Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2025-2030 Session 3 Sitting 17 Youth, Disabled, Labor and Employment Ofisi ya Waziri Mkuu-Kazi, Ajira na Mahusiano 191 2026-04-27

Name

Chacha Mwita Wambura

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Geita Mjini

Primary Question

MHE. CHACHA M. WAMBURA aliuliza:-

Je, upi mkakati wa kuunda ajira na kukuza uchumi wa vijana kupitia miradi ya uzalishaji na ujasiriamali ili kupunguza utegemezi wa sekta ya madini – Geita?

Name

Rahma Riyadh Kisuo

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA NA MAHUSIANO alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Ajira na Mahusiano, ninapenda kujibu swali zuri la Mheshimiwa Engineer Chacha Mwita Wambura, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ina mkakati wa kuunda ajira na kukuza uchumi wa vijana kwa kuwawezesha kushiriki katika miradi ya uzalishaji na ujasiriamali, sambamba na kupunguza utegemezi wa sekta ya madini.

Mheshimiwa Naibu Spika, kupitia Mradi wa Mageuzi katika Sekta ya Madini kwa Maendeleo Jumuishi na Endelevu (MBT), vijana 5,983 wamewezeshwa kwa kupatiwa leseni, mafunzo na mitaji, huku wachimbaji wadogo 658 wakipatiwa mafunzo kupitia Programu ya Taifa ya Kukuza Ujuzi katika mikoa ya kimadini ya Geita, Mbogwe na Chunya.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, Serikali inatekeleza mikakati jumuishi ikiwemo uratibu wa utekelezaji wa Sera ya Ajira ya Mwaka 2008 pamoja na sera nyingine za kisekta. Vilevile, utekelezaji wa programu za kuwawezesha vijana kama BBT na BBT-LIFE, pamoja na utoaji wa mikopo yenye masharti nafuu kupitia Halmashauri na Mfuko wa Maendeleo ya Vijana.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali pia inaendelea kukuza ujuzi wa vijana, kuratibu fursa za ajira ndani na nje ya nchi, na kuhakikisha masuala ya ajira yanajumuishwa katika mipango ya maendeleo, hatua zinazolenga kukuza fursa za ajira na kuimarisha uchumi wa vijana kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba kuwasilisha.