Bunge la Tanzania
Jamhuri ya Muungano ya Tanzania
Name
Stella Alex Ikupa
Sex
Female
Party
CCM
Constituent
Special Seats
Primary Question
MHE. STELLA I. ALEX K.n.y. MHE. MARIAM N. KISANGI aliuliza:- Je, wananchi wa Temeke wananufaikaje na uwepo wa Uwanja wa Taifa uliopo Wilayani humo?
Supplementary Question 1
MHE. STELLA I. ALEX: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Mheshimiwa Mariam anaishukuru Serikali kwa kujengwa kwa Uwanja huu wa Mkapa ambao unabeba watu wengi kwenye mechi mbalimbali zikiwemo mechi za Simba na Yanga na hivyo kuingiza mapato makubwa. Je, Serikali ina mpango gani wa kugawa sehemu ya mapato haya na kuyaelekeza kwenye huduma za jamii katika Jimbo la Temeke? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, Uwanja wa Mkapa na Uhuru unafanyiwa huduma mbalimbali ikiwemo kutengeneza bustani pamoja na usafi, lakini pamoja na huduma nyingine. Nini mpango wa Serikali kuwapa kazi hizi vijana wa Temeke wakiwemo vijana wenye ulemavu? Ahsante. (Makofi)
Name
Hamis Mohamed Mwinjuma
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Muheza
Answer
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA, NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru na nimshukuru Mheshimiwa Stella Ikupa, kwa niaba ya Mheshimiwa Mariam Kisangi, Mbunge wa Temeke ambaye anafanya kazi kubwa kwa ajili ya kuwapigania wananchi wa Temeke na ninamwombea Mungu aendelee kumtia nguvu na amtie moyo kwa ajili ya kuhakikisha wananchi wa Temeke wanapata kile ambacho walitarajia wakati wanamtuma kuwa Mbunge wao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kujibu maswali haya mawili mazuri ya nyongeza la kwanza lilikuwa kuhusiana na mgao. Mara nyingi Serikali haiandai matukio yanayofanyika katika Uwanja wa Benjamini Mkapa, yenyewe inatoa miundombinu hii kwa waandaaji ambao kwa mfano mechi za Simba na Yanga timu mwenyeji ndiyo ambayo inakuwa inakodishwa uwanja huu. Mapato yanayopatikana hugawanywa kwa utaratibu maalum ambao umekubalika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, 18% ya mapato hayo inakwenda kwama kodi ya ongezeko la thamani, asilimia tatu inakwenda kwa BMT, asilimia Nne inakwenda kwa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania, 15% inakwenda kama gharama za ukodishaji wa uwanja na asilimia Saba kwa ajili ya uendeshaji wa shughuli ile na asilimia Sita inakwenda kwa Chama cha Soka cha Mkoa wa Dar es Salaam. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wadau wote hawa moja ya mambo wanayoyafanya ni kuhakikisha wanarudisha kwa ajili ya shughuli mbalimbali zinazofanyika Tanzania na hasa kwa Manispaa ya Temeke ambayo uwanja huu umewekwa pale.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inachofanya kwa sasa ni kuhakikisha tunaendelea kuimarisha makusanyo haya ili kiwango ambacho kinagawiwa kwa wadau hawa ambao nao hurudisha kwa Manispaa ya Temeke na maeneo mengine mbalimbali kwa ajili ya huduma hasa za michezo kinaongezeka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunasimamia utaratibu wa kuhakikisha tunaendelea kukusanya mapato haya ili yawe na manufaa na tija kubwa zaidi kama ambavyo imekuwa ikitokea kwa wakati wote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hali kadhalika kwenye swali lake la pili, kuhusiana na huduma mbalimbali. Katika hili Serikali imetoa zabuni kwa makampuni ambayo yanatoa huduma mbalimbali zinazofanyika katika Uwanja wa Benjamini Mkapa wakati wa matukio yanayotokea pale. Tumetoa zabuni kwa makampuni ya ulinzi na makampuni ya usafi hali kadhalika. Kampuni za ulinzi tunao walinzi 25 pale, lakini tunao vijana 40 ambao wanafanya shughuli za usafi na wote hawa ni wakazi wa Manispaa ya Temeke.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hali kadhalika kuhusiana na kutenga kwa ajili ya watu wenye ulemavu moja kwa moja, hili ni wazo zuri na ninaomba nilichukue kwa ajili ya mashauriano na wenzangu kuona kama miongoni mwa vikundi vya wajasiriamali ambapo sasa hivi tunavyo vikundi vinne pale, kila kimoja kikiwa na wanachama 50, tuone kama tunaweza kutenga vikundi ambavyo vitakuwa vya watu wenye ulemavu kwa ajili ya kufanya shughuli mbalimbali panapokuwa na matukio kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru. (Makofi)
Name
Abdallah Dadi Chikota
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Nanyamba
Primary Question
MHE. STELLA I. ALEX K.n.y. MHE. MARIAM N. KISANGI aliuliza:- Je, wananchi wa Temeke wananufaikaje na uwepo wa Uwanja wa Taifa uliopo Wilayani humo?
Supplementary Question 2
MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru kwa kunipa nafasi. Uwanja wa Nangwanda Sijaona uliopo Mkoani Mtwara ni miongoni mwa viwanja ambavyo vinaingiza mapato makubwa sana mechi inapofanyika: Je, Serikali kwa kushirikiana na mmiliki wa uwanja huu ina mpango gani wa kufanya ukarabati mkubwa uwanja huu?
Name
Hamis Mohamed Mwinjuma
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Muheza
Answer
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru na nimshukuru Mheshimiwa Chikota kwa swali zuri la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Uwanja wa Nangwanda Sijaona haumilikiwi moja kwa moja na Serikali, ni uwanja wa miongoni mwa wadau wetu, Chama Cha Mapinduzi. Kama ambavyo nilishajibu mara kadhaa hapa, tunayo mazungumzo na Chama Cha Mapinduzi kuona namna ambavyo tunaweza kuhakikisha tunaweza kuvifanyia ukarabati kwa utaratibu unaofaa viwanja vingi ambavyo vinamilikiwa na taasisi hii na kuona namna ambavyo mapato yatafanyiwa mgawanyo baada ya uendeshaji kati ya Chama Cha Mapinduzi na Serikali ambayo itakuwa imefanya ukarabati wa viwanja hivi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo Uwanja wa Nangwanda Sijaona ni miongoni mwa viwanja ambavyo vipo katika fikra zetu. Tutakapokubaliana na wamiliki wa kiwanja hiki ambao ni Chama Cha Mapinduzi tutakwenda kukifanyia ukarabati na kuhakikisha kinakuwa katika hali nzuri kwa ajili ya kufanya shughuli za michezo
Copyright © Bunge Polis 2026. All Rights Reserved