Bunge la Tanzania
Jamhuri ya Muungano ya Tanzania
Name
Chief Thomas Mgonto Kitima
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Ikungi Mashariki
Primary Question
MHE. THOMAS M. KITIMA aliuliza: - Je, lini Serikali itaanza utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050?
Supplementary Question 1
MHE. THOMAS M. KITIMA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali madogo mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa dira hii inasema kwamba itawahusisha wananchi wote, kwa maana uchumi jumuishi na tunapoenda kuianza tarehe 01 Julai, 2026. Wananchi watahusikaje kwa sababu hakuna elimu ambayo imetolewa kwa umma ambayo itawafanya wawe sehemu ya mpango huu na sio wasindikizaji. Je, ni lini Serikali itatoa elimu kwa wananchi wote kabla hatujaanza kutekeleza?
Mheshimiwa Spika, swali la pili; ni kwa namna gani miradi ambayo itatumika kama benchmark ama miradi ya kielelezo tunapoanza kuitekeleza dira hii tutaanza nayo mwezi Julai, ili wakati tunaendelea basi tuwe tunafanyiana assessment kupitia hiyo miradi ambayo tunaenda kuanza kuitekeleza tutakapoanza kutekeleza dira hii?
Name
Laurent Deogratius Luswetula
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Kavuu
Answer
NAIBU WAZIRI WA FEDHA (MHE. LAURENT D. LUSWETULA) K.n.y. WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MIPANGO NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, kwanza nipende kumpongeza sana Mbunge wa Ikungi Mashariki, Mheshimiwa Thomas Kitima, kwa kuendelea kupambania sana wananchi wa jimbo hilo, lakini pia kama mjumbe makini katika Kamati yetu ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti.
Mheshimiwa Spika, nikianza na swali la kwanza; niseme kabisa moja ya majukumu ya Wizara yetu ya Mipango na Uwekezaji kupitia Tume ya Taifa ya Mipango kwanza ni kuratibu na usimamizi wa uchumi, kupanga mipango ya maendeleo, pamoja na kutekeleza mipango ya maendeleo ambayo tayari imeshakwisha kuidhinishwa. Hii ni pamoja na kukusanya, kuchakata pamoja na kufanya tathmini ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo ambayo tayari imeidhinishwa.
Mheshimiwa Spika, mimi niseme ni Naibu Waziri wa Fedha, na sisi kama Wizara ya Fedha, kwanza tumejidhatiti kuhakikisha kwamba Dira hii ya 2050 inatimizwa kwa 100%. Sisi tuko tayari kuhakikisha kwamba fedha ya aina yoyote ambayo inahitajika kulingana na mpango huu wa Dira ya 2050, tuko tayari kupeleka katika Wizara ya Mipango na Uwekezaji, kuhakikisha kwamba maono sasa ya mama yetu Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kuhakikisha kwamba uchumi wa nchi hii unafikia dola za Kimarekani trilioni moja ifikapo mwaka 2050, lakini pia wastani wa kipato cha mtu mmoja mmoja kufikia dola za Kimarekani 7,000 kwa mwaka.
Mheshimiwa Spika, kwa namna hiyo nimhakikishie kabisa Mheshimiwa Mbunge wa Ikungi Mashariki, sisi kama Wizara ya Fedha kwa kushirikiana na wenzetu wa Wizara ya Mipango na Uwekezaji, tuko tayari kuhakikisha kwamba mipango yote ambayo imo ndani ya Dira ya 2050 inatekelezwa bila kikwazo chochote kwa ukamilifu wake.
Mheshimiwa Spika, swali la pili ambalo ameuliza sasa ni kwa namna gani elimu kwa umma tunaenda kuifikisha huko. Kwanza niseme kabisa jambo hili la elimu kwa umma sio jambo la Serikali pekee yake, bali ni jukumu letu sisi kama Serikali, lakini pia na Wabunge wote ambapo tutakapokuwa tunakwenda kwenye majimbo yetu, ni lazima tuhakikishe ya kwamba tunatoa elimu kwa umma ili umma sasa uelewe kwamba Dira hii ya 2050 imebeba maono gani.
Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo, Dira ya Maendeleo ya miaka 25 kuanzia Julai 01, Dira ya Maendeleo 2050, kwanza na yenyewe kwa ukubwa wake, hatuwezi kuwakwepa sekta binafsi. Nazo tumezijumuisha kuhakikisha kwamba sekta binafsi zina-play role kubwa kutekeleza utekelezaji wa Ilani ya Dira ya Maendeleo 2050. Pia wenzetu wa Wizara ya Mipango, wana mpango mkakati mzuri sana wa kutoa elimu kwa umma kupitia platform mbalimbali ikiwemo makongamano, social media na vyombo vingine ambavyo vitahakikisha kwamba elimu ya utekelezaji wa Dira 2050 wananchi wanaielewa vizuri ili na wao waipokee kwa ajili ya utekelezaji wa dira hiyo.
Mheshimiwa Spika, ahsante na naomba kuwasilisha
Name
Faraji Buriani Nandala
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Ndanda
Primary Question
MHE. THOMAS M. KITIMA aliuliza: - Je, lini Serikali itaanza utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050?
Supplementary Question 2
MHE. FARAJI B. NANDALA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi ili nami niweze kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Spika, kundi la vijana ndio kundi lengwa katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025/2050 na Serikali imekuwa ikilielekeza kundi hili kwenda kufanya shughuli mbalimbali za kiuchumi ikiwemo kilimo pamoja na uvuvi.
Mheshimiwa Spika, kundi hili limekuwa likikabiliwa sana na changamoto ya mabadiliko ya tabianchi ambazo zimekuwa zikiathiri shughuli hizi za kiuchumi na kurudisha jitihada za vijana hawa.
Mheshimiwa Spika, swali langu, ni upi mpango wa Serikali kupanga bajeti maalum kwa ajili ya kundi la vijana ambao wanajishughulisha na shughuli za kilimo na uvuvi ambao wanapata changamoto sana za mabadiliko ya tabianchi? (Makofi)
Name
Laurent Deogratius Luswetula
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Kavuu
Answer
NAIBU WAZIRI WA FEDHA (MHE. LAURENT D. LUSWETULA) K.n.y. WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MIPANGO NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge; kwanza nimpongeze sana kwa namna anavyoendelea kuwatumikia wananchi wa jimbo lake. Ni ukweli kwamba Serikali kwanza imeendelea kuwawezesha vijana kupitia mifuko mingi ya vijana ikiwemo hata juzi mama yetu Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ametoa zaidi ya shilingi bilioni 200 kwenda kwenye Wizara ya Vijana. Hii yote ni kujali kwamba vijana wanafanya kazi na wanapata mitaji ya kuendesha biashara zao.
Mheshimiwa Spika, sisi kama Serikali tuseme tumejipanga vya kutosha kuhakikisha kwamba kundi hili la vijana tunaliwezesha kwa kiasi kikubwa ili lisitetereke kwa namna yoyote, waweze kujiinua kiuchumi kupitia shughuli zao wanazozifanya za kila siku.
Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha.
Name
Neema Peter Majule
Sex
Female
Party
CCM
Constituent
Special Seats
Primary Question
MHE. THOMAS M. KITIMA aliuliza: - Je, lini Serikali itaanza utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050?
Supplementary Question 3
MHE. DKT. NEEMA P. MAJULE: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kumuuliza swali Mheshimiwa Naibu Waziri kuwa tunatamani kushiriki kwenye huu uchumi jumuishi. Ni kwa jinsi gani Serikali imejipanga kuweza kushirikisha watu kutoka vijijini, wanawake, lakini vijana watakavyoshiriki kwenye huu uchumi shirikishi. Tukizingatia sana viashiria ambavyo vitawekwa kupima kwamba makundi haya maalumu nayo yameshiriki, hasa kupitia kutafutiwa masoko, lakini utumiaji teknolojia mpya, umilikishwaji wa ardhi, siyo hivyo tu, ikiwepo upatikanaji wa ajira zikiwepo ajira zilizo rasmi na ajira ambazo siyo rasmi, ili huu uchumi jumuishi ambao utatokea, usitokee kutoka kwa wawekezaji wakubwa, lakini na sisi watu wa chini ikiwepo wanawake tuwe tumeshirikishwa?
