Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2025-2030 Session 3 Sitting 17 Finance Wizara ya Fedha 198 2026-04-27

Name

Tarimba Gulam Abbas

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kinondoni

Primary Question

MHE. TARIMBA G. ABBAS aliuliza: -

Je, kwa nini Serikali haitoi bei elekezi kwa makato ya huduma za Mobile Money ili kuwapunguzia gharama wananchi?

Name

Amb. Khamis Mussa Omar

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nominated

Answer

WAZIRI WA FEDHA alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu Swali Na. 198 la Mheshimiwa Tarimba Gulam Abbas, Mbunge wa Kinondoni, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imekuwa ikichukua hatua mbalimbali kuhakikisha kuwa huduma za miamala ya fedha kwa mitandao ya simu zinapatikana kwa gharama nafuu. Hatua hizi zimejikita katika kupunguza gharama za miamala ya kielektroniki, kuimarisha miundombinu ya mifumo ya malipo na kuweka mazingira rafiki ya kisera na kikanuni ili kuchochea matumizi ya huduma za kifedha za kidijitali na kupunguza gharama.

Mheshimiwa Naibu Spika, hatua zifuatazo zimechukuliwa kwa kipindi cha mwaka 2024 na 2025: -

(i) Mwezi Aprili, 2024 Benki Kuu ya Tanzania iliweka kikomo cha juu cha gharama ya muamala kwa Mfumo wa Malipo ya Papo kwa Papo na Mfumo wa Tanzania Automated Clearing House (TACH) kwa miamala kati ya benki na benki, ambapo gharama ya juu kwa muamala mmoja ni shilingi 2,000.

(ii) Mwezi Aprili, 2025, Benki Kuu ya Tanzania iliendelea kupunguza gharama za miamala ya kutuma fedha kidijitali, ikijumuisha miamala ya kuhamisha fedha kutoka simu kwenda akaunti za benki na kutoka benki kwenda simu kupitia mfumo wa malipo madogo na ya haraka. Gharama za miamala zimepunguzwa na kuwekwa ukomo wa shilingi 5,000 kwa miamala yote inayozidi shilingi 500,000, kwa miamala isiyozidi shilingi 500,000, mwongozo wa ukomo wa gharama kwa kiwango tofauti umeainishwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, Benki Kuu ya Tanzania imeendelea kutoa leseni kwa watoa huduma mbalimbali ili kuhakikisha ushindani katika sekta ya mifumo ya malipo ya kielektroniki. Hadi kufikia mwezi Machi, 2026, watoa huduma 113 walikuwa wameshapata leseni ya kutoa huduma za mifumo ya malipo nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Benki Kuu ya Tanzania inaendelea kushirikiana na watoa huduma wa mifumo ya malipo ya kielektroniki katika kufanya tathmini ya gharama za miamala na kuchukua hatua zinazofaa za kupunguza gharama ziada, bila ya kuathiri uthabiti na usalama wa mfumo wa malipo.

Mheshimiwa Naibu Spika, maelezo ya ziada tu ni kwamba, kwa ujumla bado Serikali inaendelea kutumia Sera ya Soko Huria na kuhimiza ushindani wa haki unaozingatia haki ya mlaji na uwazi wa kupatikana taarifa za bei kupitia Benki yetu Kuu, ambayo pia inatoa mwongozo wa bei na tozo mbalimbali.