Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Asha Juma Feruz (3 total)

Mpango Elekezi wa Maendeleo wa Muda Mrefu 2026/2027–2050/2051, Mapendekezo ya Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2026/2027–2030/2031 na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Mwaka 2026/2027; na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali Katika Muda wa Kati ya 2026/2027 hadi 2028/2029.
MHE. ASHA J. FERUZ: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa nafasi hii na mimi niweze kuchangia katika hoja iliyopo Mezani ya Mpango wa Serikali. Nachukue nafasi hii kwanza kabisa ikiwa ni mara yangu ya kwanza kusimama na kuchangia, nawashukuru sana wapigakura wangu, Wajumbe wa Mkutano Mkuu wa UWT Taifa, kwa kunipa ridhaa kwa kura nyingi niweze kusimama hapa kuwa mwakilishi ninayewakilisha kundi la Vyuo na Vyuo Vikuu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia, nakishukuru sana chama changu pendwa, Chama Cha Mapinduzi, kwa kuniteua kuwa mwakilishi katika nafasi hiyo ndani ya Bunge lako Tukufu. Ninachukua nafasi hii pia, kumshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa ushindi mkubwa alioupata katika Uchaguzi Mkuu tulioufanya Oktoba, 2025.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile nachukua nafasi hii pia, kuwapongeza Mawaziri wote tukiamini kwamba, sisi ni timu moja. Wao wako mbele kumsaidia Mheshimiwa Rais kutimiza malengo na mahitaji ya wananchi wanayoyatarajia katika Serikali yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa najielekeza katika mchango wangu. Kama alivyowasilisha Waziri wa Mipango asubuhi, amesema kuwa, mpango huu umeandaliwa kutokana na Hotuba ya Rais, Ilani ya Chama Cha Mapinduzi na matamko ya viongozi ambayo ndiyo kiu ya wananchi ambao ndiyo tunawawakilisha humu ndani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kupitia mpango huu mimi najielekeza katika maeneo matatu; eneo la kwanza ni ajira kwa vijana. Katika sensa tuliyoifanya, nguvu kazi ya Taifa ni watu 25,000,000 lakini katika watu 25,000,000 milioni 14,000,000 ni vijana, sawa na 55.6%. Nini mchango wangu sasa ninaotaka kuusema? Katika Ilani ya Chama cha Mapinduzi, ukurasa wa 21, Chama Cha Mapinduzi na Serikali yake ambayo imeundwa kimejielekeza kutengeneza ajira 8,500,000. Sasa Serikali kwa mpango huu mzuri waliotuletea ninaomba kutoa ushauri kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili tuweze kuwasaidia vijana katika maeneo yetu tunaowawakilisha hapa waweze kupata ajira rasmi na zisizo rasmi, tuisadie Wizara ya Ajira. Pamoja na Wizara ya Vijana kuweza kupata taasisi chache ambazo zitakuwa na kazi ya kutoa mafunzo ya muda mfupi kwa vijana, ili vijana hawa watakapotoka kwenye hizo taasisi ama vyuo tupate positive impact kwa muda mfupi kwenye jamii zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia, naishauri Serikali kutoa mafunzo mahsusi, ikiwemo ujuzi wa fani adimu (real skills) kwa vijana, ili kupata fursa za ajira ndani na nje ya nchi. Nchi yetu ina miradi mingi ya kimkakati, nikitoa mfano Mradi wa Bomba la Mafuta, zipo kazi tunasema kwa Kiswahili chepesi, mafundi mchundo. Hawa ni watu wanaohitajika sana. Hatuna sababu ya kwenda kuchukua watu hawa nje, ili waje wafanye kazi zile hali ya kuwa sisi tuna vijana wengi ambao bado hawajapata ajira. Kwa hiyo, tutumie ombwe hilo kuweza kuwapa vijana wetu ajira za ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia, nichangie kuendeleza kuzisaidia sekta binafsi, kuwawekea mazingira bora na mazuri ya kukuza mitaji yao, ili waweze kutoa ajira kwa vijana wetu. Kuwa na utaratibu maalumu wa knowledge transformation kutoka kwa wafanyakazi wa kigeni kwenda kwa wafanyakazi wa ndani, wazawa. Hii itatusaidia kupunguza kuajiri watu kutoka nje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuwe na mkakati wa kuanzisha na kuendeleza viwanda vidogo vidogo vijijini na kukuza ongezeko la thamani katika sekta za kimkakati ikiwemo uvuvi, misitu, kilimo na mifugo. Kufuatia hayo niliyoyachangia kwenye eneo la vijana tutakuwa tunajielekeza katika kuongeza ajira kwa vijana wetu, ajira rasmi na zisizo rasmi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sehemu ya pili ni eneo la ubunifu na utafiti. Ninapenda kuipongeza Wizara ya Elimu, kupitia Chuo cha UDOM, kuwa washindi wa shindano la vyuo 29 nchini katika masuala ya cyber. Hapa chuo chetu cha UDOM kimetuonesha umahiri mkubwa na kimetuvisha nguo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nawaombe Serikali tutengeneze misingi au mpango wa kudumu kuelekea bajeti inayokuja kuimarisha ubunifu na matumizi ya teknolojia za kidigitali katika huduma za kijamii, Serikali iwekeze zaidi katika kuwaendeleza na kuwaongoza wataalamu wa Artifical Intelligence, kwa maana dunia ndiko inakojielekeza. Hii itasaidia kukidhi mahitaji ya matumizi ya AI na pia, kuendana na hali ya kiuchumi kupitia ushindani wa sekta mbalimbali zinazotumia teknolojia hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia, nawapongeza Serikali kwa kuanza kutumia teknolojia hii kwenye baadhi ya taasisi za umma, kwa mfano, Mfumo wa E-File. Tumeanza hivyo, tunavyoendelea tutaendelea kupunguza ajira za watu. Kwa hiyo, sisi hatuna budi kuweza kujikita katika eneo fulani la Artificial Intelligence. Kama tunajikita kwenye maintenance, tujikite hapo, tusibebe yote kwa wakati mmoja, tuangalie focus yetu sisi, kama Taifa, tunakwenda wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu wa mwisho ni katika eneo la elimu. Nawapongeza sana Wizara ya Elimu, tumeanza vizuri. Wiki iliyopita nimeona Mheshimiwa Rais akifungua mpango wa KKK wa kuhamasisha suala la Kusoma, Kuandika na Kuhesabu kwa watoto wetu na amesisitiza mtoto asifike darasa la tatu hajui kusoma na kuandika, lakini sasa katika bajeti nimeona inaelekea shilingi trilioni 8.19 kwa 2026/2027. Ninataka kusema nini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi hapa najielekeza zaidi katika ongezeko la mikopo ya elimu ya juu. Ni kweli, udahili umeongezeka, 2020/2021 udahili ulikuwa 295,919; 2024/2025 udahili ukawa 361,257; bajeti ya mikopo ilikuwa shilingi bilioni 570 na sasa 2025/2026 shilingi bilioni 916.7; udahili wa 2024/2025 ulikuwa 248,331. Udahili huu umeweza kuwanufaisha wanafunzi 248,331. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunaweza kuona hawa wanufaika wa mikopo ni wale ambao wanaendelea, kwa maana ya first year, second year, third year, fourth year na fifth year, kwa zile kozi zinazokwenda mpaka miaka mitano na wale wapya. Kwa hiyo, tunaweza kuona kwamba, bado uhitaji wa mikopo ya elimu ya juu ni mkubwa, fedha haitoshi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuwasaidie Wizara ya Elimu na Bodi ya Mikopo kuweza kuongeza bajeti. Pili, tuweke mikakati thabiti ni namna gani tutakiongezea hiki chombo, bodi ya mikopo, kupata fedha. Kwa nini tusi-engage private sector ili hii fedha iongezeke?

Mheshimiwa Mwenyekiti, wahitaji ni wengi, watoto wa maskini wengi wamekosa mikopo na waliomaliza chuo wengi hawajaweza kurudisha. Kutegemea source moja ambayo ni ruzuku ya Serikali, kuuchunga huu mfuko wa bodi ya mikopo, ni kazi ngumu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tuwaongezee bajeti ili mipango iweze kufikia malengo ambayo tunahitaji. Sasa wanafunzi wetu wafundishwe ujuzi pamoja na vitu ambavyo vitawasaidia kwenda kujiajiri moja kwa moja. Wakishaajiriwa au kujiajiri moja kwa moja wataweza kurudisha fedha hizi na wengine wakanufaika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, ninaomba kuunga mkono hoja iliyowekwa Mezani. Mwenyezi Mungu atusaidie wote tufanye kazi vizuri. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027
MHE. ASHA J. FERUZ: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia katika Wizara hii ya Kilimo. Awali ya yote ninapenda kuchukua nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, hakika mama huyu amefanya mapinduzi makubwa sana katika sekta ya kilimo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue pia fursa hii kuwapongeza Waziri wa Kilimo, Naibu Waziri wa Kilimo, Katibu Mkuu wa Wizara hii pamoja na watendaji wote kwa kazi nzuri wanayoifanya ya kuhakikisha kuwa tunapata pembejeo, tunapata mbegu na tafiti zinafanyika, utafutaji wa masoko unafanyika, viuatilifu vinapatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba sasa nijielekeze katika mchango wangu leo. Mchango wangu wa kwanza nitauelekeza katika eneo la mikopo ya wanawake na vijana. Ninaomba Wizara hii sasa ichukue hatua za makusudi katika mikopo ya vijana na wanawake kupitia ule Mfuko wa AGITF.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba sana Wizara hii iangalie kwa jicho la kipekee vijana wetu wanaohitimu katika vyuo vikuu ambao wamesomea kozi za kilimo. Kama tunaweza kumpatia kijana huyu mkopo wa elimu ya juu kabla hana hata haya maarifa ya kilimo, basi kijana huyu niombe aangaliwe kwa jicho la tatu pale anapohitimu masomo yake katika course za kilimo anapokwenda kuomba mkopo katika Benki ya Kilimo ama taasisi zinazotoa mikopo hiyo, akopeshwe kupitia cheti chake. Kwa sababu tunaamini kijana huyu amepata maarifa na anaweza kwenda kuya-implement na akaleta tija. Kwanza itachochea ajira kwa vijana na pili tutapata uhakika wa wataalam ambao wana-practice kile ambacho wamejifunza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wangu wa pili niuelekeze katika mazao ya horticulture. Mazao haya tumekuwa tukipoteza 30% mpaka 40% katika post-harvest losses. Kwa hiyo, ninaiomba Wizara hii iangalie umuhimu mkubwa wa kuandaa cold rooms katika maeneo ya airport na bandarini. Mkulima au mwekezaji anatumia takriban dola 2,500 katika shipment anapokwenda kusafirisha mazao haya. Umuhimu wa cold room ni mkubwa, mazao ya mbogamboga na matunda tunapoteza pesa nyingi katika maeneo haya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa niishauri Serikali yangu tuangalie katika Bandari ya Mtwara, Tanga, Dar es Salaam, tuzifanye bandari hizi kuwa ni sehemu kubwa ya kujenga hizi cold room au zile warehouse za mazao ili ziweze kufanya usafirishaji mkubwa. Pia, niombe katika Uwanja wa Ndege wa Julius Nyerere, KIA, maeneo ya Tabora na Mwanza, tunaweza tukawekeza hizi cold rooms na zikatusaidia kuokoa pesa nyingi ambazo tunazipoteza kwa kupitia Bandari ya Mtwara.

Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wangu wa tatu katika Wizara hii, ninamwomba Mheshimiwa Waziri, tunauza mazao mengi yakiwa ghafi. Tuwekeze katika viwanda vidogo, vya kati na vikubwa ili tuuze end user products. Tukifanya hivyo tutakuwa tumeweka wigo mkubwa wa upatikanaji wa ajira kwa vijana, kwa jamii zetu. Hata yule mkulima na yeye ataona tija ya kile anachokilima kwa maana ya kwamba zao limelimwa hapa, limekuwa processed hapa, pesa za kigeni tutazipata, tutainua pato la Taifa na uchumi wa wananchi wetu utakua. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, ninaomba nitumie fursa hii kuunga mkono bajeti hii iliyoko mezani na niwatakie kila la heri watekelezaji. Hakika haya yote ambayo wametuletea yakitekelezeka vizuri wananchi wetu watafurahia na kuona kuwa kilimo kwao ni option ya kwanza, siyo ya mwisho baada ya kukosa option zote. Haya yote ambayo nimeyaongea yaende sambamba na uboreshaji wa miundombinu ya barabara. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027
MHE. ASHA J. FERUZ: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia hoja iliyopo mezani. Kwanza kabisa ninapenda kuchukua fursa hii kuipongeza sana Wizara kwa utekelezaji mzuri wa bajeti inayokwisha. Hakika Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na watendaji wote wamefanya kazi nzuri sana na tunaendelea kuwapa ushirikiano tufikishe malengo ya Dira ya 2050.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, nielekeze pongezi zangu kwa Wizara na hasa kwa Mheshimiwa Rais kwa kuweza kutoa fursa kwa upatikanaji na utoaji wa ujuzi kwa vijana katika vyuo vya elimu ya ufundi na mafunzo. Tulikuwa tuna vyuo 1414, lakini sasa tuna vyuo 1446, hii ni hatua kubwa sana. Mheshimiwa Rais ametoa fedha nyingi, amewekeza ili vijana wetu waweze kupata ujuzi na kuweza kujiajiri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulikuwa tuna vyuo vya ufundi 532, lakini tuna vyuo vya ufundi stadi 914. Unaweza kuona ni kwa namna gani sasa vyuo vyetu vimeongezeka, hata VETA pia, kutoka VETA 80 hadi VETA 145. Hakika hii ni hatua kubwa sana, tuna kila sababu ya kumpongeza Mheshimiwa Rais amefanya uwekezaji mkubwa, ambao utakwenda kutatua tatizo la ajira kwa vijana wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaipongeza pia Wizara kwa mpango niliouona kwenye bajeti ya 2026/2027, inakwenda kuwekeza fedha nyingi bilioni 250, kwa kuanzisha polytechnical colleges tano kubwa maeneo ya Morogoro, Kigoma, Mwanza, Mtwara na Unguja. Hakika wameyaishi maono ya Mheshimiwa Rais, tunawatakia utekelezaji mwema na kwa kutangulia tu niseme hoja hii mimi itaiunga mkono kwa asilimia mia moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niielekeze mchango wangu wa ushauri na maoni katika eneo la Bodi ya Mikopo. Bodi hiyo wakati inaanza ilianza kwa 70,000,000,000 sasa tuna 917,000,000,000 tulikofikia. Mchango wangu ninauelekeza kuhusu mageuzi ya Bodi hii ya Mikopo. Kweli bodi inafanya kazi kubwa, lakini uhitaji wa wanafunzi kupata mkopo ni mkubwa. Fedha ama ruzuku tunayoipata haitoshelezi kuwapa wahitaji wote. Sasa ninashauri nini kifanyike.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza Bodi hii tubadilishe kutoka kwenye Bodi ya Mikopo kwenda kwenye Mfuko, ili tuweze kuipatia sheria Bodi hii au Mfuko huu tutakaouanzisha, uweze kujitanua katika eneo la kupata mapato. Kitendo cha kuendelea kusubiri chanzo kimoja cha fedha kinafanya watoto wa wanyonge, watoto wa wakulima kukosa mkopo. Tukiifanya Bodi hii kuelekea katika Mfuko, kwanza tutaipa nafasi ya kuanzisha vyanzo vyake vingine vya mapato, kwa hali iliyoko sasa hivi bodi haijitoshelezi katika utoaji wa huduma na inategemea ruzuku ya Serikali. Pia, haitumii fursa za wawekezaji na ubunifu za kifedha zilizopo nchini. Hakuna engagement ya private partnership. Tukifanya hivyo kubadilisha kutoka kwenye Bodi kwenda kwenye Mfuko itatusaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuangalie mfano, jana Mheshimiwa Aweso alitupa mfano wa namna Tanga walivyoweza kutumia maji na kuweka bonds wakapata faida. Sisi tunaweza kutumia kwenye elimu, lakini pia tuangalie Mfuko wa Bima ya Afya, watu wanawekeza baadaye anaweza kutibiwa. Pia, kwenye elimu mtu anaweza akawekeza kuanzia mwanzo, akaja akatumia mbele kule, lakini pesa ile inavyoingia itaendelea kusaidia watu wengine ambao wakati huo bado wanahitaji mkopo na wakasoma vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwanafunzi ada yake ni shilingi milioni nne, lakini bodi inampa shilingi laki saba au laki sita. Mtoto huyu wa maskini anashindwa kuendelea na masomo, kwa sababu ule mkopo alioupata katika ada yake haujafika hata nusu na mzazi hawezi kuhimili hizo gharama. Tunaendelea kusisitiza wanafunzi wasome sayansi, akienda kusoma labda fani za udaktari, ada ni kubwa, kwa hiyo tunakuwa hatumsaidii huyu mtoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni heri sasa tujielekeze mkopo wa wanafunzi. Ninajua katika pesa ya kujikimu ile boom wanapata sawa, lakini kwenye ada pesa ni ndogo, wanafunzi wanashindwa kujikimu. Kwa hiyo, ninashauri hapo kwenye pesa ya ada atleast tuwape nusu ya ada, hiyo ndiyo namna ya kumsaidia mwanafunzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu wa pili niuelekeze kwa wahadhiri. Wahadhiri waliopo chini ya TCU na wahadhiri waliopo chini ya NACTVET, wahadhiri hawa wanatofautiana maslahi. Mhadhiri wa TCU na Mhadhiri aliyepo chini ya NACTVET wanatofautiana hata mshahara, lakini wote ni wahadhiri. Ninazungumza kwa upande wa Wahadhiri Waandamizi, madaktari, associate professors and professors. Hii siyo sawa, kazi ya hawa watu wote ni kazi tatu za msingi. Kazi ya kwanza ni kufundisha, kazi ya pili ni kufanya tafiti na kazi ya tatu ni kutoa machapisho. Wote waliopo TCU na walioko na NACTVET wanafanya kazi hizi, kwa nini, kwenye maslahi tuwatofautishe? Mimi binafsi ninaona iko haja ya Serikali kufanya marekebisho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, watu hawa pia wanatofautiana hata kwenye muda wa kustaafu. Hawa watu waliopo chini ya TCU wanastaafu wakiwa na miaka 65, lakini yule aliopo chini ya NACTVET anastaafu kwa miaka 60. Kwa nini? Ninaomba Wizara ya Elimu washirikiane na Wizara ya Utumishi, kuona ni namna gani eneo hili linarekebishwa. Hii inawafanya watumishi hawa waliopo chini ya NACTVET wanakuwa wanyonge, tunawadogosha, lakini tunaamini kwamba taaluma zao zinaisaidia jamii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa wahadhiri ambao wapo chini ya NACTVET wakichapisha machapisho yao kwenye tovuti ambazo vyuo viko chini ya TCU, machapisho yao yanakataliwa yanakuwa dropped. Kwa nini? Si sawa, sisi wahadhiri tunaona hii haiendi sawa. Tuone haja na sababu sasa ya kurekebisha eneo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii pia kushauri Serikali itoe jicho la tatu, katika vyuo ambavyo vinatoa kozi ya afya. Nitatoa mfano Chuo cha MUHAS, hakina hospitali yake inayoimiliki na ni chuo cha Serikali. Ni kweli wanafunzi wa MUHAS wanategemea Hospitali ya Muhimbili na sote tunafahamu kuwa, Muhimbili ni taasisi inayojitegemea na MUHAS ni taasisi inayojitegemea. Kwa hiyo, iko haja sasa, ninashauri Serikali ione umuhimu wa kuipa MUHAS, Hospitali ya Mloganzila kama hospitali yao ya mafunzo. Hii itasaidia kuwapa wanafunzi nafasi ya kujifunza kwa vitendo vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, wapo wanafunzi ambao hawawezi kufanya mitihani ya mwisho, wakizuiliwa na uongozi wa vyuo vyao kwa kigezo cha kukosa ada. Hii si sawa. Haki ya mwanafunzi ni katika kusoma pamoja na kufanya mitihani yake. Hili lipo Mheshimiwa Waziri. Vipo baadhi ya vyuo vinazuia wanafunzi kufanya mitihani ya mwisho, end of semester exams kwa kigezo cha kwamba hajamaliza ada. Upo mchakato mrefu katika kusoma, kuna tests, kuna assignemts, walikuwa wapi kuwabana kule. Mwanafunzi akajibana, anafika end of semester kufanya mtihani anazuiliwa. Kwa hili, tunaona haliendi sawa na wanafunzi pia waangaliwe, kwa sababu ndiyo wataalam tunaowazalisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine katika eneo hili la wanafunzi, vipo vyuo vinatoa kada ambazo hazipo kwenye Sekretarieti ya Ajira. Mwanafunzi ameomba chuo, Serikali imemkubalia, ameomba mkopo, akapewa mkopo, akasoma akamaliza. Matarajio yake ni kuajirika, anapoingia kwenye Sekretarieti ya Ajira, anakuta kada aliyoisomea haipo. Anayeidhinisha kada hizi ni sisi Serikali, kwa maana ya kwamba Wizara ya Elimu, ndiyo wanatoa ruhusa ya kwenda ku-implement ile kozi ambayo inafundishwa kwenye chuo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niwaombe Wizara ya Elimu pamoja na Wizara ya Utumishi washirikiane, zile kada ambazo hazipo kwenye Sekretarieti ya Ajira ziingizwe. Ni maumivu makubwa kwa mwananchi ama mzazi kule kijijini kwetu, ambako anamsaidia mwanafunzi, kuweza kusoma, anamaliza, ana matarajio makubwa, halafu mwanafunzi yule haajiriki inaumiza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya, ninaunga mkono hoja na ninashukuru sana. (Makofi)