Mpango Elekezi wa Maendeleo wa Muda Mrefu 2026/2027–2050/2051, Mapendekezo ya Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2026/2027–2030/2031 na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Mwaka 2026/2027; na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali Katika Muda wa Kati ya 2026/2027 hadi 2028/2029.
MHE. JAPHAEL M. LUFUNGIJA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa nafasi hii. Awali ya yote nianze kwa kumshukuru Mungu kwa kunipa kibali cha kuweza kusimama ndani ya Bunge hili Tukufu nikiwa na afya njema.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitumie fursa hii pia kumshukuru sana Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan na vikao vyake vyote kuniwezesha kuniteua mimi kuwa Mbunge katika Jimbo la Ulyankulu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitumie fursa hii kuwashukuru sana wananchi wa Jimbo la Ulyankulu wote wa Chama cha Mapinduzi na wananchi wote kwa kuniamini, naweka ahadi yao kwamba nitawawakilisha vema kwa muda wangu wote, nikiwa ndani ya Bunge na nje ya Bunge.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumepokea mpango mzuri wa Serikali, mpango wa utekelezaji wa miradi kwa wananchi wetu. Mchango wangu nataka nijikite kwenye Wizara yetu ya Kilimo, ambapo naamini ajira kubwa ya Watanzania iko kule. Pamoja na mipango mizuri iliyoelezwa na Waziri wetu hapa, ninataka niishauri Serikali kwamba uwekezaji wetu mkubwa wa Serikali, twende tukawekeze kwenye kupima mashamba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiwa na mashamba ambako shughuli zote za kilimo zinafanyika kule, tutatambua kwamba eneo fulani linatumika kwa kilimo gani? Pia maeneo ya ufugaji tunaamini wananchi wetu ndio wakulima na wafugaji. Yapo maeneo mengi ambayo Baraza la Mawaziri lilifanya maamuzi ya kubadilisha matumizi, lakini tunayo migogoro mikubwa kwenye maeneo hayo ya mipaka baina ya uhifadhi na wananchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ili kuweza kuitekeleza vizuri dira hii ni vizuri kila eneo wataalam wetu, Maafisa Mipango Miji, lakini pia na watu wa Idara ya Ardhi waliopo huko kwenye maeneo yetu, kwenda kusimamia mpango wa matumizi bora ya ardhi katika maeneo hayo. Mpango huu usiposimamiwa vizuri, malengo haya tutakwenda kukwama. Nilikuwa najaribu kusisitiza sana kwenye hilo eneo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, uko mpango wa uchimbaji wa mabwawa, umewekwa vizuri na umeainishwa. Katika bajeti ambayo inapangwa, nilikuwa naweka sisitizo, maeneo haya ambayo yameainishwa kuchimbwa mabwawa kwa ajili ya umwagiliaji ni vizuri yakapewa kipaumbele ili kuendelea kutekelezwa. Tukitekeleza haya, nina imani kubwa kwamba tutaondokana na kilimo cha kutegemea mvua ili wananchi waweze kuzalisha kwa wakati wote. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo nilitaka niliwekee uzito kuishauri Serikali ni suala la huduma za afya. Tumejenga vituo vingi vya afya na zahanati, lakini katika maeneo hayo ni vizuri kuimarisha afya za Watanzania kuendelea kuimarisha miundombinu kwenye vituo vya afya ambavyo tayari vimeshaanza kujengwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunajua vimejengwa vingine watumishi wetu kwa maana ya Madakari na Manesi hakuna hata nyumba za kuweza kuishi. Wanalazimika kuishi mbali ambapo ili kuwapata wananchi, wanalazimika kutafuta usafiri wa kumfuata mhudumu kwenye eneo la kituo husika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nilitaka kuishauri Serikali iweze kusimamia jambo la kuhakikisha kwamba miundombinu rafiki kwenye maeneo yetu ya vituo vya