Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2025-2030 Session 3 Sitting 14 Finance Wizara ya Fedha 169 2026-04-22

Name

Lutengano George Mwalwiba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Busokelo

Primary Question

MHE. TIMIDA M. FYANDOMO K.n.y. MHE. LUTENGANO G. MWALWIBA aliuliza: -

Je, Serikali haioni umuhimu wa kuweka vivutio maalumu vya kikodi kwa vijana wanaoanza biashara ili kuchochea ajira na kukuza uchumi?

Name

Mshamu Ali Munde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Answer

NAIBU WAZIRI WA FEDHA (MHE. ENG. MUSHAMU A. MUNDE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Fedha, ninaomba kujibu swali la Mheshimiwa Lutengano George Mwalwiba, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, hilo ni swali No. 1,425. Kwanza ninampongeza sana Mheshimiwa Lutengano kwa kuwapambania sana wananchi wake wa Jimbo la Busekelo, na kwa namna anavyowasimamia. Pia ninafahamu Mheshimiwa Lutengano amekuwa akiwatetea sana vijana hata wakati akiwa anahudumu kwenye nafasi ya ukurugenzi kwenye mamlaka za Serikali za Mitaa ambapo tulikuwa wote huko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) inatekeleza mikakati mbalimbali ya kikodi inayolenga kukuza biashara ndogo ndogo, hususan za vijana, na kuhamasisha uingiaji wao katika uchumi rasmi. Miongoni mwa mikakati hiyo, ni utekelezaji wa Mfumo wa Kodi ya Makadirio (Presumptive Tax Scheme) unaolenga walipakodi wadogo wasiokuwa na kumbukumbu sahihi za mapato au vitabu vya hesabu, ambapo masharti yake ni mepesi na yanatabirika ili kuwahamasisha wafanyabiashara kusajili biashara zao na kuanza kulipa kodi kwa hiari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeanzisha utaratibu wa kipindi cha neema (grace period) kinachowaruhusu wafanyabiashara wapya kufanya biashara bila kulipa kodi kwa muda wa miezi sita tangu kuanza biashara. Hatua hizi zinalenga kuwapa wajasiriamali nafasi ya kukuza biashara zao bila mzigo wa kodi katika hatua za awali. Hii itaongeza ubunifu, kuvutia wafanyabiashara wa sekta isiyo rasmi kuingia kwenye mfumo rasmi, na hatimaye kuongeza mapato ya Serikali kwa njia endelevu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua umuhimu wa kutoa vivutio maalumu vya kikodi kwa vijana ili kuchochea uanzishaji wa biashara na ajira, ikiwemo msamaha wa kodi na viwango pungufu, huku ikiendelea kufanya tathmini ya athari zake ili kuhakikisha usawa, ufanisi wa sera, na uendelevu wa mapato ya Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kupitia Sheria ya Fedha ya Mwaka 2023 na maboresho yake ya mwaka 2024, Serikali pia inatoa ahirisho la kodi ya mapato (Corporate Income Tax) kwa kipindi cha miezi sita ya mwanzo kwa biashara mpya (start-ups), hatua inayolenga kusaidia biashara changa kukua na hatimaye kuwa walipakodi wakubwa na endelevu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kuwasilisha.