Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2025-2030 Session 3 Sitting 19 Water and Irrigation Wizara ya Maji 226 2026-04-29

Name

Alan Thomas Mvano

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kakonko

Primary Question

MHE. ALAN T. MVANO aliuliza: -

Je, lini Mkandarasi atakamilisha kuchimba na kujenga kisima cha maji katika Kijiji cha Kihomoka kama ilivyo kwenye mkataba wake?

Name

Kundo Andrea Mathew

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bariadi Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAJI alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji, ninaomba kujibu swali la Mheshimiwa Alan Thomas Mvano, Mbunge wa Jimbo la Kakonko, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ilipanga kuchimba visima vitano katika Wilaya ya Kakonko kupitia programu maalumu ya uchimbaji wa visima 900. Hadi sasa jumla ya visima vinne kati ya vitano vimechimbwa katika Kijiji cha Ruhuru viwili, Kihomoka kimoja, na Nyamtukuza kisima kimoja, ambapo kwa pamoja vina uwezo wa kuzalisha jumla ya maji lita 55,500 kwa saa.

Mheshimiwa Naibu Spika, visima hivyo baada ya kupata maji vimeendelezwa kwa kujengewa miundombinu rahisi ya kutolea huduma kwa wananchi (point source) na vinaendelea kutoa huduma iliyokusudiwa kwa wakazi wa vijiji hivyo. Hata hivyo kisima kimoja kilichokuwa kimepangwa kuchimbwa katika Kitongoji cha Centre B kilichopo Kijiji cha Kihomoka hakikuweza kuchimbwa. Hivyo, Serikali imekiingiza kisima hicho kwenye mpango wa programu ya vijiji 1,575 visivyokuwa na huduma ya maji ambayo inaanza kutekelezwa katika mwaka wa fedha 2026/2027.