Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2025-2030 Session 3 Sitting 19 Enviroment Ofisi ya Makamu wa Rais Mazingira na Muungano 224 2026-04-29

Name

Catherine Canute Joachim

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. DKT. CATHERINE C. JOACHIM aliuliza: -

Je, Serikali imepata matokeo gani katika kupunguza uchafuzi wa mazingira tangu kuanza kwa katazo la matumizi ya mifuko ya plastiki mwaka 2019?

Name

Kwagilwa Reuben Nhamanilo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Handeni Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, ninapenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Catherine Canute Joachim, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na changamoto za uchafuzi wa taka za plastiki na athari zake, Serikali ilipiga marufuku uingizaji nchini, uzalishaji, usambazaji, uhifadhi, usafirishaji nje ya nchi na matumizi ya mifuko ya plastiki kuanzia tarehe 01 Juni, 2019. Matokeo ya katazo hilo ni pamoja na:-

(i) Kupungua kwa zaidi ya 95% ya uzalishaji na uingizaji wa mifuko ya plastiki nchini, ambapo imechangia kupungua kwa uzalishaji wa taka za plastiki katika maeneo mbalimbali nchini;

(ii) Kuongezeka kwa kiwango cha uelewa wa wananchi kuhusu madhara ya plastiki kutoka chini ya 40% mwaka 2018 hadi kufikia zaidi ya 85% mwaka 2026;

(iii) Kupungua kwa takribani 60% ya taka za plastiki katika maeneo ya fukwe za bahari na maziwa ambapo hatua hii imepunguza hatari kwa viumbe wa majini;

(iv) Kupungua kwa gharama za kuzibua mitaro ya maji machafu kwa wastani wa 30% mpaka 40%, kwani mifuko ya plastiki ilikuwa chanzo kikuu cha uzibaji wa miundombinu hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kupitia Bunge lako Tukufu ninaomba nitoe rai kwa wananchi kuendelea kuzingatia katazo la matumizi ya mifuko ya plastiki la mwaka 2019 kwa ajili ya kulinda afya na kuhifadhi mazingira yetu kwa maendeleo endelevu ya kizazi cha sasa na kijacho.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba kuwasilisha.