afya, zahanati na hospitali yanaimarika ili kumarisha afya za Watanzania kwa ajili ya kutengeneza Taifa lenye afya bora na kuimarisha afya za Watanzania ili waweze kutimiza majukumu yao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumesikia hotuba pia ya Mwenyekiti wa Kamati, pamoja na ushauri wake, nami naungana nao kabisa, kwamba yako maeneo muhimu sasa yanatakiwa kuangaliwa. Ule ushauri wa Kamati uzingatiwe ili kwenda kuitekeleza vizuri hii Dira ya Taifa ya Maendeleo ya muda mfupi, muda wa kati na muda mrefu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, uzoefu unanionesha kwamba, asilimia kubwa ya Watanzania walioko kijijini ni vijana ambao ndio Taifa tunalolitegemea. Kwa hiyo, naendelea kushauri kwamba kuwe na sheria na sera nzuri za kuweza kutengeneza mazingira kuhamasisha vijana hawa wanakwenda kutimiza majukumu, utendaji wa kazi kuliko vijana wengi kubaki wakizurura wakati wa kazi. Kwa hiyo, nashauri sana Serikali ili kuweza kwenda vizuri na Mpango wetu wa Dira ya Maendeleo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine, tunavyo vijiji vingine vipya ambavyo Baraza la Mawaziri lilikubali viendelee ambavyo vilikuwa ndani ya hifadhi. Eneo hilo la wananchi wetu halipitiki. Ninaiomba Serikali kupitia TAMISEMI na Wizara ya Ujenzi kupeleka miundombinu ya barabara katika maeneo hayo. Kuwekwe bajeti kubwa ili barabara zifunguke ili kuwasaidia wananchi kusafirisha bidhaa wanazozalisha na kuyapata masoko bora. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wanakosa fursa ya kupata bei kwa sababu tunakuwa na changamoto maeneo mengine, usafirishaji wa mazao yao wanaingia gharama kubwa. Kwa hiyo, magari hayawezi kufika wanalazimika kusafirisha kwa usafiri ambao ni duni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naendelea kuiomba sana Serikali kuyatazama wakati wa bajeti maeneo haya ya vijiji vipya ili kuweza kufungua miundombinu ya barabara iweze kuimarika ili wananchi wetu waweze kukuza uchumi wao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango wa Serikali ambao tumeupokea hapa ni mpango mzuri. Kikubwa tu ni kuweka sheria na sera nzuri za kwenda kutekeleza vizuri mpango huo. Mimi natoka Jimbo la Ulyankulu, iko mipango ambayo Serikali iliekeza kwa muda mrefu, lakini unaweza kuona utekelezaji wake, pamoja na mambo mazuri ambayo yamefanyika, inahitaji speed ya kukimbia tu ili kuweza kuitimiza mipango ya wananchi ili waweze kupata fursa ya maendeleo katika maeneo yao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nafasi hii ya mchango wangu nilipenda kuishauri hivyo Serikali katika maeneo hayo ya uwekezaji kwenye kilimo, kwenye mifugo, kwenye mambo ya afya kuhakikisha kwamba tunaelekeza fedha nyingi ili Watanzania waweze kunufaika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana kwa nafasi. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027
MHE. JAPHAEL M. LUFUNGIJA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru kwa nafasi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumshukuru Mungu kwa kibali cha leo cha kuweza kusimama Bungeni, nikitoa mchango wangu katika Wizara ya Maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee nimshukuru sana Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais shupavu kwa nia njema ya kuwakomboa Watanzania hasa kwenye jambo kubwa hili la upatikanaji wa maji nchini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie fursa hii kumshukuru sana Waziri, Jumaa Aweso pamoja na mdogo wangu engineer Kundo kwa kazi nzuri wanazozifanya lakini wasaidizi wao; Katibu wa Wizara lakini nimshukuru engineer wangu wa Mkoa wa Tabora, ndugu yangu Kapufi pamoja na engineer wa RUWASA kule Kaliua ndugu yangu Mapambano.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Ulyankulu, lenye takribani wananchi 400,000, tunayochangamoto kubwa yam aji. Pamoja na kazi nzuri za kutuanzishia miradi saba inayotekelezwa kwenye jimbo hilo, yenye thamani ya shilingi 6,127,500,000 tunaishukuru Serikali kwa bajeti hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kati ya majimbo ya Mkoa wa Tabora 12, Jimbo la Ulyankulu ni jimbo pekee ambalo halina mradi wa maji ya Ziwa Victoria, maji hayo yamekuja mapaka eneo la Ushetu yakavuka yakaenda Kaliua, yamezunguka yakaja Urambo na yakaja Uyui. Tunao mradi mmoja tu mkubwa wa Bwawa la Ichemba, lililotengewa fedha shilingi bilioni 3.883. Mradi huu unatakribani ya miaka 10 sasa, ulianza kutekelezwa mwaka 2015 mpaka sasa mradi huu una 10%.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwombe Mheshimiwa Waziri, mimi ninakuamini, ninakukubali kwamba ni mtu usiependa kuzinguliwa, lakini ninaona kama watu wa Ulyankulu ni kama unawazingua hivi. Nikuombe mdogo wangu Mheshimiwa Jumaa Aweso, tumezungumza na wewe, ongeza kasi ya utekelezaji wa mradi huu, hatuna mradi mwingine wenye matumaini kwa wananchi hawa. Wananchi wa Jimbo la Ulyankulu kwenye hizo kata mpaka sasa pamoja na masika hii dumu la lita 20 wananunua shilingi 1,000 ni jambo ambalo ni hatari sana, nikuombe Waziri uweze ku-support mradi huu uweze kutekelezwa kwa kasi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini haitoshi, tunayo miradi ya Wizara ya Kilimo, tunayo miradi miwili kwenye Kijiji cha Konanne pamoja na Kijiji cha Mwendakulima eneo la Uyoa. Niwaombe ikikupendeza unganisha na wewe kwenye hiyo miradi ili kuipanua miradi hii iweze kwenda mashambani, lakini mingine iende kwenye mifugo na mingine itumike kwa ajili ya maji. Tunao uhaba mkubwa sana wa maji kwenye jimbo letu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kibaya zaidi Mto Igombe ambao unapeleka maji Ziwa Malagarasi kila wakati unapitisha maji mengi, sisi tunayaona kwa macho. Tuwaombe ikiwapendeza muone haja ya kukinga Mto Igombe ili sisi tuweze kupata maji ya kutosha yanayoweza kuhudumia jimbo zima kwa ujumla. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ipo miradi inayoendelea, nikuombe sana upo mradi unaotekelezwa kwenye Vijiji vya Seleli, Mwendakulima, Mwongozo, Uhindi, Kanindo, Kaswa, Sungwa, Ikonongo na Usigala. Mkadarasi alishafanya kazi yake, lakini changamoto ni malipo, nikuombe Mheshimiwa Waziri, mkandarasi na baadhi ya wazabuni walipwe ili kazi ziweze kufanyika.
Mheshimiwa Waziri, wananchi wa Jimbo la Ulyankulu umeniahidi mimi mwenyewe kwamba baada ya Bunge tutakwenda pia. Nikuombe Mheshimiwa Waziri, wewe na Naibu wako ujipange kwenye hili ili kwenda kutoa ufafanuzi vizuri juu ya suala la maji. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaombe Mawaziri wote; kumekuwa na changamoto kwenye wilaya moja yenye zaidi ya jimbo moja, jimbo ambalo halitoki makao makuu ya jimbo linasahaulika sana, aidha, kwa kutembelewa na kwenye bajeti. Ukiwa Tabora unanyooka na barabara moja inayokwenda Ulyankulu, nikuombe miaka mitano wananchi wamekosa kuona viongozi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaombe Mawaziri, eneo hilo sasa la Jimbo la Ulyankulu tufungue mlango sasa wa kupata taarifa za viongozi wa Serikali hasa Mawaziri na Naibu Mawaziri, ninawakaribisha. Ikumbukwe tu kwamba, Jimbo la Ulyankulu ndio jimbo lililopigania pia uhuru wa nchi hii, ukimsikia Mtemi Mirambo, ametokea pale ni kati ya watemi maarufu nchini.
