Bunge la Tanzania
Jamhuri ya Muungano ya Tanzania
Name
Ado Shaibu Ado
Sex
Male
Party
ACT
Constituent
Tunduru Kaskazini
Primary Question
MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA aliuliza: - Je, lini majengo mapya ya Mahakama ya Mwanzo Nanyamba yatajengwa?
Supplementary Question 1
MHE. ADO S. ADO: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali la nyongeza. Katika Wilaya ya Tunduru, Serikali inatekeleza mradi wa ujenzi wa Mahakama ya kisasa ya ngazi ya wilaya. Kwa miezi mitano hivi sasa ujenzi ule umesimama. Swali langu ni kutaka kujua, ni lini Serikali itakamilisha ujenzi wa Mahakama ile ili tuweze kupata huduma inayokusudiwa? Ahsante.
Name
Zainab Athuman Katimba
Sex
Female
Party
CCM
Constituent
Special Seats
Answer
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Ado Shaibu Ado, Wakili Msomi, kwa swali lake zuri lenye lengo la kufuatilia upatikanaji wa haki katika jimbo lake.
Mheshimiwa Spika, ninaomba niendelee tu kumsisitiza Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali ya Awamu ya Sita inatekeleza mradi wa kimkakati kabisa ambao unatokana na mpango wa ujenzi na ukarabati wa majengo ya Mahakama na kwa sasa Mahakama inatekeleza mpango huu wa pili na imetumia wastani wa shilingi bilioni 524.9 kwa ajili ya kuboresha miundombinu ya Mahakama kuanzia katika ngazi ya Mahakama za Mwanzo mpaka Makao Makuu ya Mahakama kama tunavyoliona jengo letu la Judiciary Square.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ninaomba nimpe taarifa Mheshimiwa Mbunge kwamba kwa kuwa Mahakama ya Wilaya ya Tunduru aliyoitaja tayari imeshafikiwa na mpango huu wa pili, na tayari mkandarasi yupo site anaendelea na ujenzi wa Mahakama hiyo, nimhakikishie kwamba ni dhamira ya Mahakama kuhakikisha wananchi wanapata majengo bora ya kisasa kwa ajili ya upatikanaji wa haki. Kwa hiyo, jengo hilo litajengwa na litakamilishwa ili wananchi wake waweze kupata huduma bora kabisa za upatikanaji wa haki katika jimbo lake.
Name
Adonis Alfred Bitegeko
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Muleba Kaskazini
Primary Question
MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA aliuliza: - Je, lini majengo mapya ya Mahakama ya Mwanzo Nanyamba yatajengwa?
Supplementary Question 2
MHE. ADONIS A. BITEGEKO: Mheshimiwa Spika, ninashukuru kwa kuniona na kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Tunashukuru Wilaya ya Muleba tumejengewa Mahakama ya Mwanzo katika Kata ya Izigo, lakini tuna Mahakama ya Wilaya ambayo ina changamoto ya ufinyu wa nafasi, ni chakavu na imejengwa miaka mingi na haiendani na ukubwa wa Wilaya ya Muleba yenye idadi ya watu karibu 650,000 na majimbo mawili ya uchaguzi.
Mheshimiwa Spika, je, Serikali ina mpango gani kujenga jengo jipya la Mahakama ambalo litakidhi mahitaji ya Wilaya ya Muleba?
Name
Zainab Athuman Katimba
Sex
Female
Party
CCM
Constituent
Special Seats
Answer
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, ninampongeza Mheshimiwa Mbunge kwa kufanya ufuatiliaji wa karibu kabisa kuhakikisha kwamba kwenye jimbo lake utoaji wa haki unaendelea kuimarishwa. Ninaomba nimtaarifu Mheshimiwa Mbunge kama nilivyotangulia kusema kwamba, Mahakama kwa wakati huu inatekeleza mpango wa ujenzi na ukarabati wa miundombinu, mpango wa pili ambao umegharibu wastani wa bilioni 524.9.
Mheshimiwa Spika, mpango huu haujikiti tu kwenye kuboresha miundombinu kwa maana ya majengo ya Mahakama pekee, lakini pia hata katika kujenga mifumo ya kidijiti. Ndiyo maana mtaona kwa wakati huu mwananchi anaweza akafungua shauri kidijiti kupitia mfumo wa Mahakama wa ECMS, pia mwananchi anaweza akahudhuria shauri lake kupitia mifumo ya kidijiti kupitia Mahakama Mtandao.
Mheshimiwa Spika, pia kuna mifumo mingi ambayo inamwezesha mwananchi kupunguza gharama kusafiri kufika Mahakamani na kupata huduma zilizo bora na za kisasa. Kwa hiyo, ninaomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Mahakama itafika na kuhakikisha kwamba jengo katika Wilaya hii ya Muleba inakuwa ni bora na la kisasa kwa sababu ndiyo mpango uliopo na ndiyo mpango unaotekelezwa.
Mheshimiwa Spika, jengo litajengwa na wananchi wa Mheshimiwa Mbunge katika Jimbo hili la Muleba watapata miundombinu iliyo bora katika upatikanaji wa haki.
Name
Edward Olelekaita Kisau
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Kiteto
Primary Question
MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA aliuliza: - Je, lini majengo mapya ya Mahakama ya Mwanzo Nanyamba yatajengwa?
Supplementary Question 3
MHE. EDWARD O. KISAU: Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Kiteto ina Mahakama kongwe sana ya muda mrefu. Tumeshaleta maombi na tukaambiwa ipo kwenye bajeti ya 2024/2025. Nini kauli ya Serikali kuhusu majibu ya ujenzi wa Mahakama ya Wilaya ya kisasa? Ahsante sana.
Name
Zainab Athuman Katimba
Sex
Female
Party
CCM
Constituent
Special Seats
Answer
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, ninampongeza Mheshimiwa Olelekaita Edward ambaye amekuwa akifanya ufuatiliaji wa mambo mengi sana katika sekta hii muhimu ya sheria.
Mheshimiwa Spika, kuhusiana na swali lake kuhusu ujenzi wa Mahakama hii ya Wilaya ya Kiteto, kama nilivyotangulia kusema, kwa wakati huu Mahakama inatekeleza mpango wa ujenzi na ukarabati wa miundombinu ya Mahakama ikiwemo Mahakama za Wilaya. Mahakama hii ya Wilaya ya Kiteto ipo katika mpango huu wa pili na tayari tenda ilishatangazwa kwa ajili ya kumpata mkandarasi kwa ajili ya ujenzi wa Mahakama hii.
Mheshimiwa Spika, kwa wakati huu bado majadiliano yanaendelea kwa ajili ya kusaini mkataba ili sasa ujenzi wa Mahakama ya kisasa kabisa uweze kuanza na wananchi wa Mheshimiwa Mbunge wapate majengo mazuri kwa ajili ya huduma za Kimahakama.
Copyright © Bunge Polis 2026. All Rights Reserved