Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027
MHE. YOHANA S. MSITA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana kwa kunipatia nafasi ya kuwa mchangiaji wa kwanza jioni hii. Ninaomba nichukue nafasi hii tena kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujaalia afya na uzima, lakini kuwashukuru sana wananchi wangu wa Jimbo la Itigi kwa kuendelea kuniombea, ninawaahidi kuitenda kazi kama inavyotakiwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kumpongeza sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi kubwa ambayo ameendelea kuifanya katika Sekta ya Maji. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninampongeza pia kijana mahiri kabisa Mheshimiwa Jumaa Aweso pamoja na Naibu wake na Katibu Mkuu. Kwa kweli Wizara hii ya Maji wanaitendea haki. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaona ari na nguvu na moyo walionao wa kufanya kazi. Changamoto ambayo ninaiona ni upatikanaji wa fedha. Tunakubaliana sote hapa kwamba maji ni uhai; pasipo maji hakuna maisha. Sasa, kama ndivyo Wizara hii ya Maji lazima tuipe kipaumbele sana, tuhakikishe fedha zote ambazo zinatakiwa kufika ndani ya Wizara hii zinafika kwa wakati. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa Mkoa wa Singida bajeti iliyopita ilitengewa jumla ya shilingi 10,000,000,000 kwa ajili ya maji. Mpaka kufikia mwezi Machi ilishapokea jumla ya shilingi bilioni 1.6 tu pekee. Hii maana yake nini? Maana yake ni kwamba, miradi mingi ya maji haijatekelezeka. Katika Jimbo la Itigi viko vijiji havijawahi kuonja ladha ya safi na salama, kwa maana ya maji ya bomba. Vijiji kama Ipangamasasi Kata ya Idodyandole, Mnazi Mmoja, Tulieni, Kalangali, Chabutwa, Ipalalyu na Mgandu, vijiji hivi havina miundombinu kabisa ya maji safi na salama. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tunaomba Serikali, tunapoipitisha bajeti tujitahidi kutafuta vyanzo vya fedha ili miradi hii ya maji iweze kukamilika na miundombinu iweze kujengwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Itigi lina changamoto kubwa sana ya upatikanaji wa maji chini ya ardhi. Mitambo imekuja na ninawashukuru watu wa Wizara. Mitambo imekuja imechimbwa; vijiji ambavyo maji hayajapatikana, Vijiji kama vya Mtakuja, Makale, Kayui, Chagutwa, Kintanula, Itagata, Mwamagembe, vijiji hivi lazima tuje na njia mbadala tuone namna gani tunaweza kuwasaidia wananchi wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vimechimbwa visima vingi, lakini maji hakuna. Sasa, inawezekana labda mitambo yetu uwezo wake ni mdogo, aidha, tunachimba mita ni chache zaidi. Tuje na mkakati mahsusi tuhakikishe kwamba vijiji hivi vinapatiwa maji. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye Jimbo la Itigi upatikanaji wa maji safi na salama ni 66% bado tuko chini. Ninaomba watu wa Wizara watuangalie kwa macho mawili, tuna changamoto kubwa sana ya upatikanaji wa maji katika Jimbo langu la Itigi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninasema tunayo mito, tunayo mabonde na kadhalika. Huu mpango wa kuchimba mabwawa, ninadhani kwenye Jimbo la Itigi uelekezwe kwa kasi kubwa sana, kwa sababu chini ya ardhi sehemu nyingi hatupati maji. Maeneo kama ya Mbugani, Doroto, Kitaraka, Itagata, Makale, maeneo ambayo maji hayapatikani, tuchimbe mabwawa yaweze kupunguza adha ya upatikanaji wa maji. Maji ya binadamu, lakini sisi Jimbo la Itigi pia ni wafugaji wazuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninawaomba sana, suala la uchimbaji wa mbwawa katika Jimbo la Itigi lipewe kipaumbele ili tuweze kuwasaidia wananchi wetu pamoja na mifugo yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, liko suala la vitendea kazi; Jimbo la Itigi hivi ninavyozungumza watu wa Maji pale Itigi Mjini wanayo pikipiki moja. Ile ni halmashauri, angalau basi tuongezewe pikipiki angalu zifike hata nne, lakini tupatiwe na gari ili watendaji wetu waweze kufanya kazi zao vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kumalizia, ninaiomba sana Wizara watuangalie watu wa Jimbo la Itigi kwa macho mawili ili tuweze kufika zile asilimia ambazo kwa mujibu wa Ilani ya Chama Cha Mapinduzi inatutaka tufike, hasa kwenye majimbo ya vijijini katika ile 85%. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kuunga mkono hoja na ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Katiba na Sheria kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027
MHE. YOHANA S. MSITA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana na mimi kunipatia fursa hii ya kutoa mchango wangu kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri wa Katiba na Sheria.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwanza kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ametujalia afya na uzima. Ninaomba kipekee sana niendelee kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa ambayo anaendelea kuifanya katika Taifa letu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona Mheshimiwa Rais ana moyo wa uzalendo, amejitoa kwa ajili ya kuwatumikia Watanzania. Nimpongeze pia Makamu wa Rais kwa kazi ambazo anaendelea kuzifanya, vilevile, Waziri wetu Mkuu kwa kazi kubwa ambazo wanaendelea kuzifanya nchini kwetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee sana ninaomba nimpongeze Waziri wa Katiba na Sheria, Dkt. Juma Homera pamoja na Naibu wake Zainab Katimba. Bila kumsahau Katibu Mkuu. Niseme tu mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria. Hakika watu hawa wanafanya kazi nzuri sana. Watu wa Wizara ya Katiba na Sheria wanapambana kweli kweli. Hongereni sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba uniruhusu sasa nianze kwanza kwa kutambua kauli mbiu ya Wizara hii ambayo inasema: “Haki, usawa na utawala wa sheria kwa watu wote.” Huu ndiyo msingi. Yako maandiko yanasema: “Kama misingi ikaharibika mwenye haki atafanya nini?” Tunapozungumzia Tanzania maana yake tunazungumzia Wizara hii ambayo ni Wizara mama ambao ndiyo msingi wa nchi. Wizara ya Katiba na Sheria ndiyo inabeba mambo yote, ndiyo inayoifanya Tanzania inaonekana katika sura hii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa uniruhusu nianze kuzungumzia msaada wa kisheria. Ninapozungumza msaada wa kisheria hapa ninazungumzia Mama Samia Legal Aid Campaign ambayo kwa kweli imefanya kazi kubwa sana. Niendelee kuwapongeza kwa kuendelea kufanya jambo hili zuri kwa ajili ya Watanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa ninapitia takwimu za huu msaada wa kisheria wa Mama Samia Legal Aid Campaign. Takribani wananchi 3,000,000 hadi kufikia Juni 2025 wamefikiwa na msaada huu wa kisheria, hilo ni jambo kubwa sana. Kazi kubwa imefanyika katika kutatua migogoro ya ardhi, kutatua migogoro ya mirathi na kadhalika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hili jambo si la kupuuzwa. Watu 3,000,000 ni wengi sana, lakini niendelee kutoa ushauri wangu kwa Wizara kwamba jambo hili liwe endelevu. Limewasaidia Watanzania wenzetu ambao wamekutana na changamoto mbalimbali wakati mwingine wao kushindwa kuelewana. Chombo hiki kikifika kinafanya utatuzi mzuri sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, misaada mingi ya kisheria imeendelea kuwepo ambayo kwa kweli takribani Watanzania milioni 7.4 wameendelea kusaidiwa katika kutatua changamoto mbalimbali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niseme tu mambo machache ambayo katika kutembelea miradi ambayo inasimamiwa na Wizara hii tumeona kuna mambo fulani ambayo yanahitaji kufanyiwa marekebisho kidogo au kuongeza kasi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema pale awali Wizara hii ndiyo msingi na Kamati katika kutembelea, tumetembelea miradi ikiwemo ya Jengo la Ofisi ya Taifa ya Mashtaka Mkoa wa Singida. Jengo hili ni jengo zuri, lakini ujenzi umekuwa wa kusuasua sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niiombe Serikali kama kweli tunataka kuelekea kwenye Dira ya 2050 kama ambavyo inasema katika ukurasa wa 30 kwamba Taifa la kidemokrasia linalozingatia utawala wa sheria, haki za binadamu na upatikanaji wa haki jamii lazima tuhakikishe tunaboresha miundombinu kwa kupeleka fedha ili miundombinu hii iweze kukamilika na wananchi wetu waweze kupatiwa huduma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tulitembelea pia Kituo cha Jumuishi cha Taasisi za Kisheria Mwanza. Hapa tumekuta fedha nyingi zimetumika, lakini jengo halijakamilika, bado linasuasua sana. Sasa kusuasua huku maana yake tunawachelewesha Watanzania kupatiwa haki zao na kupata huduma kwa ukaribu. Niiombe sana Serikali iendelee kukimbiza na kupeleka fedha pale.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia, tuligundua pale kuna changamoto kwa wajenzi wa Suma JKT. Hawa nao tumeona wanasuasua wameshapokea fedha karibu shilingi bilioni 2.9% lakini kwa kweli maendeleo ya kazi yalikuwa bado karibu 74%. Sasa hii ninaona ni jambo ambalo litatuchelewesha sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni kuhusu Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali ambapo kwa kweli hapa ninadhani tunahitaji kuongeza kasi sana na Serikali ije na mkakati maalum wa kuhakikisha kwamba tunafikia yale matarajio. Nimeona kwamba mashauri yalipokelewa karibu 10,398, lakini mpaka kufikia Februari, 2026 ni mashauri 604 tu ndiyo yaliyokamilika, ambayo ni sawasawa na 5.8%. Mashauri mengine bado yapo kwenye mchakato. Ninadhani Serikali ije na mpango mahususi wa kuhakikisha inaongeza kasi katika eneo hili.
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa
muda wa Mzungumzaji)
MWENYEKITI: Mheshimiwa ahsante kwa mchango wako. Muda wako umekwisha.
MHE. YOHANA S. MSITA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kuunga mkono hoja. Ahsante sana.