Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Devotha Daniel Mburarugaba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. DEVOTHA D. MBURARUGABA aliuliza:- Je, Serikali ipo tayari kutenga dirisha maalumu la mikopo kwa sekta za kipaumbele za kilimo cha kahawa, ufugaji na biashara ndogo ndogo – Kagera?

Supplementary Question 1

MHE. DEVOTHA D. MBURARUGABA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru kwa majibu mazuri ambayo nimeyapata kwa Naibu Waziri, lakini ningependa kuishauri Serikali. Mkoa wa Kagera ni mkoa ambao una wakulima wengi wa kahawa, na wakulima hawa wamekuwa wakivuna kahawa kabla hazijakomaa na wengine kushawishika kuuza nchi jirani. Je, ni lini Serikali itaamua kutoa mikopo ya dharura kwa wananchi hawa ambao wanahusiana na kilimo cha kahawa ili tuweze kutatua changamoto hizi na kuongeza mapato ya Mkoa wa Kagera kupitia AMCOS zao?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaamini wananchi hawa wanaweza wakapata hiyo mikopo ya dharura ili tuwapunguzie adha wakati wa msimu wa kahawa.

Name

Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba kumekuwa na changamoto ya baadhi ya wakulima wa kahawa katika Mkoa wa Kagera kuvuna kahawa kabla haijakomaa vizuri na kuuza ndani pia na nchi jirani. Suala hili linaleta hasara, lakini pia linaathiri ubora wa kahawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali hii imeshaweka utaratibu mzuri. Kwanza kuna fursa ya mikopo ya 10% ambayo wakulima wanaweza wakakopa, wakafanya shughuli zao za kilimo na baada ya mavuno wakarejesha zile fedha kwa utaratibu uliowekwa. Pili, kwa fursa ya mikopo ya kilimo yenye riba nafuu chini ya asilimia tisa inayopatikana katika Mkoa wa Kagera pamoja na nchini kote. Tuna fursa ya mikopo ya Benki ya Maendeleo ya Kilimo na Ushirika na pia tuna Mfuko wa Mikopo ya Pembejeo za Kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nitumie nafasi hii kuwashauri na kuwahamasisha wananchi, wakulima wa kahawa katika Mkoa wa Kagera na mikoa mingine kote nchini kuhakikisha wanatumia fursa za madirisha haya ya mikopo ya dharura ambayo yapo, hayana ukiritimba mkubwa, wapate fedha hizo ili waendeshe shughuli zao za kilimo, na baada ya mavuno, waendelee kurejesha kwa mujibu wa utaratibu.

Name

Agnes Elias Hokororo

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. DEVOTHA D. MBURARUGABA aliuliza:- Je, Serikali ipo tayari kutenga dirisha maalumu la mikopo kwa sekta za kipaumbele za kilimo cha kahawa, ufugaji na biashara ndogo ndogo – Kagera?

Supplementary Question 2

MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kama ilivyo katika swali la msingi, je, Serikali haioni haja ya kuwakopesha wakulima wa korosho kupitia wale wenye stakabadhi ghalani?

Name

Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali inatoa mikopo kwa wakulima wa mazao mbalimbali. Ofisi ya Waziri Mkuu, TAMISEMI, tutashirikiana kwa karibu na Wizara ya Kilimo kuona uwezekano wa shughuli hiyo ya mikopo kwa wakulima wa korosho na stakabadhi ghalani kuweza kutekelezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tumeichukua hoja hiyo, tutaifanyia kazi na wenzetu wa Wizara ya Kilimo ili kurahisisha upatikanaji wa mikopo kwa wakulima wa korosho.

Name

Morris Joseph Makoi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Mjini

Primary Question

MHE. DEVOTHA D. MBURARUGABA aliuliza:- Je, Serikali ipo tayari kutenga dirisha maalumu la mikopo kwa sekta za kipaumbele za kilimo cha kahawa, ufugaji na biashara ndogo ndogo – Kagera?

Supplementary Question 3

MHE. MORRIS J. MAKOI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kuniona. Kama ambavyo swali la msingi limesimama, mikopo ya 10% ambayo inatolewa na Halmashauri, inalenga zaidi vijana na wanawake, lakini wakulima wa kahawa ni makundi mbalimbali. Je, Serikali ina kauli gani kwamba mikopo hiyo sasa ijumuishe wazee pamoja na makundi mengine ambayo hayajatajwa kwenye hiyo sheria ya mikopo?

Name

Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba mikopo ya 10% ni ya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu, lakini hao pia ni moja ya makundi ambayo yanafanya shughuli za kilimo. Kwa hiyo, wanaweza wakanufaika kupitia dirisha hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ipo mikopo mingine ambayo haiendi specifically kwa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu. Kama ambavyo nimesema, mikopo ya kilimo yenye riba nafuu inakopeshwa kwa wakulima wote; mikopo ya Benki ya Maendeleo ya Kilimo, Ushirika, na pia mikopo ya Mfuko wa Mikopo ya Pembejeo za Kilimo. Hizi ni fursa ambazo mkulima yeyote anaweza akapata mkopo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nitumie nafasi hii kuwashauri na kuwahamasisha wakulima ambao hawapo kwenye kundi la wanawake, vijana na watu wenye ulemavu kutumia fursa za madirisha mengine haya ya mikopo.