Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Arif Suleiman Premji (2 total)

MHE. ARIF S. PREMJI aliuliza:-

Je, lini Serikali itakamilisha ujenzi wa Barabara kutoka Kijiji cha Hiyari kwenda Mkunwa - Makao Makuu ya Halmashauri kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapenda kujibu swali la Mheshimiwa Arifa Suleiman Premji, Mbunge wa Mtwara Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Barabara ya Hiyari – Mkunwa kilometa 10 ni sehemu ya Barabara ya Mkoa ya kutoka Msijute – Mnima – Nanyamba yenye urefu wa kilometa 78.75, inayohudumiwa na Wakala wa Barabara (TANROADS).

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hii inajengwa kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha, ambapo hadi sasa jumla ya kilometa mbili zimejengwa kwa kiwango cha lami kuanzia eneo la Msijute. Sehemu iliyobaki ya barabara hii itajengwa kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha, ahsante.
MHE. ARIF S. PREMJI aliuliza:-

Je, Shule ngapi za kidato cha tano na sita zimejengwa katika mwaka wa fedha 2025/2026 hadi kufikia robo ya pili?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, ninaomba kujibu swali la Mheshimiwa Arif Suleiman Premji, Mbunge wa Jimbo la Mtwara Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imekuwa ikijenga shule mpya za kidato cha tano na sita au kuongeza miundombinu katika shule za sekondari zilizopo ili kuzipandisha hadhi, kupokea wanafunzi wa kidato cha tano na sita, kisha kupata usajili rasmi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2025/2026 Serikali imetoa shilingi billioni 23.8 kwa ajili ya ujenzi wa madarasa 318, mabweni 116, matundu ya vyoo 542 katika shule 68 za sekondari ili kuziongezea uwezo wa kupokea wanafunzi wa kidato cha tano na sita. Aidha, hadi Aprili, 2026 shule 80 zenye uwezo wa kupokea wanafunzi 6,400 wa kidato cha tano na sita zimesajiliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2026/2027 Serikali imetenga shilingi billioni 27.5 kwa ajili ya ujenzi wa mabweni 273, madarsa 1,094 na matundu ya vyoo 1,645 katika shule 91 za sekondari kwa ajili ya wanafunzi wa kidato cha tano na sita. Ahsante.