Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2025-2030 Session 2 Sitting 9 Energy and Minerals Wizara ya Madini 145 2026-02-06

Name

Chacha Mwita Wambura

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Geita Mjini

Primary Question

MHE. CHACHA M. WAMBURA aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuanzisha Kituo cha Kuongeza Thamani na Soko la Bidhaa za Dhahabu katika Mji wa Geita?

Name

Dr. Stephen Lemomo Kiruswa Mamasita

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Longido

Answer

NAIBU WAZIRI WA MADINI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuchukua hatua madhubuti kuimarisha uongezaji thamani wa madini katika Mkoa wa Geita ili kuhakikisha manufaa ya rasilimali madini yanabaki nchini. Kutokana na uzalishaji mkubwa wa dhahabu, mkoa huu umewekewa miundombinu muhimu ikiwemo kiwanda kikubwa cha Kusafisha Dhahabu vya Geita Gold Refinery (GGR) na African Eyes Refinery na pia kuna viwanda vidogo vya teknolojia ya kisasa ya uchakataji wa madini ikiwemo mifumo inayojulikana kama (CIP (Carbon in Pulp)/CIL (Carbon in Leach)) pamoja na Vituo vya Umahiri vya Lwangasa na Katente vinavyosimamiwa na STAMICO. Hatua hizi, kwa kuzingatia sheria na sera zilizopo, zimefungua fursa kwa wadau mbalimbali kushiriki katika soko la bidhaa za madini Mjini Geita ikiwepo masuala ya usonara.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kuweka mazingira wezeshi ya kiujuzi, kiuwekezaji na kisheria ili kuimarisha uongezaji thamani madini nchini. Aidha, Wizara kupitia Kituo chetu cha Jimolojia Tanzania (Tanzania Gemological Center) ambacho kiko Arusha) inaendelea kutoa mafunzo ya vitendo ya uongezaji thamani wa madini na kuandaa wataalam wa utengenezaji wa bidhaa zitokanazo na dhahabu, fedha na vito. Hivyo, nitoe wito kwa Mheshimiwa Mbunge kuwahamasisha vijana wa Mkoa wa Geita hususani Jimbo lake la Geita Mjini kuchangamkia fursa hizi ili kujiajiri, kuongeza kipato na kuchangia maendeleo ya Taifa. Ahsante sana.