Name
Laurent Deogratius Luswetula
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Kavuu
Answer
NAIBU WAZIRI WA FEDHA (MHE. LAURENT D. LUSWETULA) K.n.y. WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MIPANGO NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, nimshukuru sana Dkt. Neema Majule kwa swali lake la nyongeza.
Mheshimiwa Spika, kwanza swali hili ni lazima kidogo turejee katika Dira ya Maendeleo ya miaka 25 ambayo imepita ambayo kwa kiasi kikubwa kwanza imefanya vizuri sana. Ambapo mpaka kufikia mwaka 2024, wastani wa pato la mtu mmoja mmoja limeweza kukua zaidi ya mara tatu, kutoka dola za Kimarekani 453 mpaka dola za Kimarekani 1,227 lakini pia umri wa kuishi nao umeongezeka kutoka wastani wa miaka 51 mpaka miaka 68.
Mheshimiwa Spika, kwa maana hiyo sasa dira hii ya miaka 25 mingine inayokuja, tumejipanga kuhakikisha kwamba makundi yote ya wanawake, vijana, wafanyabiashara, wawekezaji nao wanaenda kuguswa na dira hii ya miaka 25 ambayo tunaenda kuanza nayo tarehe 01 Julai, 2026 mpaka mwaka 2050.
Mheshimiwa Spika, kwa maana hiyo nimhakikishie kabisa Mheshimiwa Mbunge, sisi kama Serikali tumejipanga vya kutosha kuhakikisha kwamba makundi hayo ambayo ameyataja, tunaenda kuyagusa kwa kiasi kikubwa na kuyawezesha kwa kiasi kikubwa kuhakikisha kwamba wanatekeleza shughuli zao za kila siku, ahsante sana.
Name
Agnes Elias Hokororo
Sex
Female
Party
CCM
Constituent
Special Seats
Primary Question
MHE. THOMAS M. KITIMA aliuliza: - Je, lini Serikali itaanza utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050?
Supplementary Question 4
MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Spika, ahsante, kwa kuwa Bunge lako hili ndilo Bunge ambalo litaanza kutekeleza Mpango wa Dira ya Taifa 2050 kwa bajeti hii.
Je, Serikali imejipangaje kuhakikisha inaweka Kitengo cha Ufuatiliaji na Tathmini kwa kuwa malengo ya dira hii ni makubwa kuliko dira tuliyomaliza kuitekeleza? (Makofi)
Name
Laurent Deogratius Luswetula
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Kavuu
Answer
NAIBU WAZIRI WA FEDHA (MHE. LAURENT D. LUSWETULA) K.n.y. WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MIPANGO NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, nimshukuru sana Mheshimiwa Hokororo kwa swali lake nzuri la nyongeza.
Mheshimiwa Spika, kwanza nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, kama Serikali imejipanga vya kutosha na ndiyo maana imekuja na mpango wa e-Delivery, kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi, ambao ni mfumo wa kitaifa wa usimamizi wa mipango na miradi ya maendeleo, hii ni kama database ambayo sasa yenyewe itakuwa inafuatilia. Kwanza miradi yote ya maendeleo ambayo iko katika dira hii, ndio imehifadhiwa hapo, ambayo sasa itakuwa inafuatilia utekelezaji; mradi upi umekamilika, mradi upi umefikia asilimia ngapi, mradi upi unahitaji kitu gani. Ufuatiliaji kwa maana ya planning, monitoring and evaluation, mfumo huu ndio unaenda kumaliza kabisa changamoto hizo.
Mheshimiwa Spika, Wabunge hapa kipindi cha nyuma tulikuwa tunalalamika kidogo kwamba kuna mipango mingine na miradi mingine ambayo inaingizwa kwenye utekelezaji bila mpangilio maalumu. Sasa suluhisho ni mfumo huu wa e-Delivery, ambao unaenda kuhakikisha kwamba miradi yote iliyoidhinishwa ndio inakuwepo hapa. Hiyo mipango yote ikishawekwa italuwa-locked na hakuna mtu ambaye anaweza kuifungua. Lengo na madhumuni tusipate mradi mpya ambao haujaidhinishwa kuweza kuingiwa kwenye mpango kazi wa miradi ambayo tayari imekwisha idhinishwa.
Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha.