hasa wa jimbo langu, sisi ni miongoni mwa wazalishaji wa zao la mkonge na wananchi katika Jimbo la Korogwe Mjini wameonyesha utayari wao kwa kuwa wengi wamejikita katika kilimo cha mkonge, lakini tunayo changamoto ya upungufu wa mashine za kuchakata mkonge, mashine za corona.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, alivyopita katika wakati wa kampeni katika Jimbo la Korogwe Mjini na Korogwe kwa ujumla aliahidi kutuletea mashine hizi za uchakataji wa mkonge katika Jimbo la Korogwe Mjini na Korogwe Vijijini pia. Ninamwomba Mheshimiwa Waziri aone namna gani tunakwenda kupata sasa hizi mashine za corona katika eneo letu ili katani inayozalishwa isiende kuharibika kwa kukosa mashine za uchakataji wa mkonge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ninafikiri tuna fursa katika eneo hilo. Tunazalisha mkonge kwa wingi, lakini tunasafirisha mkonge nje. Hata hivyo, tunayo fursa ya kuanzisha viwanda vya kutengeneza final products za mkonge ambazo pia zitakwenda kutusaidia kukabiliana na products ambazo zinaharibu mazingira. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna wenzetu wanazalisha korosho, wanazalisha kahawa ambayo sisi tukiwekeza katika uzalishaji wa gunia tunaenda kuleta vifungashio ambavyo vitakuwa ni rafiki kwa mazingira, lakini pia tunaongeza ajira kwa maeneo ambayo tunazalisha mkonge hasa Korogwe na eneo lote la Mkoa wa Tanga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Jimbo la Korogwe Mjini tuna vikundi vingi ambavyo vimejikita katika uzalishaji wa mboga mboga, lakini changamoto tunayokutana nayo ni kwamba wakati mwingine akina mama wale na vijana wanapopeleka mbogamboga sokoni, zinakosa wateja kwa wakati huo. Ombi lao kubwa la namna ya kuboresha biashara yao na kilimo chao cha mbogamboga ni kupata cold room ambayo angalau hata kama watakwenda sokoni na watakosa wateja, basi mboga zile zisirudi kuharibika na badala yake ziwe zimetunzwa na kuwe na uhakika wa kuuzwa wakati mwingine unaofuata. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunamsihi sana Mheshimiwa Waziri aangalie katika bajeti yake namna gani tunaweza tukapata cold room kwa ajili ya storage ya mbogamboga na matunda yanayozalishwa katika Jimbo letu la Korogwe mjini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kupatiwa kiwanda cha kuchakata haya mazao ambayo ni perishable kama namna ya mojawapo ya kwenda kufanya storage na hasa nyanya ambazo zinazalishwa na wakulima hawa wadogo wadogo katika eneo letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie katika zao la machungwa. Sisi Tanga tunaamini hakuna eneo linalozalisha machungwa bora zaidi ya Mkoa wa Tanga. Sasa tunaomba kupatiwa kiwanda cha kutengeneza juisi za matunda. Korogwe ilikuwa na Kiwanda cha Tang Gold ambacho baadaye kilipewa mtu binafsi ambaye ameshindwa kukiendesha. Hata hivyo, Mheshimiwa Rais alivyopita katika Jimbo la Korogwe Mjini wakati wa kampeni alisema kiwanda kile kitarudishwa kwa wananchi na kiendelee kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba tuone namna gani sasa tunaweza tukaanza ku-process matunda yetu ndani ya eneo la Korogwe badala ya kusafirisha machungwa kwenda nchi jirani halafu baadaye tuletewe tununue kwa bei kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo ninaomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027
MHE. CHARLES M. NJAMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kulipa nafasi. Awali ya yote nianze kwa kuipongeze sana Serikali chini ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa namna ambavyo imeendelea kukamilisha adhima yake ya kumtua mama ndoo kichwani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru sisi watu wa Korogwe Mjini tunayo miradi miwili mikubwa ya maji. Tunao Mradi wa Miji 28, ambapo mradi huu ni tegemeo kubwa na tumaini lililojaa kwa wananchi wa Jimbo la Korogwe Mjini kwamba sasa tunakwenda kusahau changamoto ya maji Korogwe Mjini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia, tunao mradi wa Ndemaha. Mradi huu nao utakwenda kutusaidia kuongeza wingi wa maji katika Jimbo letu. Pamoja na miradi hii miwili, tunafahamu kumekuwa na changamoto kwa kiasi, hasa katika mradi wetu wa Miji 28 kwa kuwa tulitazamia kupata maji katika Jimbo letu la Korogwe na kuanza kuyapokea mwezi wa Nne, lakini katika ufuatiliaji inaonekana tutayapata mwezi wa Saba. Bado tuna matumaini makubwa, kwamba mradi huu utakamilika na tutapata maji haya kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi wetu wa Mto Ndemaha, bado unasuasua sana. Ninamwomba kaka yangu Waziri Aweso atusaidie, twende tukaukamilishe mradi huu ili kuhakikisha kwamba maeneo yote ya Jimbo la Korogwe Mjini, katika kata zetu zote 11, tuna uhakika wa kupata maji yanayotosha, ambayo ni safi na salama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wa Jimbo la Korogwe Mjini tuna wasiwasi. Pamoja na miradi hii mikubwa, ambayo tuna uhakika ikikamilika tutapata maji takribani cubic meter za ujazo milioni 16 ambapo ukilinganisha na uhitaji wetu wa sasa wa milioni saba, tutakuwa na ziada ya takribani lita milioni tisa ambazo tunaamini hatutakuwa na changamoto ya maji ndani ya miaka 25 hadi 30 ijayo katika Jimbo letu la Korogwe Mjini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, changamoto ambayo tunaiona mbele yetu ni wasiwasi wa kuwepo kwa upotevu wa maji baada ya maji haya kukamilika kufika katika Jimbo letu la Korogwe Mjini. Hii ni kwa sababu, miundombinu ya maji tuliyokuwa nayo katika Jimbo la Korogwe Mjini, mingi ni chakavu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninafahamu Wizara inao mpango wa kwenda kurekebisha miundombinu ile ili kuhakikisha kwamba upotevu wa maji tunaukabili iwezekanavyo. Ninamsihi Mheshimiwa Waziri pamoja na timu yake, tukaweke kipaumbele katika kukarabati miundombinu hii, ili maji yatakapofika hasa haya ya miji 28, tusiwe na upotevu wa maji katika eneo lile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia, ile nia ya maji kufika kwa wananchi iweze kukamilika. Tusije tukawa tuna maji mengi lakini wananchi wanashindwa kupata maji kwa sababu ya miundombinu ambayo imekuwa chakavu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuongelea upotevu wa maji katika ujumla wake kama nchi, ninaona kama tunayo fursa kubwa ya kwenda kuimarisha huduma ya maji katika jamii. Takwimu zinaonesha kwamba takribani 35% ya maji yanapotea, ukiya-quantify katika fedha, ni takribani shilingi bilioni 240. Ukiangalia bajeti yetu ya mwaka huu, ambayo ni shilingi trilioni 1.12, kiasi hiki kinachopotea, ni karibia 22% ya bajeti ambayo tunaenda kuipitisha mwaka huu. Maana yake ni nini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza hatuwezi kurudisha gharama za uzalishaji wa maji ambazo tunazitumia. Ukiangalia kwa hii 35% inayoongelewa ya upotevu, kama ni sahihi, maana yake ni kwamba katika kila shilingi 100 ambayo unaitumia kuzalishia maji, shilingi 35 zinapotea njiani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tukiweza kwenda kukabiliana vizuri na changamoto ya upotevu wa maji, tunao uwezo wa kuipunguzia Serikali mzigo wa kuendelea kuingiza fedha katika bajeti hii, na Wizara hii ikawa na vyanzo vya kuweza kuisaidia ku-fund bajeti yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninamwomba Mheshimiwa Waziri, na nimeona namna ambavyo amekuwa mkali katika eneo hili la upotevu wa maji, na ameleta transformation nyingi katika Wizara hii ya maji, ninaamini na hili tunao uwezo wa kwenda kulikabili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, ninaunga mkono hoja, na ninakushukuru tena kwa nafasi.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu Mwaka wa Fedha 2026/2027
MHE. CHARLES M. NJAMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi. Kwa kuwa ni mara yangu ya kwanza kuchangia hoja hii, ninaomba nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu Mwingi wa Rehema ambaye amenibariki kupata nafasi ya kushiriki katika Bunge hili Tukufu kuwawakilisha wananchi wa Jimbo la Korogwe Mjini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nikishukuru Chama changu Cha Mapinduzi chini ya uongozi wa Mwenyekiti wetu Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuniteua kati ya wengi kuwa mgombea wa Chama cha Mapinduzi katika Jimbo letu la Korogwe Mjini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ninawashukuru sana wananchi wa jimbo langu la Korogwe Mjini ambao wamenipa imani kubwa, ambao wameniunga mkono kwa kura nyingi katika uchaguzi uliofanyika Oktoba 29. Imani waliyonipa nami ninawaahidi nitawalipa kwa kufanya kazi usiku na mchana kuhakikisha kwamba tunatetea maslahi ya Jimbo la Korogwe Mjini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninampongeze Rais Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa jinsi ambavyo anatekeleza majukumu yake na hasa kwa namna alivyotekeleza ahadi zake alizoziweka kwa ajili ya siku 100 za kwanza katika uongozi wake. Hakika mama ameamua kuitumikia nchi na tunaona akifanya kwa vitendo na Mungu ambariki azidi kumpa afya njema aendelee kutekeleza majukumu yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile ninampongeza Waziri Mkuu, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba kwa namna ambavyo anaendelea kufanya kazi usiku na mchana pasipo kuchoka. Vilevile, tunamshukuru kwa ziara alizozifanya katika maeneo mengi ya nchi hususan sisi Wabunge wa Mkoa wa Tanga kwa namna ambavyo ziara yake aliyoifanya katika mkoa wetu wa Tanga imeleta tija kubwa na imeleta mwamko na uwajibikaji kwa watumishi wa Serikali katika Mkoa wetu wa Tanga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wa Jimbo la Korogwe Mjini wanamwomba, kwa kuwa katika ziara yake hawakupata nafasi ya kutoa kero zao kwa sababu kwa bahati mbaya ratiba haikuruhusu kuwa na wakati wa maswali alipokuwa katika eneo la Mswaha, basi wakati mwingine akipita atenge muda wa kukutana na wananchi wa Korogwe Mjini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninampongeza Mkuu wangu wa Mkoa Dkt. Batilda Buriani kwa namna ambavyo anaendelea kufanya kazi kwa maslahi mapana na maendeleo ya Mkoa wa Tanga, na pia Mwenyekiti wetu wa Chama Ndugu yetu Rajabu Abdallah kwa namna ambavyo amekuwa kinara wa kuhakikisha duka la Mkoa wa Tanga linaendeshwa vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya pongezi hizo, ninamshukuru Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan. Hakika katika awamu yake ya uongozi, miradi mingi mikubwa ya maendeleo imetekelezwa katika jimbo letu la Korogwe Mjini. Tumeona shule nyingi za sekondari zikiwa zimejengwa katika jimbo letu la Korogwe Mjini, tumeona sasa hivi ujenzi wa barabara ya TACTIC kilometa 10.4 ukiwa unaendelea na tunatazamia kabla ya mwisho wa mwaka huu, ujenzi ule utakamilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ujenzi ule utakwenda kubadili sura na mwonekano wa jimbo letu la Korogwe Mjini. Tutakuwa tunakwenda kupata barabara za lami, lakini pia taa za barabarani pamoja na mifereji, tunamshukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nirudi katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu imejaa matumaini makubwa kwa wananchi, imejaa nuru kwa wafanyabiashara, lakini vivyo hivyo pia matarajio ya maendeleo katika maeneo mengi na nyanja tofauti tofauti katika nchi yetu ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kwa upande wa Jimbo letu la Korogwe Mjini tunapoongelea mageuzi ya kiuchumi na ongezeko la ajira, tuna vitu kadhaa ambavyo kwetu ni kipaumbele. Katika ziara ya kampeni ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan alivyopita katika jimbo letu la Korogwe Mjini tulimwomba na aliridhia ujenzi wa bandari kavu katika Jimbo la Korogwe Mjini katika eneo letu la Kata ya Old Korogwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bandari kavu hii ina maana kubwa sana katika uchumi wa watu wa Korogwe. Bandari kavu hii itakwenda kupunguza congestion ya malori katika barabara ya Tanga – Segera.