Bunge la Tanzania
Jamhuri ya Muungano ya Tanzania
| Term | Session | Sitting | Sector | Ministry | Qn No | Date |
|---|---|---|---|---|---|---|
| 2025-2030 | Session 3 | Sitting 18 | Finance | Wizara ya Fedha | 213 | 2026-04-28 |
Name
Dickson Nathan Lutevele
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Mafinga Mjini
Primary Question
MHE. TIMIDA M. FYANDOMO K.n.y. MHE. DICKSON N. LUTEVELE aliuliza: -
Je, Serikali ina mkakati gani wa kuondoa Kodi ya 30% katika export ya Mazao ya Misitu ambayo imeua kabisa Viwanda?
Name
Amb. Khamis Mussa Omar
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Nominated
Answer
WAZIRI WA FEDHA alijibu: -
Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla ya marekebisho ya Sheria, kulikuwa na usafirishaji mkubwa wa mazao ya misitu nje ya nchi yasiyochakatwa au yaliyochakatwa kidogo na ni mfano wa magogo na Veneer sheets. Hivyo, mwaka 2025 Serikali ilifanya marekebisho kwenye Sheria ya Usafirishaji wa Bidhaa Nje ya Nchi, Sura 196 ili kutoza ushuru kwa kiwango cha 30% au shilingi 150 kutegemeana na kiwango kitakachokuwa kikubwa kwa kila kilo moja ya vinia inayotambulika kwa Tariff Heading 44.08 inayosafirishwa kwenda nje ya nchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ilifanya marekebisho hayo ili kulinda viwanda vya ndani katika kuhakikisha upatikanaji wa malighafi za viwanda vyetu vya ndani vinavyotengeneza bidhaa za mbao ikiwemo plywood na marine board. Pamoja na marekebisho hayo, Serikali pia ilifanya marekebisho kwa kuongeza ushuru wa forodha kwa marine board zinazoingizwa nchini kutoka 25% hadi 35% ili kuviongezea viwanda vyetu vya ndani ushindani dhidi ya bidhaa zinazoagizwa kutoka nje.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, Serikali imepokea changamoto aliyoieleza Mheshimiwa Mbunge kuwa hatua hii imeathiri baadhi ya Viwanda. Viwanda vinavyoweza kuathirika ni vile vinavyochakata mazao ya misitu bila kufikia hatua za mwisho za uzalishaji wa bidhaa za misitu kwa matumizi yaliyokusudiwa. Hivyo, Serikali inaendelea kujielekeza kwenye kutafuta suluhu ambayo haitaleta athari hasi kwenye sekta hii ndogo kutokana na hatua zinazochukuliwa ili kuilinda sekta hii muhimu katika uchumi wetu, na pia kwa kuhakikisha kuwa kuna uongezaji thamani wa mazao ya misitu kabla ya kuuzwa nje ya nchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itaendelea kufanya tathmini ya kina kupitia Wizara ya Maliasili na Utalii na Wizara ya Fedha ili kuona namna ya kurekebisha kodi hii pale itakapothibitika kuwa inazuia ukuaji wa viwanda badala ya kuvilinda, ili kuhakikisha mnyororo wa thamani wa misitu unamnufaisha mwekezaji na Taifa kwa ujumla.
Copyright © Bunge Polis 2026. All Rights Reserved