Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Rashid Mohamed Mtima (2 total)

MHE. RASHID M. MTIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuuliza swali la nyongeza katika sekta hii ya kilimo kwamba, ni lini Serikali itakamilisha designing ya mradi wa umwagiliaji eneo la Chikwedu, Chipalang’anda na Lipeleng’inyi ambalo utawezesha wananchi wa Vijiji vya Chihanga, Mpilipili, Chiunjila na Tarafa ya Mkunya jumla, ili kutumia maji ya Mto Ruvuma kuweza kumwagilia na kuongeza kipato kupitia sekta hii ya uzalishaji ya Kilimo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo nimejibu katika maswali niliyotangulia, ni kwamba miradi yote ya umwagiliaji ikiwemo hii ambayo ameitaja Chipalang’anda, (majina yake ni magumu kidogo), lakini miradi yote hii sisi kama Serikali tulishapewa maagizo na Mheshimiwa Rais kuingiza katika mipango, kuifanyia upembuzi yakinifu na usanifu wa kina ili tupate gharama halisi, na baada ya hapo tuweze kuitangaza ili iweze kufanyiwa kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, at least kwenye suala la miradi ya umwagiliaji, kwa sababu ni ajenda kubwa ya Serikali ya Awamu ya Sita, niseme tu kwamba haya ni maelekezo ya Mheshimiwa Rais, na sisi jukumu letu ni kutekeleza. Kwa hiyo nimwondoe tu shaka Mheshimiwa Mbunge kwamba tunalifahamu, na kazi inaendelea.
MHE. RASHID M. MTIMA: Mheshimiwa Spika, ninashukuru kupata nafasi ya kuuliza swali la nyongeza katika Wizara hii.

Mheshimiwa Spika, ni lini Serikali itatatua tatizo la upatikanaji wa simu katika maeneo yafuatayo katika Jimbo la Newala Mjini: Kata ya Nanguruwe, Kijiji cha Nanguruwe, Mnanje, na Mtawe; Kata ya Mcholi I, Kijiji cha Chikwedu na Chiunjila; Kata ya Namiyonga, Kijiji cha Nakachela na Mandumba; Kata ya Mnekachi Kijiji cha Kazamoyo; na Kata ya Mtumachi, Kijiji cha Mcholi Godauni? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Spika, kama ambavyo nimekuwa nikieleza katika majibu yangu kwamba Serikali imeandaa mkakati wa miaka mitano wa kuyafikia maeneo yote nchini ambayo yana changamoto ya mawasiliano. Kwa hiyo, ninamhakikishia Mheshimiwa Mbunge katika mkakati wetu wa miaka mitano maeneo yake hayo pia tutayafikia, lakini kwa sababu ameeleza kwamba ana changamoto kubwa, tutayapa kipaumbele wakati wa kutekeleza mkakati wetu huu wa Serikali, ninakushukuru.