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bandari kavu hii itakwenda kuongeza mzunguko wa fedha kwa wafanyabiashara wadogo wadogo, na wa kati katika Mji wetu wa Korogwe Mjini. Kwa hiyo, tunaomba, katika bajeti itakayoletwa, tuone utekelezaji wa ujenzi wa bandari kavu katika mji wa Korogwe, kwa sababu kwetu sisi hii inakwenda kukuza uchumi na kuongeza ajira kwa vijana wa Korogwe Mjini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia, Serikali ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ilipitisha ujenzi wa bonde la umwagiliaji katika Kata yetu ya Kwamsisi kwa takribani shilingi bilioni 24.5 na pia, katika Kata ya Kwamndolwa kwa takribani shilingi bilioni nne. Ujenzi ule hauendelei kwa sasa. Tunaomba katika bajeti ya kilimo itakayokuja, basi miradi hii ioneshwe namna gani inakwenda kutekelezwa katika kipindi cha bajeti hiyo inayokuja kwa mwaka wa fedha 2026/2027.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii nayo inakwenda kuchochea uchumi na uzalishaji wa mazao ya chakula pamoja na mbogamboga katika maeneo yetu ya Jimbo la Korogwe Mjini. Miradi hii ina tija kubwa, ninaomba tuipe kipaumbele cha juu ili kuhakikisha tunakwenda kuitekeleza na kukamilika kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi wa Kwamndolwa umekaa kwa muda mrefu, wakandarasi wameenda pale zaidi ya watatu wakiwa wanabadilishwa badilishwa kwa kushindwa kutekeleza mradi ule. Sasa wananchi wa Kata ya Kwamndolwa hawana imani kama kweli ahadi iliyowekwa itakwenda kutekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa imani yangu kubwa tuliyokuwanayo kwa Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan pamoja na Waziri Mkuu, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba na Waziri mahiri wa Kilimo tunaamini mradi ule unakwenda kutekelezwa na ninaomba upewe kipaumbele cha kwanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba alipofanya ziara yake Mkoa wa Tanga tulimwomba kuhusiana na hospitali yetu ya Magunga. Kutokana na eneo iliyopo, Hospitali ya Magunga inahudumia watu wengi na siyo tu wakazi wa Jimbo la Korogwe Mjini, bali Wilaya za Lushoto, Handeni, na maeneo ya karibu ya Wilaya ya Muheza wote wanapata huduma hapa. Siyo hayo tu, kwa sababu ipo katikati ya barabara kubwa, wagonjwa wanaotokana na ajali za barabarani wengi wamekuwa kimbilio lao la kwanza ni Hospitali ya Magunga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hospitali hiyo imekuwa kongwe kwa kuwa imejengwa tangu mwaka 1952, na sasa ina umri wa miaka zaidi ya 73. Tuliomba hospitali ile ijengwe upya na tunashukuru Serikali ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan imetuletea shilingi bilioni moja ambayo tunatazamia kuanza ujenzi wa maternity complex.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba sasa badala ya kuweka viraka katika hospitali ile, bajeti ya mwaka huu 2026/2027 na kuendelea, sasa iwekwe angalau kila mwaka tupate jengo moja kubwa jipya ili baada ya miaka mitatu au mitano tuwe tumepata majengo yote mapya ya Hospitali ya Magunga, iendane na hadhi ya ukuaji wa Mji wa Korogwe, na pia uendane na barabara hii sasa ambayo tunaitoa kutoka NMB kwenda katika Hospitali ile ya Magunga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika upande wa barabara pamoja na kupata kilometa 10.4 za TARURA kupitia TACTIC, na bado jimbo letu lina changamoto kubwa sana ya barabara. Hivi tunavyoongea, na mvua zinazoendelea katika Mkoa wa Tanga Kata zetu za Mtonga, Bagamoyo, na Kilole miundombinu yake haipitiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninawaomba wenzetu wa TAMISEMI katika bajeti yao watutengee angalau kuongeza kilometa 10 - 15 za changarawe katika Jimbo la Korogwe Mjini. Kwa kufanya hivyo, tutakuwa tumepunguza changamoto ambazo watakuwa wanazipata.

MWENYEKITI: Mheshimiwa, muda wako umekwisha.

MHE. CHARLES M. NJAMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante ninaomba kuunga mkono hoja. (Makofi)