Kwa hiyo, nikuombe na mimi mtambue tu kwamba na mimi ni chifu, utakapokuja Waziri na Naibu Waziri, nitakufikisha kwa Chifu Mirambo na kwangu kwa chifu mwenyewe ukashuhudie kazi nzuri zinazofanyika kwenye eneo hilo ukaweze kupata baraka hizo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vipo vijiji ambavyo vilifanyiwa utafiti wa uchimbaji wa maji, lakini mpaka sasa havijafanyiwa uchimbaji wa maji kwa ukosefu wa fedha. Nikuombe Waziri, vipo vijiji 13, nikuombe sana kazi hiyo ya fedha zipatikane ili vijiji vikaweze kuchimbiwa; Kijiji cha Ilege, Usonga, Mwendakulima, Ulanga, Utantwamke, Ibambo pamoja Ikonongo na Sungwa yenyewe.
Mheshimiwa Waziri, nikuombe sana uweze kutoa fedha kwenye maeneo hayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapozungumzia maji, maji ndio yamebeba kila kitu, maji ndio yamebeba kila kitu Mheshimiwa Waziri, nikuombe sana katika miradi hii ambayo umetupa miradi saba, kasi ya maji ni ndogo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazo sekondari 17, watoto wa shule wanatembea na vidumu kwenda shuleni. Tunazo shule za msingi zisizopungua 64, watoto kila wakati wanatembea na vidumu vya maji, wewe ndio mwarubaini wetu, tukuombe sana Mheshimiwa Waziri uone umuhimu wa kutu-support, lakini haitoshi tufikirie pia kwenye mpango wa Ziwa Victoria, kwa sababu Ulyankulu tumekaa kama ambavyo jengo hili la Bunge lilivyojengwa, sisi tupo katikati. Ukiizunumza Uyoa, ukiizungumza Uloa naizungumzia kama ambako walipo mwisho wa viti vya Bunge na upande wako kwa maana ya Kaliua. Sisi hapa katikati ndio tumebaki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwombe sana Mheshimiwa Waziri pamoja na watendaji, ninayoimani kubwa sana na wewe kwamba jambo hili ukisimama vizuri tunaweza tukayapata haya maji ya Ziwa Victoria. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi inayoendelea nimeiona, kuna mradi kwenye vijiji vya Sungwa, Ikonongo, Usigala yenye thamani ya shilingi milioni 957.1 kasi yake Mheshimiwa Waziri ni ndogo, tukuombe sana kasi iendelee kutekelezwa, mradi huo upo 15%. Ni kama ambavyo ulivyo mradi wa bwawa la Ichemba, upo 10% miaka 10, lakini cha kusikitisha Mheshimiwa Waziri, nimeangalia kwenye hotuba yako, mradi wa Bwawa la Ichemba sisi kwenye jimbo tunatambua utahudumia kata tisa na vijiji 27, lakini kwenye hotuba yako umeonesha kwamba utahudumia kata saba na vijiji 22, ninaomba wakati wa kuhitimisha hotuba yako uweze kuwaeleza Wana-Ulyankulu kwamba...
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
MWENYEKITI: Mheshimiwa muda wako umeisha.
MHE. JAPHAEL M. LUFUNGIJA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru sana, lakini nikushukuru na kukupongeza Mheshimiwa Waziri, ninaunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi