Bunge la Tanzania
Jamhuri ya Muungano ya Tanzania
Name
Chacha Mwita Wambura
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Geita Mjini
Primary Question
MHE. CHACHA M. WAMBURA aliuliza:- Je, Serikali ina mpango gani wa kuanzisha Kituo cha Kuongeza Thamani na Soko la Bidhaa za Dhahabu katika Mji wa Geita?
Supplementary Question 1
MHE. CHACHA M. WAMBURA: Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kumpongeza Mheshimiwa Naibu Waziri wa Madini kwa majibu yake mazuri, lakini niseme tu kwamba wote humu ndani tunajua kwamba tunazalisha dhahabu nyingi Tanzania na hususani katika Mkoa wetu wa Geita, lakini dhahabu yote hii tunai-export, tunaisafirisha kwenda nje bila kuitengenezea vifaa vinavyotokana na dhahabu. Tukiweza kutengeneza vifaa hivi kama pete, mikufu na vinginevyo ambavyo vinatokana na dhahabu tutaenda kuongeza ajira, mapato, lakini pia tutakuwa sasa tunatengeneza Tanzania tuna-export, tutategemea tutopata wageni, lakini tutapata watalii.
Mheshimiwa Spika, swali la kwanza; je, Serikali ina mpango gani mahsusi wa kuhakikisha kwamba tunaanzisha kituo maalum cha utengenezaji hivi vitu ambavyo vinatokana na dhahabu ili basi tuweze kuhakikisha kwamba vijana na wajasiriamali wa Geita wanaweza kuhusika moja kwa moja kwenye mnyororo huo wa utengenezaji wa vitu hivi?
Mheshimiwa Spika, swali la pili; endapo itatokea Serikali haina mpango wa moja kwa moja wa kuanzisha kituo hiki, je Serikali iko tayari kushirikiana na sekta binafsi au Halmashauri ya Manispaa ya Geita kuwawezesha kuanzisha vituo hivi, maana ninaamini kabisa kwamba kwenye Geita na Taifa hili litaenda kuwa na faida kubwa? (Makofi)
Name
Dr. Stephen Lemomo Kiruswa Mamasita
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Longido
Answer
NAIBU WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Spika, awali ya yote nimpongeze sana Mheshimiwa Chacha kwa maswali yake mazuri na pia nimkaribishe katika Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kwa sababu nina taarifa kwamba hivi karibuni amepata kuelekezwa awe Mjumbe wa Kamati hiyo. Ninajua kwamba ni Engineer mwenye uzoefu na tunahitaji kuvuna hazina ya elimu aliyonayo katika Wizara ya Madini.
Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, nijibu sasa maswali yake kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, viwanda vya kuchakata madini na kutengeneza bidhaa za mlaji wa mwisho (end user products). Tayari zipo katika sehemu mbalimbali nchini kama nilivyoelezea kwenye majibu ya swali la msingi, lakini kwa upande wa huko Geita sasa na kwa sababu Mheshimiwa Mbunge anataka kujua hasa bidhaa zinazotokana na dhahabu ni kweli kwamba sasa hivi dhahabu nyingi inachakatwa, wanachoma, wanatengeneza zile ground bars na zinauzwa hivyo hivyo ila ni kwa Geita tu na baadhi ya maeneo mengine nchini, lakini tayari tuna viwanda vinavyochakata dhahabu na kutengeneza bidhaa za dhahabu.
Mheshimiwa Spika, moja ya mfano hai ambao upo na hata Wanageita wanaweza kwenda kujifunza ni Kiwanda cha Banjul Limited kilichoko Dar es Salaam ambacho kinafanya biashara ya kuchakata madini ya dhahabu na kuuza dhahabu nje kama wanavyouza wengine, lakini pia wanatengeneza vidani, mikufu, pete, bangili, lakini siyo ya dhahabu tu na madini mengine mbalimbali ikiweko madini ya metali pamoja na madini ya vito.
Mheshimiwa Spika, nitumie nafasi hii pia katika kujibu swali lake la pili kumwelekeza Mheshimiwa Mbunge, ashauriane na Halmashauri yake maana na yeye ni Mjumbe Halmashauri ya Geita siyo maskini, wakitaka kuanzisha kiwanda cha kuongeza thamani ya madini ya dhahabu na kutengeneza bidhaa za mlaji wa mwisho, sisi kama Wizara tuko tayari kutoa ujuzi na elimu kwa kuwaletea wataalam waweze kuanzisha kiwanda ambacho kitahakikisha kwamba dhahabu ile inatengenezewa bidhaa mbalimbali zinazoweza kutumika nchini na Watanzania wote, siyo lazima kuuza bidhaa ambazo zimechakatwa tu kwa asilimia Fulani.
Mheshimiwa Spika, tunaweza kutengeneza bidhaa za mlaji wa mwisho na wako wengi ambao ninapenda kuwapongeza wanaotengeneza bidhaa za madini ya vito hasa kule Arusha ambako kuna kile chuo chetu cha TGC, lakini pia kuna wadau mbalimbali katika mikoa mbalimbali nchini, Mererani pia wanafanya hivyo katika madini ya Tanzanite na Dar es Salaam kuna watu binafsi ambao wanajishughulisha na biashara hiyo.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, sisi tuko tayari kama Wizara kuiwezesha Halmashauri ya Geita kwa kuwapa utaalam ili waweze kuanzisha kiwanda cha kuchakata madini au kituo kikubwa kama kile cha Tanzanite City Center.
Name
Fadhili Fabian Ngajilo
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Iringa Mjini
Primary Question
MHE. CHACHA M. WAMBURA aliuliza:- Je, Serikali ina mpango gani wa kuanzisha Kituo cha Kuongeza Thamani na Soko la Bidhaa za Dhahabu katika Mji wa Geita?
Supplementary Question 2
MHE. FADHILI F. NGAJILO: Mheshimiwa Spika, ninashukuru kwa kupewa nafasi hii kuuliza swali la nyongeza. Mkoa wa Iringa unasemekana una maeneo yenye madini. Ukienda mfano Ihomasa, Ihandutwa, Sinai, Ulata, Mtera, Kitonga, Image na maeneo mbalimbali ya Mkoa wa Iringa. Swali, je, ni lini sasa Serikali wataifungua na kuipa kipaumbele Iringa ili mkoa huu ujulikane ni mkoa wa madini kwa kufanya mining survey lakini kutangaza maeneo yenye madini na kuwawezesha vijana kwa teknolojia ya kuchimba madini na kutengeneza mabilionea kutoka mkoa wa Iringa?
Name
Dr. Stephen Lemomo Kiruswa Mamasita
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Longido
Answer
NAIBU WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Spika, ninampongeza Mheshimiwa Mbunge kwa swali lake zuri na nimjulishe tu kwamba Iringa nayo ni mikoa yetu ya kimadini, wana madini ya aina mbalimbali na nimpe ushauri kwamba atembelee Kituo chetu cha Jiolojia (TGC) pale GST kwa sababu kuna kitabu ambacho huwa kinahuishwa kila baada ya miaka mitatu, kinachoeleza madini yanayopatikana katika kila eneo la nchi yetu ikiwepo Mkoa wa Iringa.
Mheshimiwa Spika, hatuishii hapo tu, tuna wachimbaji wadogo wengi pale Iringa, eneo la Nyakavangala ambalo lipo katika Jimbo la Mheshimiwa Lukuvi, tayari ambako kuna wachimbaji wa dhahabu na madini ujenzi. Hivyo ni wajibu wetu kama Wizara kuendelea kutoa elimu kwa vijana ili waingie katika sekta hii kwa wingi, kwa sababu madini haya yanaenda kubadilisha sura ya uchumi wa wananchi wetu na vijana hasa ambao wanahitaji ajira.
Mheshimiwa Spika, kwa suala la survey, sisi kama Wizara ya Madini kwa maelekezo ya Rais tuko katika mchakato wa mwisho wa kununua ndege yetu wenyewe ya kufanya survey, lakini pia tuna wadau wa sekta binafsi ambao wameanza kurusha ndege, wameanza kurusha helikopta, wameanza pia kurusha na zile ndege nyuki katika kutafuta madini yalipo katika maeneo mbalimbali ya nchi yetu. Tumeshafanya hivyo Shinyanga, wiki iliyopita na maeneo mengine.
Mheshimiwa Spika, ninaomba kuwasilisha.
Copyright © Bunge Polis 2026. All Rights Reserved